WADAU WA HABARI WAISHAURI MAMLAKA KUZINGATIA MAPENDEKEZO YA WADAU KUHUSU MSWADA WA SHERIA YA HUDUMA ZA HABARI ZANZIBAR.



NA MARYAM NASSOR

Taasisi za kihabari, wadau wa haki za binadamu pamoja na waandishi wa habari wabobevu Zanzibar zimeishauri Wizara ya Habari kuzingatia kikamilifu mapendekezo yaliyotolewa na wadau kuhusu Mswada wa Sheria Mpya ya Huduma za Habari Zanzibar, wakisisitiza kuwa maoni hayo ni muhimu katika kulinda uhuru wa vyombo vya habari na haki ya wananchi kupata taarifa.

Wadau hao wameeleza kuwa kupuuza mapendekezo hayo kutazidi kudhoofisha mazingira ya kazi za kihabari na kuhatarisha misingi ya uwazi, uwajibikaji na demokrasia. Hivyo, wameitaka Wizara ya Habari kuendelea na mashauriano ya wazi na shirikishi ili kuhakikisha upatikanaji wa sheria mpya ya habari inayokidhi vigezo muhimu vya kukuza na kuendeleza tasnia ya habari Zanzibar.

Wamesema kauli ya Mheshimiwa Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Dkt. Riziki Pembe Juma aliyoitoa katika Mkutano na wadau wa habari mnamo tarehe 28 Januari 2026 kwamba Wizara yake imejizatiti kuendelea na mchakato wa mabadiliko ya sheria mpya ya huduma za habari imetoa mwanga wa matumaini kwa tasnia nzima ya habari kwavile hicho ni   kilio cha muda mrefu.

Hata hivyo, wadau hao wameeleza wasiwasi wao kuhusu mchakato wa marekebisho ya sheria ya hiyo ulioanza tangu mwaka 2008, wakibainisha kuwa hadi sasa bado haijawekwa wazi ni mabadiliko gani mahsusi yamefanyika na kama mapungufu yaliyoainishwa na wadau kwa kipindi chote yamezingatiwa ipasavyo. Wamesema kuwa mchakato huo umekumbwa na changamoto za ushirikishwaji hafifu, ukosefu wa taarifa za mara kwa mara, pamoja na kutokuwepo kwa mrejesho wa wazi juu ya mapendekezo yaliyotolewa, hali inayozua mashaka kuhusu mwelekeo na dhamira ya muswada huo.

Aidha, wadau wameeleza kuwa sheria zinazotumika kwa sasa, hususan Sheria ya Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu Na. 5 ya mwaka 1988 pamoja na Sheria ya Tume ya Utangazaji Zanzibar Na. 7 ya mwaka 1997, zimepitwa na wakati na zinatoa mamlaka makubwa kwa Viongozi wa Serikali na kuruhusu vyombo vya dola kuingilia shughuli za kihabari. Wakitoa mfano wamesema, Waziri wa habari amepewa mamlaka ya kufungia gazeti na kutoa au kusitisha leseni kwa chombo cha Habari kazi ambayo inapaswa kufanywa na Chombo cha Habari kinachojitegemea na ikishindwa suluhu basi malalamiko yote yapelekwe Mahakamani. Pia sheria hizo hazitoi ulinzi kwa waandishi wa Habari na haki ya kupata taarifa hali ambayo imeathiri uhuru wa kujieleza, usalama wa waandishi wa habari na uwezo wa vyombo vya habari kutekeleza wajibu wao wa kuuhabarisha umma kwa weledi na uwajibikaji.

Wadau pia wameonesha wasiwasi wao kuwa mswaada huo umetia maanani mabadiliko makubwa ya teknolojia ikiwemo matumizi ya majukwaa ya kidijitali, uandishi wa habari mtandaoni, maendeleo ya akili mnemba (Artificial Intelligence) ambayo yanazidi kuonesha kuwa sheria za Habari zimepitwa na wakati katika maeneo mengi yakiwemo ya kisiasa, kijamii, kiuchumi na kiteknolojia.

