UMUHIMU WA LUGHA YA ALAMA KWA WATU WENYE ULEMAVU WA UZIWI


Na Maryam Nassor

Katika jamii yoyote ile  mawasiliano ni daraja la kuelewana    Hata hivyo  kwa watu wenye ulemavu wa uziwi, mawasiliano hukumbwa na changamoto kubwa endapo lugha ya alama haitatiliwa mkazo.

 Lugha ya alama si chombo cha mawasiliano pekee  bali ni nguzo ya kujumuisha,  kuondoa vikwazo  na kutoa fursa sawa za elimu  ajira na ushiriki wa kijamii.

Hata hivyo, bado kuna changamoto ya uelewa mdogo kutoka kwa jamii na taasisi nyingi kuhusu nafasi ya lugha ya alama kama haki ya msingi.

Mikataba ya kimataifa kama Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (CRPD) wa Umoja wa Mataifa unasisitiza katika Kifungu cha 21 juu ya haki ya watu wenye uziwi kutumia lugha ya alama kama nyenzo kuu ya upatikanaji wa taarifa na huduma.

Zanzibar na Tanzania zikiwa washiriki wa mkataba huu, zina jukumu la kuhakikisha lugha ya alama inatambulika rasmi na kutumika katika taasisi zote za umma na binafsi.

Akizungumza na mwandishi wa makala hii. Aisha Salah mkaazi wa  Fuoni wilaya ya Magharibi B Unguja mwenye ulemavu wa uziwi amesema wanakumbana na changamoto kubwa ya mawasiliano.

Amesema kuwa, lugha ya alama ni nyenzo muhimu kwa wenye ulemavu wa uziwi ,lakini lugha hiyo watu wengi hawaijui hata hao wenyewe wenye ulemavu wa uziwi.

“ Changamoto nyengine ni kutokufundishwa katika maskuli lugha ya alama hivyo hata sisi ambao tuna uziwi  baadhi yetu hatujui lugha ya alama “ amesema hivyo kuiomba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuiweka kwenye mitaala  ya Wizara ya Elimu lugha hiyo.

Aidha amesema kuwa, Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Zanzibar Na. 9 ya mwaka 2006 zinatoa haki kwa watu wenye ulemavu kupata huduma pasipo  na ubaguzi, ikiwemo haki ya kutumia lugha ya alama.

“ Ingawa Sheria hizi zinasisitiza usawa katika elimu, afya, na huduma nyinginezo za kijamii kwa watu wenye uziwi lakini bado utekelezaji wake bado unasua sua“ amesema Aisha.

 Nae, Fatma Omar, mwanachama wa Jumuiya ya Watu Wenye Uziwi Zanzibar (JUVIZA) amesema lugha ya alama ndiyo suluhisho pekee kwa watu wenye ulemavu wa uziwi.

 

 Amesema kuwa, endapo jamii itakuwa na uwelewa wa kutosha kuhusu lugha ya alama basi wao watakuwa hawana ulemavu tena.

 “Lugha ya alama ndiyo daraja letu la kueleza hisia na mahitaji yetu   Bila lugha hii tunabaki kando ya jamii siku zote , ” amesema Fatma.

Ni wajibu wa serikali, jamii na taasisi binafsi kuhakikisha lugha ya alama inatambuliwa na  watu wote  na kutumika kikamilifu ili  hakuna mtu anayeachwa nyuma.

 

Ali Haji  mwalimu mwenye uziwi, amesema  Elimu bora kwa watu wenye uziwi haiwezi kupatikana bila walimu wa lugha ya  

alama na vitendea kazi vya lugha hii mashuleni.

 

Amesema kuwa,  ni vyema Serikali kupitia wizara ya elimu  kulifanyia kazi suala la umuhimu walugha ya alama mashuleni ili kuondokana na changamoto ya mawasiliano.

 

“ Tunaiomba Serikali kuona umuhimu wa lugha ya alama mashuleni ili kila mtu aweze kujifunza tuondokane na ubaguzi uliopo wa mawasiliano“ amesema .

 

Abdallah Alawi Abdallah ni Katibu Mtendaji kutoka Jumuiya ya Viziwi Zanzibar ( JUVIZA) amesema kuna umuhimu mkubwa wa lugha ya alama na wakalimani wa lugha  hiyo.

 

Amesema kuwa, wao kama JUVIZA wana maoni tofauti  juu ya  lugha ya alama wanataka lugha hiyo, ingizwe kwenye mitaala ya wizara ya elimu na kusomeshwa mashuleni kuanzia ngazi ya msingi hadi Chuo kikuu.

 

“ Tukiwa  na mitaala ya lugha ya alama katika ngazi ya msingi hadi chuo kikuu basi sisi Viziwi tutakuwa sio watu wenye ulemavu tena kwani mazingira yatakuwa jumuishi , hatutojihisi tena ni walemavu“ amesema Abdallah.

 

 Aidha ameiomba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kulifanyia kazi ombi lao hilo la kuanzisha mitaala ya lugha ya alama ili kuondokana na changamoto za mawasiliano wanazokumba nazo.

 

“ Tunajua kuwa  hata baadhi ya sisi watu wenye ulemavu wa uziwi wengine hatujui lugha ya alama hivyo, hata tukiwekea wakalimani kila kwenye Ofisi za Umma  na binafsi tatizo halitoondoka kwasababu baadhi yetu hawajui lugha ya alama“ amesema Abdallah kwa msisitizo.

Aidha, amesema kuwa  jumuiya za watu wenye ulemavu zinasisitiza haja ya Serikali kuwekeza zaidi katika mafunzo ya wakalimani wa lugha ya alama, kuongeza uelewa wa jamii, na kuhakikisha kwamba lugha hii inakuwa sehemu ya mafunzo rasmi ili kusiwe na pengo kati ya wenye uziwi na wengine.

“Lugha ya alama siyo ishara tu ya mawasiliano  bali ni haki ya msingi ya kijamii inayowaunganisha na kuwawezesha watu wenye uziwi kushiriki kikamilifu katika maisha ya kila siku.” Amesema Katibu Mkuu  huyo wa Jumuiya ya Viziwi Zanzibar ( JUVIZA)

 

 

                                               Mwisho           Top of Form

Bottom of Form

 

No comments

Powered by Blogger.