ZANZIBAR YAENDELEA KUPIGA HATUA KATIKA MAPAMBANO DHIDI YA UKIMWI
Na Maryam Nassor
Tarehe 1 Desemba ya kila mwaka, Dunia huadhimisha Siku ya
Ukimwi, siku iliyotengwa kwa ajili ya kueneza ufahamu wa ugonjwa wa Ukimwi
unaosababishwa na virusi vya ukimwi.
Katika kuadhimisha siku hii kwa Zanzibar, Makamu wa Pili wa
Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla amesema, “Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar imeandaa mpango maalum endelevu wa kupambana na ugonjwa wa Ukimwi.”
Amesema madhumuni ya mpango huo ni kuhakikisha mapambano
dhidi ya Ukimwi yanakuwa endelevu kwa kutenga fedha za ndani ili kufikia lengo
la kumaliza ugonjwa huo ifikapo mwaka 2030.
Makamu huyo wa Pili wa Rais amesema, “Zaidi ya miongo
mitatu Zanzibar imepiga hatua kubwa kudhibiti kiwango cha maambukizo ya virusi
vya Ukimwi na kuwa chini ya asilimia moja.”
Tafiti zinaonesha kwamba asilimia 0.4 ya wakaazi wa
Zanzibar wanaishi na maambukizo ya Virusi vya Ukimwi sawa na watu 10,256 kwa
mwaka 2025.
Amesema kuwa, “Zanzibar imefanikiwa kupunguza
maambukizi mapya kutoka watu 362 mwaka 2020 hadi watu 211 mwaka 2025.”
Aidha, amesema, “Tumeweza kupunguza vifo vitokanavyo na maradhi hayo kutoka vifo 230 mwaka 2020 hadi vifo 115 mwaka 2025.”
Hemed amesema kuwa, “Serikali itahakikisha sheria na
sera zote zinazingatiwa na zinalindwa dhidi ya ubaguzi, na upatikanaji wa
huduma za afya unakuwa wa haki kwa wote bila ubaguzi.”
Licha ya mafanikio hayo, amesema bado kuna changamoto
zinazohitaji nguvu ya pamoja ikiwemo upungufu wa rasilimali fedha, unyanyapaa
na tabia hatarishi miongoni mwa vijana.
Aidha alibainisha kwamba, “Desemba 1 inatukumbusha
kwamba mapambano dhidi ya ugonjwa huu bado hayajaisha, hivyo kila mmoja
anapaswa kushiriki kwa vitendo kuijenga Zanzibar isiyo na maambukizo mapya.”
Hemed aliwahakikishia watu wanaoishi na VVU kwamba Serikali
ya Awamu ya Nane itazifanyia kazi changamoto zilizotolewa na jumuiya ya ZAPHA+,
ikiwemo kuongeza bajeti ya upatikanaji wa dawa, vipimo na kuimarisha harakati
za mapambano.
Takwimu za Hali ya Ukimwi Zanzibar
Akiwasilisha taarifa ya hali ya Ukimwi
Zanzibar, Mwenyekiti wa Bodi ya Tume ya Ukimwi, Dk. Ali Salim Ali
alisema, “Kwa mwaka 2025 jumla ya watu 105,786 walipimwa; wanawake 58,397
sawa na asilimia 55 na wanaume 47,397 sawa na asilimia 45.”
Amesema watu 79,526 sawa na asilimia
75 walipimwa Unguja na 26,230 sawa na asilimia 25 kisiwani Pemba ambapo watu
697 sawa na asilimia 0.7 waligundulika na maambukizo ya VVU.
Alisema, “Kati ya hawa, wanawake
ni 466 sawa na asilimia 67 na wanaume 231 sawa na asilimia 33; kundi kubwa
likiwa umri wa miaka 25 hadi 49 ambalo linachangia asilimia 71.”
Amebainisha kuwa takwimu hizo
zinaonesha uhitaji wa kuimarisha mikakati ya kinga, elimu ya VVU na kuendelea
kuwaelimisha vijana ili kupunguza tabia hatarishi.
Amesema, “Juhudi za kuzuia maambukizo kutoka kwa mama
kwenda kwa mtoto zimefanikiwa; hadi Septemba wajawazito 53,706 walihudhuria
kliniki na 53,031 walifanyiwa vipimo vya VVU sawa na asilimia 99, na 98
walikuwa na maambukizo sawa na asilimia 0.5.”
Kwa upande wa watoto, alisema, “362 walipimwa kwa
kipimo cha DNA-PCR na wawili waligundulika na maambukizo sawa na asilimia 0.5.”
Mchango wa Wadau
Mshauri wa Programu na Afisa Mwakilishi wa UNAIDS Zanzibar,
Dk. George Anthony alisema, “Zanzibar imepiga hatua kubwa katika mapambano
ya Ukimwi, ikiwa ni ushahidi wa sera thabiti na mshikamano wa wadau.”
Amesema, “Bado kuna changamoto kwa makundi yaliyo
hatarini zaidi, ambapo viwango vya maambukizo yapo kati ya asilimia 11 hadi
19.”
Aidha ameongeza kuwa, “Safari ya kumaliza Ukimwi
ifikapo 2030 inahitaji hatua madhubuti ikiwemo kuimarisha mifumo ya ndani ya
kugharamia VVU na kuongeza uwekezaji wa kitaifa.”
Sauti za Watu Wanaoishi na VVU
Akisoma risala ya watu wanaoishi na VVU, Sara Abdi Mwita
alisema,
“Kutokana na mashirika na wafadhili kusua sua katika kutoa misaada, tunaomba
Serikali kuweka dawa za ARV kwenye bajeti ya Serikali ili huduma iendelee kuwa
endelevu.”
Amesema wagonjwa wanakabiliwa na changamoto katika huduma
za kijamii hivyo wanaomba kutambuliwa kupitia mifumo ya utoaji huduma.
Naye Asha Subeti (si jina lake halisi), mtu anayeishi na
VVU, alisema,
“Tumefarijika sana kupewa matumaini katika siku hii, kwani tunakabiliwa na
changamoto nyingi ikiwemo ukosefu wa ufadhili.”
Ameongeza, “Serikali yetu ni sikivu, itutatulie
changamoto zinazoikumba jumuiya zetu.”
Siku ya Ukimwi Duniani huadhimishwa kila mwaka Desemba
1, ambapo kauli mbiu ya mwaka 2025 “Tuvishinde
Vikwazo vya Kifedha, Tuimarishe Mapambano ya Ukimwi.”
Mwisho
Post a Comment