MRAJISI WA ASASI ZA KIRAIA AHIMIZA JAMII KUJITOA KATIKA UHIFADHI WA MAZINGIRA
Na Maryam Nassor
Mrajisi wa
Asasi za Kiraia Zanzibar, Ahmed Ghalid Mohamed, amesema Afisi yake iko tayari
kushirikiana na uongozi wa Mkoa wa Kusini Unguja kuwa mfano wa utekelezaji wa
shughuli za uhifadhi wa mazingira.
Akizungumza
katika Kongamano la Kiiamani kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi lililofanyika
katika Afisi za Zanzibar Climate Change Alliance (ZACCA) Jumbi Ipa, alisema ni
muhimu jamii kujitoa na kuwa sehemu ya juhudi za utunzaji wa mazingira.
Amesema Mkoa
wa Kusini Unguja ni miongoni mwa maeneo yaliyoathiriwa zaidi na mabadiliko ya
tabianchi, hivyo ni wajibu wa wananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za
uhifadhi wa mazingira.
“Jamii zetu ziwe sehemu kubwa ya uhifadhi wa mazingira badala ya kuyaharibu kwa kukata kuni na mkaa,” alisema Ahmed.
Katika hatua
nyengine, alikabidhi shilingi milioni tano kwa vikundi viwili vya Unguja na
Pemba vinavyotekeleza shughuli za utunzaji wa mikoko, kwa lengo la kuviwezesha
kuendeleza kazi hizo.
Amevitaka vikundi hivyo kutumia fedha hizo kwa malengo yaliyokusudiwa na kuahidi kufanya ziara ya mara kwa mara kufuatilia maendeleo ya utekelezaji.
“Nawashukuru
sana DANMISSION kwa kujitoa kuzisaidia taasisi zetu ili kurejesha uoto wa asili
na kuisaidia jamii kwa ujumla,” aliongeza.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa ZACCA, Mahfoudh Shabaan Haji, alisema wameamua kufanya kazi na jamii kwa kuvipatia msaada vikundi hivyo — kikundi cha Uzi kutoka Mkoa wa Kusini Unguja na kikundi cha TUJIPE kutoka Kaskazini Pemba.
Amesema
ZACCA inatekeleza Mradi wa COFOMA ambao unalenga kuwawezesha wananchi kuhifadhi
mazingira yao kupitia upandaji wa mikoko.
“Lengo kuu
la mradi huu ni kushirikiana na jamii katika kuihifadhi mikoko ili kupambana na
mabadiliko ya tabianchi ambayo yametuathiri kwa kiasi kikubwa,” alisema
Mahfoudh.
Naye Afisa Mradi wa Uhifadhi Mazingira kutoka DANMISSION, Dickson Shekibom, alisema matokeo ya mwaka mmoja wa mradi huo ndiyo yatatoa mwelekeo wa uwezekano wa kubuni mradi mwingine wa muda mrefu.
“Tuna imani kubwa na vikundi hivi. Wakionesha matokeo
mazuri ndani ya mwaka mmoja, tutaweza kubuni mradi mkubwa zaidi wa miaka mitano
au sita,” alieleza.
Walisema taasisi za dini zitaendelea kutoa elimu ya
utunzaji wa mazingira ili kuhamasisha jamii kuwa mstari wa mbele katika
mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.
Nao baadhi ya wanachama wa kikundi cha Tustahamiliane kutoka Uzi waliishukuru ZACCA kwa kuwapatia fedha za utekelezaji wa shughuli za uhifadhi wa mikoko katika shehia yao.
Kongamano hilo limewashirikisha wadau mbalimbali wa
mazingira kwa lengo la kujadiliana kuhusu njia bora za ushirikiano katika
kulinda na kuhifadhi mazingira.
MWISHO





Post a Comment