VIJANA WAONJWA KUACHANA NA TABIA HATARISHI ILI KUDHIDITI MAAMBUKIZI MAPYA, KUELEKEA SIKU YA UKIMWI DUNIANI.



Na Maryam Nassor

Kuelekea maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani yanayoadhimishwa Desemba 1 kila mwaka, Mkurugenzi wa Tume ya UKIMWI Zanzibar, Dk. Ahmed Mohd Khatibu, amewataka vijana kuacha tabia hatarishi zinazoweza kuongeza uwezekano wa kupata maambukizi ya virusi vya ukimwi.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Afisi za Tume hiyo,  kwa Mchina   Zanzibar, Dk. Khatibu amesema licha ya jitihada zinazochukuliwa, bado vijana wanaendelea kushiriki katika vitendo hatarishi vinavyo pelekea maambukizi mapya.

Amesema mwitikio wa dunia katika kupambana na UKIMWI umepungua, hasa baada ya Serikali ya Marekani kusitisha baadhi ya ufadhili wake wakati wa utawala wa Rais Donald Trump ulipoingia madarakani Januari mwaka huu.

Dk. Khatibu amesema kuwa, ingawa  Zanzibar wengi wanaoambukizwa virusi vya UKIMWI ni watu wazima kuanzia miaka 40 na kuendelea, lakini duniani kwa ujumla waathirika wakubwa ni vijana.

“Vijana hatuwezi kuwaacha nyuma katika mapambano dhidi ya UKIMWI, kutokana na kuendelea na tabia hatarishi zinazopelekea kujiingiza kwenye ugonjwa huu,” amesema.

Amesema katika kuelekea maadhimisho ya mwaka huu, Tume imefanya kampeni maalum kwa kuwafikia vijana wa vyuo vikuu na vyuo vya kati ili kuwapa elimu sahihi ya namna ya kujikinga.

Aidha, amebainisha kuwa baadhi ya vijana wanajiingiza katika mahusiano na watu wenye umri mkubwa wanaowalipia ada au kuwasaidia kifedha bila kujua hali zao za maambukizi, jambo ambalo ni hatari kwa afya zao.

“Unapokuwa na uhusiano na mtu mwenye umri mkubwa huwezi kujua ametoka wapi au historia yake ya afya. Pia vijana wengi hawana uelewa wa kutosha kuhusu njia za maambukizi,” ameongeza.

Amesisitiza umuhimu wa viongozi wa dini kushirikiana na Tume  hiyo, kutoa elimu kwa vijana ili kuongeza uelewa na kupunguza maambukizi mapya.

Aidha , amewahimiza vijana kutumia vituo vya huduma rafiki kwa vijana ambavyo vinatoa taarifa sahihi , ushauri na huduma za afya zinazoweza kuwakinga dhidi ya UKIMWI.

Katika hatua nyingine, Dk. Khatibu amesema kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya mwaka huu atakuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar,  Hemed  Suleiman  Abdullah. na Kaulimbiu ya mwaka huu ni:

“TUVISHINDE VIKWAZO VYA KIFEDHA, TUIMARISHE MAPAMBANO DHIDI YA UKIMWI.”

Mwisho

No comments

Powered by Blogger.