Wanawake si wafuasi tu wa siasa, bali ni wabeba mabadiliko ya jamii – Nadhra Ali Haji.

 

 


Na Maryam Nassor

Katika historia ya kisiasa ya Zanzibar, nafasi ya wanawake mara nyingi imekuwa haionekani  ipasavyo,  Lakini kila kizazi kimekuwa na mashujaa wake waliothubutu kuvunja ukuta wa kimya.

Miongoni mwao ni Nadhra Ali Haji, mgombea ubunge wa Jimbo la Malindi kupitia Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC). Ujasiri wake, uzoefu wa kisiasa na dhamira ya kuimarisha ushiriki wa wanawake katika maendeleo ni kielelezo cha kiongozi wa kizazi kipya.

Safari yake ya kisiasa, uzoefu wa uongozi na mtazamo wa kijinsia ni kielelezo cha namna wanawake wanavyoweza kuchangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

MAISHA YAKE BINAFSI

Nadhra Ali Haji alizaliwa mwaka 1970  Mtaa wa Vikokotoni Mjini , Unguja Zanzibar.  Akiwa mtoto wa familia yenye maadili ya heshima na mshikamano, alikulia katika mazingira yaliyochanganya historia, utamaduni na harakati za kijamii, hali iliyompa msingi wa mapema wa kujiamini na kujitolea.

Elimu yake ameanzia  katika Shule ya Msingi   Tumekuja kisha akaendelea na masomo ya sekondari katika Shule ya Ben bembela.

Kwa wakati huo  baada ya kumaliza elimu yake  ya Sekondary  alikwenda kujiunga na kikosi cha  Idara ya anga  ambapo elimu hiyo  ilimjengea msingi imara wa kuunganisha taaluma na vitendo katika uongozi.

SAFARI YAKE YA KISIASA

Nadhra Ali Haji alijiunga rasmi na chama cha CUF mwaka 1993, kipindi ambacho chama hicho kilikuwa kinapanua wigo wake katika harakati za kidemokrasia nchini.

Safari yake ya uongozi imenza akiwa mwanachama  mdogo kabisa katika  chama wananchi CUF , ambapo alikuwa  ni katibu katika  tawi la Shangani na Mji mkongwe Unguja.

Amesema na baadae  mwaka  1995 akiwa Pemba alihamasika   kugombea nafasi ya viti maalum  kura zilifungana yeye na mwenzake , lakini kutokana na umri mdogo aliokuwa nayo  alikuwa hajui  baada ya kushinda atakuwa nani hivyo nafasi hiyo akamuachia menziwe.

 “ Najivunia sana katika siasa mimi niliazia tawi ambapo nilikuwa  muhamasishaji mzuri wakati mwengine nilifuatwa na watu wa chama cha Mapinduzi nijiunge na chama hicho” amesema Bi Nadhra.

Akiwa mwanachama wa mwanzo kabisa, alikuwa katibu wa  tawi la  mji Mkongwe na  alishiriki moja kwa moja katika mikutano ya hadhara, warsha za mafunzo, na mijadala ya kisiasa iliyojikita katika kutafuta misingi imara ya chama.

Kutokana na mabadiliko ya mfumo na viongozi  kwa chama hicho mwaka 2024 Nadhra alijiunga  na chama cha ADC  na  alijipatia umaarufu mkubwa kama mwanasiasa mwenye msimamo thabiti, aliyejenga hoja zenye mashiko na mwenye mtazamo mpana kuhusu nafasi ya mwanamke katika siasa.

UZOEFU WAKE KATIKA KUSHIRIKI UCHAGUZI.

Kabla ya kugombea Ubunge wa Jimbo la Malindi mwaka huu, Nadhra aliwahi kushiriki uchaguzi wa  mwaka 2010 akiwa katika  chama cha wananchi CUF, ambapo alisimama kugombea nafasi ya  viti maalum katika chama hicho ingawa hakushinda.

