ASASI ZA KIRAIA ZATOA WITO WA HAKI ZENYE MIZANI KATIKA KESI ZA UKATILI ZANZIBAR
Asasi hizo zinasisitiza kuwa, tukio hili halipaswi kutazamwa kwa
kumlenga mhusika mmoja pekee, bali kwa kuchambua mchango wa mifumo, mahusiano
ya kifamilia na wajibu wa wahusika wote waliokuwepo katika mazingira
yaliyopelekea tukio hilo.
Aidha, asasi hizo ambazo ni Jumuiya ya Wanawake wenye Ulemavu
Zanzibar (JUWAUZA), Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA), Jumuiya
ya Mazingira, Jinsia na Utetezi Pemba (PEGAO) na Chama cha Waandishi wa Habari
Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ) zinaona umuhimu wa mamlaka husika
kuangalia kwa kina nafasi na mchango wa mume katika tukio hili, ikiwemo wajibu
wake wa kisheria, kijamii na kimaadili katika kusimamia familia yake na kuzuia
mazingira yanayoweza kuchochea migogoro na hatimaye ukatili. Haki ya kweli
inapaswa kuzingatia wajibu wa kila mhusika, bila upendeleo wa kijinsia au
misingi ya kimfumo dume.
Vilevile, asasi hizo zinaeleza wasiwasi wao kuhusu mwenendo wa
haki katika kesi za ukatili wa kijinsia, hasa mauaji na vipigo dhidi ya
wanawake, ambapo kesi nyingi zimekuwa zikichukua muda mrefu bila kupatiwa
hukumu.
Kwa mujibu wa rikodi za TAMWA ZNZ, matukio 33 ya mauwaji ya wanawake na watoto yameripotiwa (wanawake 27 na Watoto 6) tokea mwishoni mwa mwaka 2016 hadi mwanzoni mwa mwaka 2026.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka
Zanzibar (DPP) imeeleza kuwa jumla ya kesi sita zilipatiwa hatia za sheria
ikiwemo kuachiwa huru watuhumiwa (kesi 2), kufungwa kwa jalada (1), kunyongwa
hadi kufa (2) na kifungo (1). Ambapo kesi nyengine sita (6) zimeelezwa kuwa
zipo mahakamani zinaendelea na nyengine zimekuwa ngumu kupatikana kwa taarifa
kutokana na kukosekana kwa namba za kesi kutoka vituo vya polisi na mahakamani
pamoja na kukosekana kwa majina ya washitakiwa.
JUWAUZA, PEGAO, ZAFELA na TAMWA - ZNZ zinatoa wito kwa vyombo vya
haki kuhakikisha kuwa kasi na uzito uliotumika katika kesi hii utumike pia
katika kesi nyingine zote za ukatili dhidi ya wanawake na watoto bila ubaguzi
wa mhusika au mazingira ya tukio.
Kwa kuzingatia muktadha wa kijamii na kidini Zanzibar, asasi hizo
zinakumbusha kuwa katika dini ya Kiislamu, ndoa ya wake zaidi ya mmoja ina
masharti ya kufanya haki, uadilifu, uwajibikaji na ulinzi kwa wake na watoto.
Hivyo, tunatoa wito kwa viongozi wa dini kuendelea kutoa elimu sahihi kwa
jamii, hususan kwa wanaume, kuhusu wajibu wao wa kusimamia haki, amani na
ustawi wa familia zao.
Sambamba na hilo, JUWAUZA, PEGAO, ZAFELA na TAMWA - ZNZ
zinaishauri Serikali kuangalia uwezekano wa kuweka au kuimarisha mifumo na
taratibu zitakazosaidia kudhibiti ndoa za wake wengi zisizo na maandalizi ya
kutosha, ili kuzuia migogoro ya kifamilia na vitendo vya ukatili vinavyoathiri
wanawake na watoto.
Pia zinawaasa wanawake na jamii kwa ujumla kutambua madhara
makubwa ya maamuzi yanayochochewa na hasira, kwani mara nyingi huzaa hasara
kubwa kwa wahusika na familia zao. Tukio hili limeacha watoto wanaohitaji
malezi, ulinzi na msaada, hali inayoibua maswali mengi ya kijamii yanayohitaji
majibu ya pamoja.
JUWAUZA, PEGAO, ZAFELA na TAMWA - ZNZ zinasisitiza kuwa hatua
stahiki za kisheria zinapaswa kuchukuliwa kwa wahusika wote katika mazingira
yanayopelekea matukio ya ukatili, ili kuhakikisha haki inatendeka kwa pande
zote mbili bila ya kuupa nafasi mfumo dume.
Imetolewa na:
JUWAUZA, PEGAO, ZAFELA na TAMWA
ZANZIBAR

Post a Comment