Wanawake wahimizwa kujikomboa Kiuchumi na kuwasaidia wengine


NA NUSRA SHAABAN

WANAWAKE wamehimizwa  kujikomboa kiuchumi kupitia biashara ndogo ndogo, ujasiriamali, na mafunzo ya stadi mbalimbali, huku wakitumia fursa hizo pia kuwasaidia wanawake wengine katika jamii zao.

Hayo yamezungumzwa na  Ofisa mradi wa uwezeshaji wanawake na upatikanaji wa msaada wa kisheria kutoka Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA), Mwanaisha Mustafa Makame, huko Katika ukumbi wa Malaria Mwanakwerekwe Unguja.

Mwanaisha alisema ni vyema  wanawake  kushiriki kikamilifu mafunzo hayo ili kuimarisha   hali yao ya kiuchumi.

Alisisitiza kuwa wanawake waliopata mafunzo hayo wanapaswa kutumia  elimu wanayopata, ili kujijengea uwezo wa kiuchumi, kujikomboa kifedha, na kuwa mfano wa kuigwa kwa wanawake wengine katika jamii zao.

“Wanawake ni nguzo muhimu katika maendeleo ya familia na jamii. Tunawaomba mkawe mabalozi wa ujuzi huu, mjikomboe kiuchumi na pia muwasaidie wanawake wengine,” alisema Mwanaisha.

Kwa upande wake, Mratibu wa mradi   kutoka UNDP, Gamaliel Sunu, alibainisha kuwa lengo kuu la mradi huo ni kuwawezesha wanawake wengi zaidi kupata fursa za kiuchumi kupitia mafunzo ya ujasiriamali na msaada wa kisheria.

“Awamu ya kwanza ya mradi kupitia ZAFELA tulifanikiwa kuwafikia wanawake 14. Katika awamu hii ya pili, tumewafikia wanawake 30, na matarajio yetu ni kuongeza wigo hadi Pemba ili wanawake wengi zaidi wanufaike,” alisema.

Aidha, alifafanua kuwa washiriki wamegawanywa katika makundi mawili; kundi la vyakula na kundi la bidhaa nyinginezo, ambapo kila kundi litapewa mbinu mahsusi kulingana na shughuli wanazojihusisha nazo.

Aliongeza kuwa mradi huo, unalenga si tu kuongeza kipato cha wanawake, bali pia kuimarisha nafasi yao katika maamuzi ya kifamilia na kijamii kupitia uelewa wa kisheria na kiuchumi.

Naye Mkufunzi wa mafunzo hayo Maryam Abdallah Hemed, alisema mafunzo hayo yatawasaidia wanawake kujiepusha na utegemezi.

“wapo wanawake ambao  hawana wazo lolote la kufanya na  wapo tu wametulia majumbani, leo hii wamepata fursa hii,  hivyo  itawasaidia kujihusisha na ujasiriamali” alisema Maryam.

Laila Khamis Jumbe, mjasiriamali  wa kutengeneza pilipili za aina zote kutoka Mombasa Zanzibar, alisema mafunzo hayo yatamsaidia kuongeza ujuzi na maarifa ya ujasiriamali ambao utamlipa zaidi.

“Napenda kuwaambia wanawake wenzangu kwamba ujasiriamali unalipa na unapesa, hivyo,tusiudharau” alisema Laila.


Naye Mwanaime Bakari Twaha, mjasiriamali kutoka Jangombe alisema mafunzo hayo ya ujasiriamali yamemsaidia   kupata elimu ya ujasiriamali ambayo hapo awali alikuwa hajaipata.

Aliongeza kuwa matarajio yake  ni kuwa mjasiriamali mkubwa na kuahidi  kuendelea  kuisambaza taaluma aliyoipata kwa wengine.

Aidha, mafunzo  hayo  ya siku tano yaliyofadhiliwa  na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), yamewakutanisha wanawake 30, ambao wameanza kupatiwa mafunzo ya awali ya kutambua fursa za biashara pamoja na mbinu za utunzaji wa fedha.





 

No comments

Powered by Blogger.