Changamoto za Upatikanaji wa Mikopo kwa Watu Wenye Ulemavu Zanzibar



Na Maryam Nassor

Mfumo wa mikopo ambao Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeanzishwa ukiwa na lengo la kuwawezesha wajasiriamali na vijana kujitegemea kiuchumi.

 Umekuwa pia ukihusisha makundi maalum yakiwemo watu wenye ulemavu, Hatua hii ni sehemu ya jitihada za serikali kuhakikisha kila mmoja anashiriki katika maendeleo ya taifa bila kubaguliwa.

Hata hivyo, pamoja na dhamira njema ya serikali  bado kuna changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika kupata fursa hizo  hali inayowafanya watu wenye ulemavu kuhisi kama hawajanufaika ipasavyo na haki zao za kiuchumi  na kijamii.

Wengi wao wanakumbana na masharti magumu, upungufu wa taarifa sahihi, na ukosefu wa miundombinu rafiki  jambo linalokwamisha jitihada za kujikwamua kiuchumi kupitia mikopo.

Ushuhuda wa Watu Wenye Ulemavu

Akizungumza na mwandishi wa makala hii, Aisha Omar  mjasiriamali na mlemavu wa uoni kutoka Kikwajuni  Mjini Unguja, amesema changamoto kubwa zinazowakumba ni pamoja na masharti magumu ya dhamana na nyaraka za mikopo.

 Aisha  anayejishughulisha na utengenezaji wa udi, mafuta ya mgando na krimu za ngozi, alisema anahitaji mkopo wa angalau shilingi milioni moja, lakini hadi sasa hajaufanikisha kutokana na ugumu wa masharti.

“Kutokana na shughuli zangu za ujasiriamali nahitaji mkopo angalau wa milioni moja, lakini bado sijafanikiwa kuupata kwani mara nyingi mikopo inayotolewa huwa ni ya vikundi. Mikopo ya mtu mmoja mmoja masharti yake huwa magumu mno,” amesema Aisha.

Aisha aliongeza kuwa uelewa mdogo kwa baadhi ya watu wenye ulemavu ni tatizo kubwa kwani wengi wao hawapati taarifa sahihi kuhusu namna ya kuomba na kupata mikopo.

 Alieleza kuwa aliwahi kuomba mkopo wa 4-4-2 lakini alikosa kutokana na kushindwa kutoa dhamana, hali iliyomkatisha tamaa licha ya dhamira yake ya kukuza biashara ndogo.

Kwa upande wake, Juma Hassan, kijana mfanyabiashara na mlemavu wa macho kutoka Mwanakwerekwe, amesema watu wenye ulemavu bado hawajafikiwa ipasavyo na elimu ya mikopo.

“Changamoto kubwa kwetu ni upatikanaji wa taarifa. Mara nyingi matangazo yanatolewa kwa maandishi pekee, sisi wasioona tunakosa kabisa nafasi ya kujua mapema,” amesema Juma.

Ameongeza kuwa mara nyingine jamii huwapuuza watu wenye ulemavu kwa kudhani hawana uwezo wa kurejesha mikopo, jambo linaloathiri imani ya taasisi zinazotoa huduma hizo.

Fatma Ali, mlemavu wa usikivu kutoka Chaani mkoa wa  Kaskazini Unguja, amesema watu wenye ulemavu wa uziwi mara nyingi hukosa taarifa sahihi kutokana na kukosekana kwa wakalimani katika vikao vya kutoa elimu ya mikopo.

“Sisi viziwi mara nyingi hatuna wakalimani kwenye vikao vya elimu ya mikopo. Tukifika  tunakaa tu bila kuelewa, mwisho wa siku tunabaki nyuma kimaendeleo,” amesema Fatma.

Fatma amesisitiza kuwa mikopo ni fursa muhimu kwa wananchi wote, lakini changamoto wanazokabiliana nazo watu wenye ulemavu zinahitaji suluhisho la haraka kupitia taratibu bora, utoaji wa taarifa kwa njia jumuishi, na kuwepo kwa miundombinu rafiki.

Sheria ya Watu Wenye Ulemavu

Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Zanzibar ya mwaka 2006 pamoja na marekebisho yake, imeweka wazi kwamba watu wenye ulemavu wana haki ya kupata fursa sawa katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

 Kifungu cha sheria hiyo kinatoa wajibu kwa serikali kuhakikisha hakuna mtu anayeachwa nyuma kwa sababu ya hali yake ya ulemavu.

Kwa mantiki hiyo, watu wenye ulemavu wanapaswa kupewa kipaumbele maalum katika upatikanaji wa mikopo kama ya 4-4-2 ili kujenga usawa wa kijamii na kupunguza pengo la kiuchumi kati yao na makundi mengine.

Nae, Mkuu wa Divisheni ya Mfuko wa Uwezeshaji  wananchi kiuchumi  Zanzibar ( ZEEA) Hashimu Iddi Simba  amesema  kupitia  programu ya 4 4 2  ni fursa adhimu  kwa watu wenye ulemavu  kujiendeleza kiuchumi.

Amesema kuwa,  tokea ianzishwe programu hiyo  mwaka Septemba  2024,  mpaka sasa  jumla ya watu wenye ulemavu  170 wamenufaika kuwezeshwa  kiuchumi, wanawake  wakiwa ni 93 na wanaume 79.

Licha ya mafanikio hayo, lakini anakiri kuwa bado kuna changamoto kubwa ya kuwafikia watu wengi wenye ulemavu kutokana na kutokukidhi vigezo na masharti.

“ Ni kweli bado hatujawafikia watu wengi wenye ulemavu kuwezeshwa kiuchumi kwa sababu wengi wao wanakosa vigezo vya kukopesheka“ amesema.

Kauli ya Serikali

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Mhe. Mudrik Ramadhan Soraga, alipoulizwa kuhusu suala hili, alisema

“Serikali imekusudia kuhakikisha mikopo  inawanufaisha wote bila ubaguzi ,Tumeanza kuweka utaratibu maalum wa kuyajengea uwezo makundi maalum, hususan watu wenye ulemavu  kwa kutoa elimu, kurahisisha masharti na kuhakikisha ushirikishwaji wao unakuzwa zaidi.”

Kauli hii inaonesha dhamira ya dhati ya serikali kuhakikisha kila mwananchi ananufaika na mikopo hiyo, japo changamoto za kiutekelezaji bado zinahitaji kushughulikiwa kwa haraka.

                        Mwisho

No comments

Powered by Blogger.