Hofu zinazowakumba wagombea wanawake kutoka vyama vya siasa nchini Tanzania


Na Maryam Nassor

Mwaka 2025 ni mwaka wa uchaguzi mkuu nchini Tanzania. Kadiri siku zinavyosogea, maandalizi ya uchaguzi yanaendelea kushika kasi, huku vyama 11 vya siasa vikijipanga kuwasimamisha wagombea wake.

Kwa mujibu wa Ripoti ya Taasisi ya Kidemokrasia ya  NDI  ikishirikiana na Chama Cha Waandishi wa Habari Wanawake  Tanzania Zanzibar ( TAMWA ZNZ) ya mwaka (2021), imesema  asilimia 41 ya wanawake waliogombea waliripoti kukumbwa na vitendo vya unyanyasaji au vitisho wakati wa kampeni. Hali hii imewafanya   baadhi ya wanawake  kuamua kuacha kugombea kabisa.

Hata hivyo, kwa upande wa wanawake hasa kutoka vyama vya upinzani, hofu na mashaka vinaendelea kutawala nafsi zao kutokana na matukio yaliyowahi kujitokeza katika chaguzi zilizopita.


Mtumwa Faiz  Ali  (40), mgombea Ubunge Jimbo la Chumbuni  kutoka  Chama Cha Upinzani  cha Allience for Democrats Change ( ADC) , amesema uzoefu wa chaguzi zilizopita unamfanya ajiulize kama kweli anapaswa tena kuingia kwenye kinyang’anyiro cha siasa.


“Kila mara uchaguzi unapokaribia, wanawake  tunahisi hatari , Tunatishwa, tunazomewa, na mara nyingine tunafuatiliwa.  Hatuna  hofu ya kushindwa tu, bali hofu ya usalama wetu,” amesema Mtumwa.

Amesema kuwa,  mara nyingi wagombea wanawake kipindi cha uchaguzi na kampeni  hukumbana na vitisho, ghasia na fujo.

“Kutokana na hali za uchaguzi zinavyokuwa Visiwani Zanzibar bado wanawake  wanaogopa kugombea nafasi za uongozi hasa kutoka vyama vya upinzani , hivyo tunaiyomba Serikali ituwekee mazingira rafiki kwa  vyama vyote” amesema.

Amesema kuwa,  mwaka 2020 alishuhudia wenzake wakipoteza mali, wengine wakikamatwa, huku baadhi wakilazimika kujificha kwa muda. “Kama mazingira ya siasa yatabaki hivi, wanawake wengi wataona bora wakubali kushangilia badala ya kugombea,” ameongea kwa huzuni.


 Aidha amesema kuwa, wanawake wengi wa vyama vya upinzani, hofu kubwa zaidi ni usalama wakati wa kampeni. Katika chaguzi zilizopita, matukio ya vurugu, kukamatwa kiholela, na kupigwa yaliripotiwa na vyombo vya habari na mashirika ya haki za binadamu.

“Sio kwamba wanawake hatutaki kugombea, bali tunataka mazingira salama Tunataka tuchaguliwe kwa hoja, siyo kwa hofu,” amesema Mtumwa.

Kwa mujibu wa utafiti wa Tanzania Gender Networking Programme (TGNP, 2023), umeonesha  wanawake wengi wanaojihusisha na siasa hukumbwa na changamoto za vitisho, matusi ya kijinsia, na kudharauliwa kwa kisingizio cha jinsia yao.

Hali hii, imechangia idadi ndogo ya wanawake kujitokeza kugombea nafasi za uongozi, hususan katika vyama vya upinzani.

Licha ya hofu kutoka nje, baadhi ya wanawake wanasema changamoto nyingine hutokana na mfumo wa ndani wa vyama vyao.

 Salha Said Hamad  mgombea Ubunge Jimbo la Donge Mkoa wa Kaskazini Unguja kupitia chama cha United Democratic Party  ( UDP)   amesema wagombea wanawake kutoka vyama vya upizani hukumbwa na hofu kubwa  katika kipindi cha uchaguzi kutokana na mazingira  yanayokuwepo.

“ Chaguzi nyingi zinazofanyika wanaosimamia uchaguzi ni vyombo vya dola ambao wakiwepo hofu hutanda ndani ya nyoyo za watu ‘’ amesema.

Salha amesema kuwa, Licha ya changamoto hizo, wanawake wengi bado wana matumaini katika kugombea nafasi za uongozi.


“Hofu ipo, lakini hatutarudi nyuma, Tunataka mwaka huu kuandika historia mpya ya wanawake katika siasa,” amesema  Salha kwa ujasiri.

Mgombea huyo amesema , kwa upande wa Kaskazini Unguja   vyama vya upizani haviko huru ukilinganisha na vyama vyengine bado watu wanaogopa hata kugombea katika vyama hivyo.

“ Huku kwetu  kaskazini Unguja unajiona huko salama kipindi cha uchaguzi ukiwa ni mgombea  hasa  kutoka vyama vya upinzani unaonekana kama muasi “


Kwa mujibu wa Sheria ya  vyama vya siasa  ya mwaka 1992 iliyoongeza kifungu cha 10 C ndani ya sheria hiyo,  ina vitaka vyama vya siasa  kuhakikisha Usawa wa Jinsia  ndani ya  vyama  hivyo.

Hata hivyo, utekelezaji wa sheria hiyo bado unasua sua   Hali hiyo imeongeza hofu kwa wanawake , hata kama watajitokeza kugombea, huenda wasipewe nafasi stahiki ndani ya vyama vyao.


Utafiti wa Taasisi ya Uongozi Bora (2022) unaonyesha kuwa asilimia 62 ya wanawake waliohojiwa walikiri kuhisi hofu ya kushiriki siasa kutokana na kejeli na mashambulizi ya maneno kutoka kwa jamii na mitandao ya kijamii.

Dr. Mzuri Issa, Mkurugenzi wa  Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania kwa upande wa Zanzibar (TAMWA  ZNZ), amesema hofu hizi zinatokana na mazingira dume yanayowatisha wanawake.


“Kuna wanawake wanaothubutu, lakini jamii inawavunja moyo kwa kauli za kubeza, Tunapaswa kujenga mazingira salama ya kisiasa kwa wote, hasa wanawake,” amesisitiza Dk. Mzuri.

Aidha ameitaka Tume ya Uchaguzi Zanzibar ( ZEC) kuweka mazingira mazuri kwa wagombea wa vyama vyote vya siasa ili kuwawezesha kushiriki katika uchaguzi  kwa amani .


“Wanawake wakihisi wanalindwa, watajitokeza zaidi kugombea. Lakini bila ulinzi wa kisheria na kijamii, wengi watabaki kimya,” amesema.

Taasisi za kiraia kama  Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake  Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ ) ,Tanzania  Gender Networking Program  ( TGNP )  na  Women in Law and Development in Afirica (WiLDAF ) zimekuwa zikitoa wito kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kuhakikisha mikakati madhubuti ya kulinda wagombea wanawake.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Thabiti Idarous Faina, amesema tume inaendelea kuandaa miongozo itakayowalinda wagombea wote bila ubaguzi.


“Tunatambua changamoto zilizopo, hasa kwa wanawake. Tunataka uchaguzi wa haki, amani, na ushiriki sawa kwa wote,” amesema.

                                             Mwisho

No comments

Powered by Blogger.