KWANINI VYAMA VYA SIASA HAWAAMINI KUWASIMAMISHA WAGOMBEA WENYE ULEMAVU MAJIMBONI
Na Maryam Nassor
Mwaka huu wa 2025 Tanzania inatarajia kufanya uchaguzi mkuu
wa Rais, Wabunge na Madiwani, na kwa upande wa Tanzania Zanzibar, uchaguzi wa
Rais wa Zanzibar, Wawakilishi na Madiwani utafanyika hapo tarehe 29 Oktoba.
Katika nafasi hizo, kwa hapa Zanzibar, jumla ya vyama 11
vimethibitisha kuwa vitashiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu. Lakini cha
kusikitisha, hadi sasa hakuna ripoti ya mgombea mwenye ulemavu ambaye amegombea
katika majimbo kwa Zanzibar.
Sio kwamba hawataki kugombea nafasi hizo, la hasha, lakini
wengi wao wanadai kuwa upungufu wa elimu ya kisiasa na ukosefu wa sera
shirikishi ndani ya vyama vyenyewe ndiyo sababu inayopelekea wasishiriki katika
kugombea nafasi hizo.
Mitazamo ya Vyama vya Siasa
Nadhra Ali Haji, Mwenyekiti wa Wanawake katika Chama
cha Alliance for Democrats Change (ADC), amesema hawajaweza
kusimamisha mgombea mwenye ulemavu kwa sababu ya mazingira na siasa za
Zanzibar.
Amesema kuwa mazingira ya siasa za Zanzibar ni magumu
wakati wa uchaguzi, kiasi kwamba watu wa kawaida hushindwa kuyamudu, sembuse
watu wenye ulemavu.
“Kiukweli
hatujaweza kusimamisha wagombea wenye ulemavu kutokana na mazingira ya siasa za
hapa kwetu Kipindi cha uchaguzi hali
huwa tete, hivyo ni shida huzidi kwa upande wao,” amesema Nadhra.
Aidha, amesema wanatoa nafasi za viti maalum kwa
mtu yeyote mwenye ulemavu atakayejitokeza kugombea.
Kwa mujibu wa ripoti ya Umoja wa Mataifa ya mwaka 2019,
inasisitiza kwamba demokrasia ya kweli haina maana iwapo sehemu ya jamii
inaachwa nyuma.
“Demokrasia
ya kweli haiwezi kuwa na maana iwapo sehemu ya jamii inaachwa nyuma kwa kigezo
cha ulemavu.” – Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN, 2019).
Katika mazingira ya siasa za Tanzania na Zanzibar, ushiriki
wa watu wenye ulemavu bado unaonekana kuegemea zaidi katika nafasi za viti
maalum na siyo kwenye nafasi za kugombea uongozi wa moja kwa moja katika
majimbo.
Ushirikishwaji Ndani ya Vyama
Tunu Juma Kondo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania
kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM), amesema kuwa chama chao huwa kinahamasisha
watu wote kugombea nafasi za uongozi, wakiwemo wenye ulemavu.
“Chama
chetu cha Mapinduzi tunahamasisha watu wote kugombea nafasi za uongozi.
Hatumbagui mtu kutokana na hali yake, kwani tunaamini kila mtu ni mlemavu
mtarajiwa,” amesema Bi. Tunu.
Naye, Halim Ibrahim kutoka Chama cha ACT-Wazalendo amesema
hawakuweza kusimamisha wagombea wenye ulemavu kutokana na vurugu zinazotokea
wakati wa uchaguzi.
“Hatukuweza
kusimamisha mgombea mwenye ulemavu ingawa tunayo sera ya kuhamasisha watu wenye
ulemavu kugombea katika chama chetu,” amesema Halim.
Aidha, amewashauri watu wenye ulemavu kujitokeza kwa wingi
katika nafasi za viti maalum ambazo hazina misukosuko kama nafasi za
majimbo.
Mitazamo ya Viongozi na Wachambuzi
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake Wenye Ulemavu Zanzibar
(JUWAUZA), Bi. Salma Saadat amesema
changamoto kubwa ni mtazamo hasi wa jamii kuhusu siasa na watu wenye ulemavu.
“Vyama
vingi vinawaona watu wenye ulemavu kama kundi la kupigiwa kura pekee, si
washindani wa kisiasa , Wanaogopa kuwa hawataweza kushinda kutokana na mitazamo
ya jamii,” amesema Bi. Salma.
Amesema hali hiyo hupelekea kundi hili kusalia nyuma licha
ya kuwa na haki sawa kisheria na kijamii kushiriki kikamilifu katika kugombea
nafasi za uongozi.
Aidha, upungufu wa elimu ya kisiasa na ukosefu wa sera
shirikishi ndani ya vyama vyenyewe bado ni changamoto kubwa.
Almas Mohamed, mchambuzi wa masuala ya siasa Zanzibar,
amesema kuwa tatizo kubwa lipo kwenye mfumo wa vyama vya siasa.
“Vyama
vingi vya siasa havijajenga misingi ya kutengeneza mazingira rafiki kwa
wagombea wenye ulemavu, Kuna dhana kwamba mtu mwenye ulemavu hawezi kuhimili
kampeni au majukumu ya ubunge,” amesema Almas.
Ameongeza kuwa changamoto kubwa siyo ulemavu wa mwili, bali
ni ulemavu wa mitazamo ya kisiasa na kijamii.
Akibainisha kuwa
iwapo vyama vya siasa vitabadilisha mtazamo na kuwekeza kwa wagombea wenye
ulemavu, taifa litanufaika kwa viongozi wabunifu na wenye dhamira.
Mtazamo wa Kisheria
Kwa mujibu wa Sheria ya Watu Wenye Ulemavu ya Zanzibar
ya mwaka 2006, pamoja na Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Watu Wenye
Ulemavu (CRPD), watu wenye ulemavu wanayo haki ya kushiriki katika maisha ya
kisiasa na ya umma bila kubaguliwa.
Vifungu vya sheria hizo vinabainisha kuwa kila mtu ana haki
ya kuchagua na kuchaguliwa, kushiriki kampeni, na kuwa sehemu ya maamuzi ya
taifa lake. Kifungu cha 29 cha CRPD kinasisitiza ushiriki sawa wa
watu wenye ulemavu katika siasa na maisha ya umma.
Mwisho
.jpeg)
Post a Comment