 Aidha, mwaka 2015 alijaribu tena kugombea nafasi ya ubunge kupitia chama hicho, lakini hakuweza kufanikisha ushindi kutokana na changamoto za kisiasa za wakati huo.

Hata hivyo, kushiriki kwake katika chaguzi hizi kumemjengea uzoefu wa kisiasa, uimara wa kisaikolojia, na uelewa wa karibu wa changamoto zinazowakabili wapiga kura wake.

MTAZAMO WA KIJINSIA .

Nadhra Ali Haji ni miongoni mwa viongozi wachache wanaoamini kwamba maendeleo ya kweli ya Zanzibar hayawezi kufanikiwa bila ushiriki wa wanawake.

Amesema kuwa ,wanawake hawapaswi kuachwa nyuma katika siasa , elimu, uchumi na afya ambapo  anapigania uwezeshaji wa wanawake kiuchumi kupitia vikundi vya mikopo midogo midogo na mafunzo ya ujasiriamali.

Amesema kuwa, Elimu ya mtoto wa kike  ni muhimu akiamini kwamba elimu ni daraja la kumtoa mwanamke kwenye umasikini na utegemezi.

 

Aidha amesema kuwa, Ushiriki wa wanawake katika uamuzi wa kisiasa,  ni muhimu huku akihimiza vyama vya siasa  na serikali kutenga nafasi zaidi kwa wanawake kwenye ngazi za uongozi.

 

Kupitia nafasi yake ndani ya ADC ya Mwenyekiti wa wanawake katika chama hicho   amekuwa mstari wa mbele kuhamasisha wanachama wanawake kushiriki kikamilifu kwenye mikutano, warsha na kampeni.

 

MALENGO YAKE YA BAADAE.

Iwapo atapata ridhaa ya wananchi, Nadhra ameahidi kusukuma ajenda zifuatazo , Kwanza Kuimarisha huduma za elimu na afya kwa wanawake na Watoto katika jimbo hilo.

Ameseme kuwa  atawawezesha vijana na wanawake kwa miradi ya kiuchumi na maendeleo kwa kuanzisha  viwanda vidogo vidogo katika jimbo hilo.

 Aidha  kutoa huduma ya mikopo nafuu kwa wanawake na wanaume wajasiriamali  ili  kujikwamua kiuchumi.

 

“ Nitahakikisha  nasimamia uwakilishi wa wanawake na vijana katika nafasi za maamuzi jimboni ‘’ amesema .

 

WATU WANAOMFAHAMU  WANAMZUNGUMZIAJE.

Mtumwa Feisal mgombea ubunge  jimbo la Chumbuni  kwa tiketi ya chama hicho,  amesema Nadhra Ali Haji si tu mgombea wa ubunge  ni alama ya matumaini mapya kwa Malindi.

’’ Kiukweli Nadhra ni mgombea  shupavu  mwenye maono na mapenzi ya kweli kwa wananchi na mpenda maendeleo  ni alama ya matumaini  kwa wana Malindi” amesema.

Amesema kuwa,   tangu alipojiunga na ADC , safari yake imekuwa ni ushahidi  na ujasiri wa mwanamke anayeamini kwamba siasa ni chombo cha maendeleo ya kijamii.

Nae, Abdallah Ali mwanachama wa chama hicho amesema Mgombea huyu anabeba matumaini ya wanawake na wanaume wa Malindi, akiwakilisha kizazi kipya cha wanasiasa wenye nia ya dhati ya kulijenga taifa kwa mshikamano na mshikikano wa kijinsia

 Amesema kuwa, Kwa wananchi wa Malindi  Nadhra anawakilisha siasa zenye maono  siasa zinazojali jinsia  na siasa zinazolenga maendeleo kwa wote.

“ Ushindi wake unaweza kuwa si ushindi binafsi, bali ni ushindi wa wanawake wote wa Zanzibar wanaopigania nafasi ya kusikika na kushirikishwa “ amesema .

       Bottom of Form

                                      

 

                               Mwisho

No comments

Powered by Blogger.