TAMWA ZNZ, CFP NA CFI YAZINDUA TUNZO YA UANDISHI WA HABARI ZA TABIANCHI ZA 'COMMUNITY FORESTS'


NA MWANDISHI WETU 

CHAMA cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania - Zanzibar (TAMWA ZNZ) kwa kushirikiana na Community Forests Pemba (CFP) na Community Forests International (CFI) kupitia mradi wa Zanzibar Women’s Leadership in Adaptation (ZanzAdapt), kina furaha kuwatangazia rasmi uzinduzi wa Tuzo “Uandishi wa Habari za Tabianchi za ‘Community Forests. Yenye kaulimbiu isemayo:“Kupaza Sauti za Wanawake katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi”.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ufunguzi wa Tuzo hizo, huko katika ukumbi wa  Chama hicho Tunguu , Mkurugenzi wa  ( CFP ) Mbarouk Mussa Omar  amesema  lengo la tunzo hizo ni  kutatambua mchango wa waandishi wa habari na vyombo vya habari Zanzibar vinavyoandika, kurusha na kusambaza habari zinazoonesha mchango wa wanawake na uongozi katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, hususan katika eneo la mikoko, kilimo mseto himilivu cha tabianchi (climate-smart agriculture) na kukuza usawa wa kijinsia kupitia kazi zao.

Amesema kuwa, Kupitia tuzo hizo, TAMWA ZNZ, Community Forests Pemba na Community Forests international zinalenga,  Kukuza uandishi wa habari unaoonyesha uongozi wa wanawake katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Amesema  lengo jengine la tunzo hizo ni Kutambua mchango wa waandishi wa habari mahiri wanaoandika habari zinazohusu wanawake na uongozi kwenye masuala ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi

  • Kuhamasisha uandishi wa habari unaozingatia usawa wa kijinsia, ushahidi wa kisayansi na hadithi za mabadiliko chanya kutoka ngazi ya jamii.
  • Kuongeza uelewa wa jamii kuhusu mchango na uongozi wa wanawake katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi Zanzibar.
  • Kuweka mazingira ya ushindani kwa waandishi wa habari kuandika habari zenye ubora na athari chanya kuhusu wanawake na uongozi na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa nini Tuzo hizi ni Muhimu:

 Nae, Manager wa Mawasiliano Kitengo cha Habari TAMWA ZNZ, Sophia Ngalapi amesema ,Licha ya wanawake kuwa mstari wa mbele na kutoa mchango mkubwa katika shughuli za kilimo-misitu (agroforestry), uhifadhi wa mikoko, na mikakati mingine ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kutumia mbinu za asili, lakini uongozi na mchango wao bado hauonekani vya kutosha katika vyombo vya habari na kwa jamii.

 Amesema kuwa, Uwakilishi mdogo wa wanawake katika simulizi za vyombo vya habari haupunguzi tu nafasi yao ya kushiriki na kuongoza, bali hupunguza mwonekano wa mikakati bora ya jamii katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Aidha amesema kuwa, Utafiti uliofanywa na mradi wa ZanAdapt Juni 2024 ulibaini kwamba, kati ya habari 4,548 kutoka vyombo vya habari mbalimbali ni asilimia 1.1 tu ya habari zilizojumuisha sauti za wanawake na wasichana, na asilimia 0.4 pekee zilizoonyesha wanawake kama viongozi katika muktadha wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Mradi ZanzAdapt, unaotekelezwa na Community Forests International na Community Forests Pemba kwa ushirikiano na TAMWA Zanzibar, unalenga kuziba pengo hili kwa kuhamasisha uandishi wa habari unaozingatia usawa wa kijinsia na kutambua uongozi wa wanawake katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Ili kukabiliana na changamoto hii, Tuzo ya ““Uandishi wa Habari za Tabianchi za ‘Community Forests”.Yenye kaulimbiu isemayo “Kupaza Sauti za Wanawake katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi”. imeanzishwa kutambua mchango wa vyombo vya habari na kuhamasisha waandishi wa habari kuongeza juhudi katika kuandika habari za wanawake na uongozi katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi Zanzibar.

