TAMWA-ZNZ, yazindua Tuzo ya uwiano wa kijinsia kwa Vyombo vya Habari: "Kalamu Yangu, Mchango Wangu kwa Wanawake."

NA MARYAM NASSOR
JUMUIYA ya
Wanawake wenye Ulemavu Zanzibar (JUWAUZA), Jumuiya ya Wanasheria Wanawake
Zanzibar (ZAFELA) Jumuiya ya Mazingira, Jinsia na Utetezi Pemba (PEGAO), na
Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA -ZNZ) kwa
mashirikiano na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar (WEMA wametangaza
rasmi uzinduzi wa Tuzo ya uwiano wa kijinsia kwa mwaka 2025/2026 yenye ujumbe
unaosema "Kalamu Yangu, Mchango Wangu kwa Wanawake."
Akizungumza na
vyombo vya habari, Tunguu mkoa wa kusini Unguja Mkurugenzi wa Chama hicho
Nairat Ali Abdullah amesema tunzo hiyo itatambua waandishi wa habari na
watengeneza maudhui (content creators) wa Zanzibar wanaoandika na kuandaa
maudhui ya kina yanayoangazia mafanikio, changamoto na michango ya wanawake
katika uongozi pamoja na kutatambua wahamasishaji jamii waliofanya vizuri
katika ngazi za wilaya kwa namna wanavyoshiriki kikamilifu katika kukuza usawa
wa kijinsia na kuhamasisha jamii kupitia kazi zao.
Amesema ,Malengo
yao Kupitia tuzo hiyo, JUWAUZA, PEGAO, ZAFELA, WEMA na TAMWA
ZNZ, wanalenga:
- Kuhamasisha uandishi na utengenezaji wa maudhui
unaokuza usawa wa kijinsia.
- Kukuza na kuimarisha uongozi wa wanawake katika
sekta ya elimu.
- Kukuza sauti za wanawake katika uongozi na maamuzi kwa ujumla
- Kutambua mchango wa waandishi, wahamasishaji
jamii na watengeneza maudhui katika kuleta mabadiliko ya kijamii.
- Kuimarisha uhamasishaji wa jamii kuhusu umuhimu
wa wanawake kushiriki katika uongozi na michakato ya kidemokrasia.
Utambuzi wa
Waandishi, Wahamasishaji jamii na Watengenezaji wa maudhui
Tuzo hii
itahusisha kazi zilizotolewa katika makundi yafuatayo:
- Uandishi wa habari za makala katika magazeti.
- Vipindi vya redio.
- Vipindi vya televisheni.
- Makala au kampeni za mitandao ya kijamii.
Vigezo Muhimu vya
Kuzingatia kwa waandishi wa Habari
· Ubora wa kazi
iliyowasilishwa.
· Upekee wa mada.
· Umuhimu wa
kuzingatia uwiano sawa wa jinsia.
· Vyanzo vingi vya
habari vilivyojitawanya.
· Ubunifu wa mada
husika.
· Matokeo baada ya
kutoka kwa habari au kampeni hiyo (impact).
· Uwasilishaji wa
mada husika.
· Mpangilio wa
mada.
· Ufasaha na
mtiririko wa lugha.
· Kuzingatia
maadili ya uandishi wa habari.
· Uweledi na
matumizi ya takwimu.
Kipindi cha Redio
na Televisheni kisizidi dakika 30, na sauti pamoja na picha ziwe katika ubora
unaostahiki.
Kazi
zinazowasilishwa lazima ziwe zimechapishwa au kurushwa hewani katika kipindi
cha kuanzia Januari 1 hadi Disemba 31, 2025.
Mchakato wa
Uwasilishaji na Tathmini:
Maombi
yamefunguliwa leo na kazi zitaendelea kupokelewa hadi tarehe 13 Aprili,
2026.
Kazi zinaweza
kuwasilishwa moja kwa moja katika Ofisi za TAMWA ZNZ zilizopo Tunguu - Unguja
na Mkanjuni Chakechake - Pemba, au kupitia barua pepe ya info@tamwaznz.or.tz
pamoja na kiungo kitakachotumwa kwenye mitandao ya kijamii.
Vigezo muhimu vya kuzingatia kwa
watengenezaji wa maudhui (Content Creators).
- Ubunifu na uhalisia wa maudhui
- Uelewa wa mada na
kufikisha ujumbe kwa usahihi.
- Ubora wa
uwasilishaji maudhui kwa kutumia lugha, picha au video.
- Uwezo wa maudhui kuhamasisha
uelewa au mabadiliko chanya kwa jamii.
- Kuhakikisha maudhui yanafuata
maadili na yanatoa taarifa sahihi.
- Maudhui yaliyosambaa na kuwafikia
watu wengi.
Vigezo Muhimu vya Kuzingatia kwa
wahamasishaji jamii (Citizen Brigades)
- Kwa upande wa wahamasishaji wa jamii
tunaowatumia kuhamasisha jamii kuhusu masuala ya wanawake na uongozi
katika ngazi za chini, tuzo itatolewa kwa wilaya mbili zitakazojitokeza
kwa utendaji bora zaidi, wilaya moja kutoka Unguja na wilaya moja kutoka
Pemba.
- Tathmini ya utendaji wao itazingatia kiwango
cha juhudi za uhamasishaji walizozifanya, kiwango cha ushiriki wa jamii,
- Ubunifu wa mbinu walizotumia katika
kufikisha ujumbe, pamoja na
- Matokeo chanya yaliyojitokeza katika
jamii kutokana na shughuli hizo.
- Uwasilishaji wa ripoti za kazi zao kwa wakati.
- Majaji wa kazi:
- Katika kuhakikisha malengo ya tunzo hizi,
kutakuwa na jopo la majaji ambalo litakuwa na watu wenye sifa za ujuzi,
uzoefu, usawa na uadilifu kutoka katika maeneo yote yanayoangaliwa.
Washindi wote
watatambuliwa na kupewa tuzo siku ya tarehe 02 Mwezi Mei 2026, shughuli ambayo
itawashirikisha pia wadau mbali mbali wa wanawake na uongozi.
Aidha amesema
kuwa, Huu ni msimu wa tano wa utoaji wa Tuzo hizi kupitia grogram ya kuwajengea
Wanawake uwezo katika Uongozi (SWIL) inayotekelezwa kwa mashirikiano na Ubalozi
wa Norway (RNE). Tuzo hizi ni mwendelezo wa jitihada za kuongeza ushiriki wa
wanawake katika uongozi na kuimarisha ushiriki wa kidemokrasia Zanzibar.
Mpaka sasa, jumla
ya waandishi wa habari 53 pamoja na vyombo vya habari vitatu vimetambuliwa kwa
kuandika na kurusha maudhui yanayochangia kuongeza ushiriki wa wanawake katika
uongozi katika kipindi cha kuanzia mwaka 2021 hadi 2024.
Kwa maelezo
zaidi, tafadhali wasiliana nasi kupitia info@tamwaznz.or.tz au ngalapi@tamwaznz.or.tz
Post a Comment