USHIRIKI WA WANAUME KATIKA KUBORESHA USAWA WA KIJINSIA: NGUZO KUU YA KUBADILI MIENENDO YA JAMII NA UDHIBITI WA RASILIMALI


Na Maryam Nassor

Katika jitihada za kujenga jamii yenye haki, usawa na maendeleo endelevu, suala la ushiriki wa wanaume iwe kama wanafamilia, waume ama viongozi ,limeendelea kupata uzito mkubwa katika mijadala ya kijamii na sera za maendeleo.

Ingawa wanawake wamekuwa mstari wa mbele kudai haki na nafasi sawa, wataalamu wa jinsia wanasisitiza kwamba mabadiliko ya kweli hayawezi kupatikana bila ushiriki madhubuti wa wanaume katika kubadili mitazamo, kushiriki majukumu ya kifamilia na kuhakikisha usawa katika matumizi na udhibiti wa rasilimali.

Mienendo ya kijamii bado inawalazimisha wanawake kukaa nyuma

Katika jamii nyingi nchini Tanzania, ikiwemo Zanzibar, mfumo dume bado unatoa mamlaka makubwa kwa wanaume katika maamuzi ya kifamilia, kiuchumi na kijamii. Mwanamke bado anakumbana na changamoto nyingi katika kumiliki ardhi, kufanya maamuzi ya kifedha au kushiriki kikamilifu katika siasa na uongozi.

Katika Kijiji cha Ngambwa, mkoa wa Kusini Unguja, bado kuna changamoto kubwa katika kuhakikisha wanawake wanapata nafasi ya maamuzi na ushiriki wa maendeleo, ikiwemo umiliki wa rasilimali kama ardhi.

Bi. Asha Kombo, mkazi wa Ngambwa, anasema ni muhimu wanaume kuhamasisha wanawake kumiliki rasilimali kwani wao ni walezi na nguzo kuu za familia.

 Anabainisha kuwa wanawake wengi wanajishughulisha na shughuli za kilimo, lakini wengi hawana mashamba yao.

“Mabadiliko yapo, lakini bado mila na desturi zinawafanya baadhi ya wanaume kuhisi kupoteza nguvu zao endapo watakubali usawa wa kijinsia katika kumiliki rasilimali,” anasema Bi. Asha.

Ushiriki wa wanaume ni suluhisho, si tishio

Wataalamu wa masuala ya jinsia wanasisitiza kuwa usawa wa kijinsia hauko dhidi ya wanaume, bali ni kwa manufaa ya familia nzima. Pale wanaume wanaposhiriki katika malezi, kushirikiana katika shughuli za kiuchumi na kuruhusu wanawake kushiriki maamuzi, familia inakuwa imara zaidi.

Salama Khamis, mkazi wa Shehia ya Ngambwa, anasema tangu ajiunge na mradi wa Zanz Adapt, maisha yake yamebadilika kwa kuwa sasa ana uhakika wa upatikanaji wa chakula kwa familia yake.

Anaongeza kuwa mume wake alimpa shamba walime kwa pamoja na kwamba mchango wa wanaume katika kuendesha familia ni muhimu, lakini wanawake pia ni nguvu kubwa katika kuijenga jamii bora.

Kwa upande wake, Mzee Khamis Said, kiongozi wa kijamii Ngambwa, anasema kadiri wanaume wanavyoshiriki kubadilisha fikra, kuondoa mifumo kandamizi na kushirikiana na wanawake katika maamuzi ya rasilimali na majukumu ya kifamilia, ndivyo jamii inavyopiga hatua kuelekea usawa wa kweli.

Ushiriki wa wanaume katika udhibiti wa rasilimali

Handhari Saidi, mkazi wa Bungi, anasema maeneo yanayosababisha ukosefu wa usawa ni umiliki na matumizi ya rasilimali—hasa ardhi na fedha. Mara nyingi, mwanamke anapochangia kipato bado maamuzi ya matumizi hufanywa na mwanaume pekee.

Utafiti wa ndani kutoka kwa asasi zinazotekeleza programu za jinsia unaonyesha kuwa familia ambazo wanaume wanaridhia kufanya maamuzi ya pamoja hupata ushirikiano bora kwenye malezi na shughuli za kiuchumi.

Wananchi wanaona mabadiliko, lakini safari bado ni ndefu

Jafari Omar, kijana wa miaka 27, anasema ni muhimu wanawake kumiliki rasilimali zao ili kuepuka kunyanyasika katika familia na jamii.

Anasema kuwa, wanawake wake wanajishughulisha na kilimo na ufugaji lakini hawana maeneo yao wenyewe , hivyo hupelekea kushindwa kuendeleza ikitokea ugomvi wa kifamilia au kuachana.

“ Ni muda sasa wanaume kuwa mstari wa mbele kuhamasisha wanawake kumiliki ardhi kwa ajili ya shuguli zao za kiuchumi ikiwemo kilimo na ufugaji” anashauri.

Mikataba na katiba zinasemaje?

Ushiriki wa wanaume katika kuimarisha usawa wa kijinsia unaungwa mkono na mikataba na sera mbalimbali za kitaifa na kimataifa kama vile:

Mkataba wa  CEDAW (1979)  ambao  unaitaka serikali kuhakikisha wanawake wanapata haki sawa na wanaume katika rasilimali na maamuzi.

Mkataba wa  Beijing Platform for Action (1995) unasisitiza ushiriki wa wanaume katika kupinga ukatili na kukuza usawa wa kijinsia.

Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia Tanzania (2000) Inahimiza ushiriki wa wanaume katika kubadili mitazamo kandamizi dhidi ya wanawake.

 Katiba ya Zanzibar ya 1984  Inatoa haki ya usawa kwa wanawake na wanaume bila ubaguzi.lakini bado utekelezaji wa Katiba na mikata

Rhoda Daniel Kadaso kutoka Community Forestry Pemba (CFP) anabainisha kuwa zaidi ya asilimia 80 ya walengwa wa mradi wa Zanz Adapt ni wanawake, lakini wengi wao hawana ardhi ya kuendesha kilimo.

“Ikitokea mwanamke kalima mazao kwenye shamba la mume mpaka karibu ya kuvuna halafu wakaachana, kuna uwezekano mkubwa akabaki bila kitu,” anasema Rhoda, akisisitiza umuhimu wa wanawake kumiliki rasilimali zao ili waweze kuendeleza kiuchumi. Anasisitiza  Rhoda.

 

Mwisho

 


No comments

Powered by Blogger.