Kupitia mradi wa ZanzAdapt, waandishi wa habari 30 (20 Unguja na 10 Pemba) pamoja na wahariri 20 wamejengewa uwezo  kitaaluma ili waweze kuandika habari kwa ubora, ambapo wameweza  kuandika habari zaidi 242 zinazozingatia uongozi wa wanawake katika kukabiliana na tabianchi. Tuzo hii inakuja kuthamini, kuendeleza na kuongeza juhudi hizo.

Tunzo hii itahusisha kazi zilizotolewa na waaandishi wa habari katika vyombo vya habari vya aina nne (4) kama ifuatavyo:). 

1.    Uandishi wa makala katika magazeti (feature articles).

2.    Uandishi wa habari wa vipindi katika redio (radio program).

3.    Uandishi wa habari katika Televisheni (TV program).

4.    Uandishi wa makala katika mitandao ya kijamii (feature articles in social media)

Kazi zote lazima zionyeshe masuala ya mabadiliko ya tabianchi Zanzibar na ushiriki, sauti na uongozi wa wanawake Zanzibar.

Tuzo maalumu: Pia kutakuwa na tuzo maalum nne ambazo ni:  

1.    Kutambua chombo cha habari kilichoonyesha uwajibikaji zaidi katika masuala ya wanawake na uongozi katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.  Hivyo vigezo vitakavyotumika ni kuangalia chombo cha habari kilichoongoza kuzalisha habari zenye ubora zilizorushwa au kuchapisha zinazohusu uongozi wa wanawake katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kuonyesha jinsi kinavyolenga kuenzi na kuimarisha sauti za wanawake katika masuala ya tabianchi na uwiano wa kijinsia kati ya wafanyakazi.

 

2.    Tuzo ya mwandishi wa habari kijana wa habari za mabadiliko ya tabianchi (miaka 18-30). Vigezo kwamba mwandishi yoyote kijana, mwenye umri kuanzia miaka 18 hadi 30 anayefanya kazi katika chombo cha habari cha gazeti,television, redio na mitandao ya kijamii ambae ameandika habari inayohusu masuala ya wanawake na uongozi katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

 

3.    Tuzo ya uandishi wa habari wa mitandao ya kijamii. Vigezo ni kwamba kazi iwe imeangaliwa na watu wengi zaidi.

 

4.     Tuzo kwa habari iliyoangazia kwa ukubwa nafasi ya wanawake na uongozi katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Vigezo muhimu vya kuzingatia:

·       Habari za Wanawake na uongozi katika mabadiliko ya tabianchi

·       Umuhimu wa kuzingatia uwiano sawa wa jinsia
Usahihi wa taarifa na unaozingatia maadili ya uandishi wa habari

·       Ubora wa uandishi wa habari kwa picha (Visual Journalism Quality)

·       Simulizi ya kipekee ya mada husika

·       Ubunifu, uchunguzi bora wa mada

·       Ufasaha na mtiririko wa lugha

·       Ubora katika utayarishaji, sauti na uwasilishaji wa mada

·       Ushawishi na ushirikishwaji wa hadhiara mitandaoni

aKipindi cha Redio na Television kisizidi dakika 30 na pia sauti na picha ziwe katika ubora unaostahiki.

Kwa Vyombo vya Habari Pekee:

·       Dhamira ya chombo cha habari katika mabadiliko ya tabianchi

·       Program zenye ubunifu na ushirikishwaji wa jamii

Vigezo kwa vyombo cha habari:

Chombo cha habari kinapaswa kuwasilisha andiko/maelezo ya kurasa mbili ikionyesha idadi na ubora wa habari au makala zilizochapishwa au kurushwa zinazohusu uongozi wa wanawake katika mabadiliko ya tabianchi, kuonyesha jinsi kinavyolenga kuenzi na kuimarisha sauti za wanawake katika masuala ya tabianchi, uwepo wa mwandishi wa habari maalum anayeshughulikia masuala ya mazingira na tabianchi miongoni mwa wafanyakazi wake, na uwiano wa kijinsia kati ya wafanyakazi. Vilevile, vyombo vya habari vinaweza kuweka taarifa nyingine yoyote wanayoiona inafaa ili kuimarisha maombi yao.

