MGOMBEA URAIS ADC AHIMIZA AMANI, AHAIDI ELIMU NA CHAKULA KWA WOTE
Na Maryam Nassor
Mgombea Urais kwa tiketi ya chama cha Alliance for
Democrats Change (ADC), Hamad Rashid Mohammed, amewataka Wazanzibari
kutokubali kurubuniwa na mtu yeyote ili kuivunja amani iliyopo nchini.
Akizungumza katika viwanja vya Kibanda Maiti, wakati wa
uzinduzi wa kampeni za chama hicho, Hamad alisema amani ni hazina kubwa kwa
wananchi wa Zanzibar na inalindwa kwa gharama zote.
“Sisi
chama cha ADC tunahamasisha Wazanzibari kuendelea kuitunza amani yetu, kwani
tunayajua madhara makubwa ya uvunjifu wa amani,” alisema mgombea huyo.
Hamad ameahidi kuwa endapo chama chake kitapewa ridhaa na wananchi, ndani ya siku 100 za kwanza atahakikisha kila Mzanzibari atanunua kilo ya mchele kwa shilingi 1,500
Aidha, alisema
kipaumbele chake cha kwanza ni kuhakikisha wananchi wanapata shibe kwa kuweka
mazingira mazuri ya upatikanaji wa chakula na kila familia inakuwa na akiba ya
chakula.
Ameahidi elimu bure
kuanzia chekechea hadi chuo kikuu, pamoja na kima cha chini cha mshahara kwa
kila mfanyakazi kuwa shilingi 600,000 za Kitanzania.
“Nawaombeni
sana ndugu zangu kukipigia kura chama chetu ili vipaumbele vyetu viweze
kutekelezeka,” alisisitiza Hamad.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wanawake wa chama hicho na mgombea ubunge Jimbo la Malindi, Nadhra Ali Haji, amewaomba wanaume kutowanyima wake zao ruhusa ya kushiriki kupiga kura ifikapo Oktoba 29 mwaka huu.
Alisema mara nyingi kipindi cha uchaguzi kumeibuka migogoro
ya ndoa kutokana na wanaume kuzuia wake zao kushiriki uchaguzi, jambo
linalowanyima haki ya kikatiba.
“Waacheni
wanawake wakatimize haki yao ya msingi na ya kikatiba ya kupiga kura.
Tunavyoona kutokana na sera za chama chetu, wengi watakipigia kura,” alisema
Bi. Nadhra.
Nae, mgombea ubunge Jimbo la Chumbuni kwa tiketi ya
ADC, Mafunda Faisal Ali, amewataka wananchi kuendelea kulinda amani ya
nchi kwani bila amani hakuna maendeleo.
“Ndugu
zangu tuendelee kutunza amani ya nchi yetu. Nawaombeni sana kukipigia kura
chama chetu ili tushirikiane kuleta maendeleo,” alisema Mafunda.
Awali, Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kupitia ADC, Wilson Elius, alisema chama hicho kikishika dola kitapunguza
gharama za maisha kwa kila Mtanzania kwa kuondoa tozo mbalimbali.
Aidha, aliwataka wananchi kufuata sheria katika kipindi
chote cha kampeni na uchaguzi ili taifa lisije likajikuta katika matatizo.
MWISHO

Post a Comment