Imane Duwe Mkufunzi toka chuo kikuu cha Zanzibar SUZA alisema kuwa “Sheria zilizopo kwa sasa zimepitwa na wakati na zinatoa mamlaka makubwa kwa vyombo vya dola bila ulinzi wa kutosha kwa waandishi wa habari, jambo linalohatarisha uhuru wa kujieleza na usalama wao.”

Salim Said Salim mwandishi mkongwe na mkufunzi katika masuala ya habari alisema “Hatuhitaji tena ahadi; tunahitaji sheria itakayolinda uhuru wetu, usalama wetu na haki ya wananchi kupata taarifa bila hofu.” Aliongeza kuwa katika kipindi cha hivi karibuni kumepitishwa zaidi ya sheria 285 hivyo vitendo vinahitajika katika kukamiisha sheria nzuri ya habari.

Jabir Idriss mwandishi mwandamizi alisema “Sheria za sasa zimepitwa na wakati na zimekuwa chombo cha kutunyamazisha badala ya kutulinda kama waandishi wa habari.”

Maryam Hamdan mwandishi mkongwe ambaye ametumikia tasnia ya habari kwa muda mrefu amesema kuwa sheria za habari ni muhimu katika kuimarisha kada ya habari na hivyo kilio cha muda mrefu cha waandishi wa habari kunahitajika hatua za vitendo katika kuimarisha kada ya habari na mojawapo ni kuwa na sheria rafiki na nzuri kwa waandishi wa habari.

Katika ripoti ya kamati ya wataalamu wa habari (ZAMECO) ya mwaka jana 2025, ambayo imetolewa hivi karibuni imeonesha kuwa sheria za habari zimekuwa moja ya vikwazo katika kuimarisha uhuru wa habari lakini waandishi wamekuwa wanashindwa kufanya kazi zao kwa weledi na umahiri.

Pamoja na changamoto hizo, wadau wa habari wameeleza kuridhishwa kwao na hatua ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kupitia Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Mheshimiwa Dkt. Riziki Pembe Juma, ya kuandaa mkutano wa pamoja na wadau wa habari kwa ajili ya kujadili masuala ya tasnia ya habari, wakieleza kuwa kwa muda mrefu mikutano ya aina hiyo ilikuwa nadra kufanyika.

Wadau pia wamesisitiza umuhimu wa utekelezaji wa ahadi ya kuuwasilisha Mswada wa Sheria ya Huduma za Habari Zanzibar katika kikao cha Baraza la Wawakilishi (BLW) cha mwezi Septemba 2026, wakieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuimarisha mazingira huru, salama na wezeshi ya utendaji wa waandishi wa habari na vyombo vya habari Zanzibar. Wamesema kuwa kuwasilishwa kwa Mswada huo BLW kutafungua fursa ya mjadala mpana, ushirikishwaji wa wadau na maboresho yatakayolenga kulinda uhuru wa vyombo vya habari, usawa wa kupata taarifa, uwajibikaji wa kitaaluma na maslahi ya umma.

Katika mkutano huo, wadau walijadili pia changamoto mbalimbali zinazoikabili tasnia ya habari Zanzibar, ikiwemo unyanyasaji na vitisho dhidi ya waandishi wa habari, maslahi duni, kodi na gharama kubwa za uendeshaji hususan kwa redio za kijamii, pamoja na ukosefu wa mifumo madhubuti ya kuwawezesha waandishi chipukizi na vyombo vya habari vinavyoanzishwa mtandaoni.

Sambamba na hilo, wadau walisisitiza wajibu wa vyombo vya habari kufanya utafiti wa kina na kutoa sauti za makundi ya pembezoni ikiwemo wanawake, watu wenye ulemavu, vijana na wananchi wa vijijini, ili kuhakikisha habari zinazotolewa zinawakilisha maslahi ya jamii yote.

Kwa pamoja, wadau wa tasnia ya habari wamesisitiza kuwa upatikanaji wa Sheria Mpya ya Huduma za Habari Zanzibar ni hitaji la msingi na la dharura hivyo linahitaji kupewa uzito unaostahiki.

IMETOLEWA NA:

 Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC),

Chama Cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA-ZNZ)

Waandishi wa Habari za Maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA)

Baraza la Habari Tanzania, Zanzibar (MCT, ZNZ)

 Jukwaa la Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania, Zanzibar (THRDC, ZNZ)

 

 

No comments

Powered by Blogger.