WANUFAIKA WA ZANZ ADAPT WATAKIWA KUANZISHA VIKUNDI VYA KUCHUKUA HATUA KATIKA SHEHIA ZAO
NA MARYAM NASSOR
Mkurugenzi Mtendaji wa Community Forest
Pemba (CFP), Mbarouk Mussa
Omar , amewataka wahamasishaji jamii ambao ni wanufaika wa mradi wa Kukabiliana
na Mabadiliko ya Tabianchi (Zanz Adapt ) kuanzisha vikundi vya kuchukua
hatua katika shehia zao kwa lengo la kutatua changamoto zinazoikumba jamii.
Akizungumza katika warsha ya siku mbili iliyofanyika Tunguu,katika ukumbi wa Chama cha Waandishi wa
Habari Wanawake Tanzania ( TAMWA ZNZ) ,amesema
lengo la mafunzo hayo ni kuwawezesha wahamasishaji jamii kuanzisha vikundi vitakavyoweza kuchukua hatua mbalimbali za
kutatua changamoto zinazotokea katika
maeneo yao.
Akieleza baadhi ya changamoto zinazoikumba jamii ni Pamoja na
umiliki mdogo wa ardhi kwa wanawake, uharibifu wa mikoko na usawa wa kijinsia
katika kuleta maendeleo.
Amesema, kupitia vikundi hivyo vitasaidia katika kuelimisha
jamii , kupata uwelewa na kuchukua hatua
stahiki.
“Lengo la mafunzo haya ni kuwajengea uwezo wana vikundi ili kusaidia
kuhamasisha ushiriki wa jamii katika utunzaji wa mikoko, kwa mashirikiano
makubwa na Wizara ya Kilimo na Uvuvi,” alisema.
Kwa upande wake, Mkuugenzi mwendeshaji wa Community Forest Pemba (CFP), Omar
Mtarika amesema kuanzishwa kwa vikundi hivyo kutaimarisha ushirikiano na
viongozi wa shehia na viongozi wa dini katika kuhamasisha na kulinda rasilimali
za mikoko na ardhi.
Ameongeza kuwa ,vikundi hivyo vitafanya kazi kwa karibu na idara za Serikali
ili kuharakisha maendeleo ya kijamii na ya Serikali kwa ujumla.
“Tumechagua watu kutoka rika mbalimbali vijana, wazee,
wanawake na viongozi wa dini wenye ushawishi katika jamii ili kuleta ufanisi
katika majukumu yetu,” amesema.
Naye Emmy Auma, kutoka Taasisi ya ( AFRICA CSID) amesema
ni muhimu kwa jamii kufanya kazi kwa pamoja ili kufanikisha usawa wa kijinsia,
huku akisisitiza kuwa kazi hiyo ni ngumu na inahitaji kujitolea.
Amefafanua kuwa, AFRICA CSID kwa
kushirikiana na Community Forest Pemba (CFP) wamefanya
uchambuzi wa matatizo na kuwajengea
uwezo wanajamii wenye ushawishi ili kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya
tabianchi na usawa wa kijinsia.
“Kufanya kazi na jamii si rahisi kunahitaji kujitoa kwa sababu changamoto ni
nyingi na matunda yake huchukua muda kuonekana,” amesema.
Nao washiriki wa mafunzo hayo, kutoka Shehia ya Uzi na
Ng’ambwa, Maryam Juma Chumu na Issa Mohmaed Issa, wamesema
mafunzo hayo yataleta ufumbuzi wa matatizo yanayoikumba jamii yao kwani sasa
wataanza kuchukua hatua madhubuti.
Wameeleza kuwa jamii zao zinakabiliwa na migogoro mbalimbali ikiwemo masuala ya
usawa wa kijinsia na uharibifu wa mazingira.
Mafunzo hayo ya siku mbili yameandaliwa na Community
Forest Pemba (CFP) kwa kushirikiana na Community Forest
Intenational ( CFI) , yakihusisha washiriki kutoka shehia za Bungi, Unguja
Ukuu, Uzi na Ng’ambwa, kwa lengo la kuanzisha vikundi vya kuchukua hatua za
kijamii (Community Action Groups) vitakavyohamasisha umiliki wa ardhi, upandaji wa mikoko na usawa wa kijinsia katika
uhifadhi wa mazingira.




Post a Comment