WAANDISHI WA HABARI WATAKIWA KURIPOTI ZAIDI MATUKIO YA UDHALILISHAJI VIJIJINI


NA MARYAM NASSOR

WAANDISHI wa habari nchini wametakiwa kuripoti kwa kina matukio ya udhalilishaji, hasa katika maeneo ya vijijini ambako wananchi wengi bado hawana mwamko wa kuyafichua na kuyatolea taarifa.

Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika katika Kituo cha Utengamano Welezo, Dk. Sikujua Omar  amesema vyombo vya habari vina jukumu kubwa la kuibua na kuripoti vitendo vya udhalilishaji vinavyoendelea katika jamii.

Amesema, bado jamii haina mwamko wa kuripoti matukio hayo, hususan katika maeneo ya vijijini ambako vitendo vya udhalilishaji hutokea kwa wingi lakini mara nyingi hubaki bila kuripotiwa.

“Ni jukumu la waandishi wa habari kutoa elimu na kuripoti matukio ya udhalilishaji, hasa katika maeneo ya vijijini ambako bado yanaendelea kwa kasi na jamii haina uelewa wa kuyatolea taarifa,” amesema Dk. Sikujua

Ameongeza kuwa, ni muhimu kuendelea kutoa elimu kupitia vyombo mbalimbali vya habari ili kupunguza au kumaliza kabisa vitendo vya udhalilishaji dhidi ya watoto na wanawake nchini.

Kwa upande wake, Mwanasheria wa mradi huo, Peter Marwa, amesema ni wajibu wa jamii kushirikiana katika kupambana na kuondosha vitendo vya udhalilishaji kwa watoto na wanawake ili kujenga jamii salama.

Amesema ,vyombo vya habari vina nafasi muhimu katika kutoa elimu na kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika kulinda haki za binadamu.

“Jukumu la kukuza haki za binadamu ni la jamii nzima, hivyo ni vyema kushirikiana katika kuondoa vitendo vya udhalilishaji nchini,” amesema.

Awali, Sister Simwe akitambulisha mradi wa kuwawezesha wananchi kuhusu haki za binadamu na utawala bora, amesema mradi huo unatarajiwa kutekelezwa katika shehia tano za Mkoa wa Kaskazini Unguja, ambako bado wananchi hawana mwamko na uelewa wa kuripoti matukio ya udhalilishaji.

Amesema, lengo la mradi huo ni kuongeza uelewa wa haki za binadamu pamoja na haki za kisheria katika jamii.

“Tuna imani kuwa wananchi wakizijua haki zao itakuwa rahisi kuzilinda na kufanya utetezi wa sera ili kila mwanajamii apate haki zake,” amesema.

Aidha, amesema kupitia mradi huo pia wanawake na vijana watawezeshwa kiuchumi ili kuongeza uhuru wao wa kifedha.

Nao, baadhi ya waandishi wa habari waliohudhuria kikao hicho, akiwemo Huwaida Nassor kutoka Asalam FM pamoja na Malik Shakhran, wamesema wamenufaika na mafunzo ya mradi huo na wako tayari kushiriki katika kutoa elimu kwa jamii kuhusu kupinga vitendo vya udhalilishaji.

 

Top of Form

Bottom of Form

 


No comments

Powered by Blogger.