JAMII TUWAUNGE MKONO WANAWAKE WALIOJITOKEZA KUGOMBEA NAFASI ZA UONGOZI_ TAMWA ZNZ.


NA MARYAM NASSOR,


 WANANCHI wa  Zanzibar na Tanzania kwa ujumla wametakiwa  kuunga mkono juhudi za wanawake waliojitokeza kugombea nafasi  mbali  mbali za uongozi katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu,  ili kufikia   asilimia 50/50 katika nafasi za uongozi na vyombo vya maamuzi.

 Akifungua mafunzo ya siku tatu Meneja Mawasiliano kutoka Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ) Ndg.Sophia Ngalapi kwa  wagombea wanawake  ambao wamepitishwa na vyama vyao vya siasa kugombea nafasi mbali mbali za uongozi , wakiwemo wa nafasi ya urais, makamo wa rais ,wabunge, wawakilishi na madiwani huko katika ukumbi wa Chama hicho Tunguu Unguja.

Amesema, lengo la mafunzo hayo kwa wagombea hao ni  kuwapa elimu wazidi kujiamini,  kushinda changamoto  na kuongeza ufanishi katika majukwaa ya kampeni na uchaguzi .

 Amesema  kuwa ,  tafiti zinaonesha wanawake wanapokuwa viongozi wanafanya vizuri zaidi katika kuihudumia jamii , ukilinganisha na wenzao  wanaume kutokana na kuwa ni waadilifu, wawazi, wachapakazi lakini pia wanayajua matatizo  yanayowakumba  wananchi.

“ Baada ya kumaliza mafunzo haya ya siku tatu, Imani  yetu kwenu wagombea    muwe mumejifunza   mambo mengi ili muwengeze ufanisi  katika  ngazi zenu  na kushinda changamoto za kwenye majukwaa ya kampeni na uchaguzi kwa ujumla”

 Aidha amesema kuwa,  wao  kama wadau wanajua changamoto zinazowakumba wagombea wanawake   katika  kutafuta nafasi za  uongozi ikiwemo uhaba wa rasilimali fedha, hivyo  wanawapongeza kwa jitihada zao hadi kufikia hapo walipofika.

Nae, mkufunzi wa mafunzo hayo,  Bi. Halima Mselem amewataka wagombea hao kusoma maadili ya uongozi ili wasiende kinyume na maadili hayo.Top of Form

Amesema kuwa,  katika uchaguzi wa mwaka huu wanawake wamejitoa hadi kugombea nafasi ya urais,  si hatua ndogo  hivyo ni vyema kupambana na kufikia malengo yao.

Aidha amesema kuwa, takwimu zinaonesha mwaka huu wanawake 13 wamejitokeza kugombea nafasi ya urais na makamo wa rais  katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Nae,  Afisa  mradi wa kuwawezesha wanawake  katika maswala ya uongozi na haki za kidemokrasia  kutoka Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ)  Sabrina Yussuf amewapongeza wagombea hao kwa kuchaguliwa na vyama vyao kugombea nafasi mbali mbali za uongozi.

 Aidha amewataka  , wanawake hao wanaogombea  nafasi mbali mbali za uongozi kuendelea kupigania malengo yao ili kufanikiwa ,.

 Nao, baadhi ya  wagombea walioshiriki  mafunzo hayo  ya siku tatu  Amana Suleiman Mzee kutoka chama cha  Tanzania Labour Party ( TLP) na  Isha Salim Hamad kutoka chama  cha kijamii ( CCK) wamewashukuru TAMWA ZNZ, kwa kuwapa mafunzo hayo  kwa ajili ya kuwanoa kuelekea kwenye  kampeni na uchaguzi mkuu.

 Mafunzo hayo, ya siku tatu kwa wagombea  wanawake 56  wa Zanzibar kutoka vyama 18 vya siasa  kuelekea  Uchaguzi  Mkuu wa Oktoba mwaka huu, yameandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ)  Jumuiya ya wanawake wenye Ulemavu Zanzibar (JUWAUZA) Chama cha Wanasheria Wanawake Zanzibar ( ZAFELA) na PEGAO .

                             MWISHO

Bottom of Form

 

No comments

Powered by Blogger.