Mchakato wa Uwasilishaji na vigezo vya tathmini. 

Dirisha la kupokea kazi liko wazi kwa waandishi wa habari wa Unguja na Pemba kutoka vyombo vya habari mbalimbali kutuma kazi zao, ikiwemo magazeti, televisheni, redio, na mitandao ya kijamii. Kazi zitakazopokelewa ni zile zilizochapishwa au kurushwa HEWANI kuanzia tarehe 01 Juni 2024 hadi tarehe 31 Disemba 2025, na lazima zihusishe:

 

  • Masuala ya mabadiliko ya tabianchi Zanzibar;
  • Wanawake na uongozi katika mabadiliko ya tabianchi Zanzibar

 

Maombi yamefunguliwa leo na kazi zitaanza kupokelewa kwa muda wa siku 21 kuanzia tarehe ya leo hadi tarehe 23 Januari hadi tarehe 14 Feburuari, 2026.

Waandishi wa habari mtatakiwa kuwasilisha kazi mbili (2) ambazo zimezalishwa, kuchapishwa na kurushwa HEWANI kwa kipindi kilichotajwa hapo juu kupitia kiungo/link itakayotumwa kwenye mitandao ya kijamii au kuleta moja kwa moja Ofisi za TAMWA ZNZ zilizopo Tunguu, Unguja na Mkanjuni Chakechake Pemba.

Jopo la majaji likiwa na wataalamu wa uandishi wa habari na jinsia,pamoja na wataalamu wa masuala ya mabadiliko ya tabianchi  litapitia kazi zote zilizowasilishwa kwa umakini mkubwa mara tu baada ya kufungwa kwa zoezi la uwasilishaji na ukusanyaji kazi hizo.

Kazi zote zitakazowasilishwa zitapitia uhakiki wa awali wa jumla na majaji ili kuhakikisha zinakidhi vigezo vya msingi vifuatavyo:

1.    Lugha ya kazi iwe Kiswahili au Kiingereza.

2.    Mwandishi wa habari awe na umri wa miaka 18 au zaidi.

3.    Kazi iwe imechapishwa ndani ya kipindi kinachokubalika kwa mujibu wa kanuni za tuzo (kuanzia tarehe 1 Juni, 2024 hadi tarehe 31 Disemba, 2025).

4.    Kazi ijikite katika masuala ya mabadiliko ya tabianchi Zanzibar.

5.    Kazi ionyeshe uongozi wa wanawake wa Kizanzibari.

6.    Kazi iwe katika moja ya makundi ya vyombo vya habari yaliyobainishwa.

7.    Mwandishi wa habari au chombo cha habari kiwe na makao yake Zanzibar.

8.    Kazi ikidhi vigezo vyote vya majaji.

Tarehe ya Tuzo:

Hafla ya utoaji wa tuzo inatarajiwa kufanyika tarehe 28 Machi 2026, kuanzia saa moja usiku katika hafla itakayowakutanisha waandishi wa habari, wahariri wa vyombo vya habari, wamiliki wa vyombo vya habari, taasisi za kiserikali, zisizo za kiserikali, za kimataifa na wanajamii.

Hitimisho:

TAMWA ZNZ, Community Forest Pemba na Community Forest International tunawakaribisha waandishi wa habari na vyombo vya habari vya Zanzibar kushiriki kikamilifu katika tuzo hizi, tuzo hizi ni jukwaa muhimu la kuonesha nguvu ya uandishi wa habari katika kuleta mabadiliko ya kijamii na kimazingira kwa kuzingatia usawa wa kijinsia na sauti za wanawake na uongozi katika kukabiliana namabadiliko ya tabianchi ili kujenga uelewa kwa jamii na kuleta mabadiliko chanya.

Tuzo hizi ambazo ni mara ya kwanza kufanyika zimeandaliwa kupitia mradi wa Zanzibar Women’s Leadership in Adaptation (ZanzAdapt) kwa mashirikiano na Serikali ya Canada.

Kwa maelezo zaidi, tafadhali wasiliana nasi kupitia:  info@tamwaznz.or.tz & ngalapi@tamwaznz.or.tz.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

No comments

Powered by Blogger.