UMUHIMU WA VITUO VYA HUDUMA RAFIKI KWA VIJANA



NA MARYAM NASSOR

Vijana ndiyo nguzo kuu ya maendeleo ya taifa lolote  duniani. Hata hivyo changamoto zao za kiafya, kijamii na kimaadili mara nyingi zimekuwa hazipewi kipaumbele cha kutosha.

 Ili kujibu changamoto hizo, serikali na wadau wa maendeleo wameanzisha vituo vya huduma rafiki kwa vijana, ambavyo vina lengo la kutoa msaada, ushauri na huduma za kiafya, kisaikolojia na kielimu kwa njia inayowafaa vijana.

 Vituo hivi vimekusudiwa kuwa mahali salama kwa  vijana ambapo wanaweza kupata huduma bila hofu ya hukumu, unyanyapaa au masharti magumu.

Lakini licha ya kuwepo vituo hivyo   vya huduma  rafiki kwa vijana, jee vijana wana elewa umuhimu wa vituo hivyo na jamii imevipokeaje  kwa ujumla.

  Akizungumza na   mwandishi wa Makala hii,Msimamizi wa kituo cha Huduma Rafiki kwa Vijana  kilichopo Mahonda  Wilaya ya Kaskazini ‘B’ Unguja  Mansour Abdalla Ali , amesema  lengo la  kuanzishwa  vituo hivyo,  ni kuwafikia vijana kuwapa elimu ya Afya ya uzazi, elimu ya Saikolojia  na elimu ya kutosha kuhusu  Ukimwi.

Amesema kuwa,  kituo hicho cha Wilaya ya Kaskazini ‘B’   kinawahudumia  wakaazi wapatao  99,921 kwa shehia 21 zilizopo katika wilaya hiyo.

Aidha amesema kuwa, Vituo vya huduma rafiki kwa vijana ni nyenzo muhimu ya maendeleo ya taifa. Kupitia vituo hivyo, vijana hupata msaada wa kiafya, kielimu na kisaikolojia, jambo linalowasaidia kuwa raia wenye afya bora na maamuzi sahihi kwa maisha yao ya sasa na baadaye.

“ Kupitia vituo hivi vya huduma rafiki kwa vijana ni sehemu salama kwao , ambapo wakifika wanapata msaada wa matatizo yao ya kiafya hata ya makuzi na saikolojia , hivyo tunawaasa wavitumie kutatua shida zao zinazowakabili “ ameshauri Mansour.

 

Umuhimu wa vituo hivi kwa vijana
 Harith Ali (23) mkaazi wa kinduni wilaya ya kaskazini “B’ Unguja amesema , Vituo vya huduma rafiki kwa vijana  vina nafasi ya kipekee katika maisha ya vijana, Kwanza  vinatoa huduma za afya ya uzazi na ushauri juu ya maambukizi ya magonjwa ya ngono pamoja na virusi vya Ukimwi.

 

“ Vituo hivi  vinatusaidia vijana kupata elimu sahihi juu ya lishe, afya ya akili na namna ya kukabiliana na changamoto za makuzi” amesema Harith.

 

 Amesema  kuwa, kupitia vituo hivyo  vijana  vinawawezesha kupata msaada wa kisaikolojia pale wanapokumbana na msongo wa mawazo au matatizo ya kifamilia,vituo hivi vimekuwa daraja la kuwajengea vijana ujasiri na maarifa ya kufanya maamuzi bora kwa mustakabali wao.

 

Asha Makame (31) mkaazi wa Donge, wilaya ya Kaskazini ‘B’ Unguja, amesema Serikali imethibitisha dhamira yake ya kuendeleza huduma hizo, lakini bado kunahitajika juhudi za pamoja kuhakikisha jamii nzima inavipokea kwa mtazamo Chanya vituo hivyo.

 Amesema kuwa, Ili kufanikisha malengo yake,  lazima kuwepo kwa kampeni endelevu za uhamasishaji, ushirikiano wa karibu na wazazi pamoja na uboreshaji wa rasilimali katika vituo  hivyo.

“Bila shaka iwapo vitatumiwa ipasavyo  vituo hivi vitakuwa nguzo ya ustawi wa vijana na maendeleo ya taifa kwa ujumla kwa  kuwaelimisha vijana  na kuwakinga na matatizo mbali mbali ya kiafya kwa kupata elimu’’. Amesema.

 

Kauli ya Serikali

Serikali kwa upande wake  kupitia Waziri wa Afya Zanzibar  Nassor Ahmed Mazurui , amekuwa akisisitiza umuhimu wa vituo hivi kama mkakati wa kitaifa wa kupunguza changamoto za vijana na  hatua za kupambana na maradhi ya Ukimwi.

 

 Aidha amesema kuwa, Serikali imekuwa ikihimiza kuanzishwa kwa vituo zaidi na kutoa miongozo ya utoaji huduma rafiki, kwani  inatambua kuwa vijana wana haki ya kupata taarifa na huduma za afya bila vikwazo, jambo linaloendana na sera za vijana na malengo ya maendeleo endelevu (SDGs).

 

Mapokezi ya jamii


 Fatma Hussein (45) mkaazi wa Mahonda  wilaya ya Kaskazini ‘B’ Unguja  amesema ,Jamii kwa ujumla imepokea vituo hivi kwa mitazamo tofauti.

 

Amesema,  Wapo wazazi na walezi wanaona vina faida kubwa katika kulea vijana walio salama na wenye maarifa. Hata hivyo, changamoto zipo nyingi.

 

Juma Makame, amesema  Baadhi ya watu wanaona vituo hivi kama njia ya kuhalalisha tabia zisizofaa, hususan pale vinapohusiana na elimu ya afya ya uzazi.

 

 Amesema  kuwa, Hali hii mara nyingine husababisha vijana kujikuta bado wakikosa uungwaji mkono wa kutosha kutoka kwa kwa jamii na familia zao kwa ujumla.

  

 Je, vinatumika kama ilivyokusudiwa?
Utafiti unaonesha kuwa licha ya umuhimu wake, si vijana wote wanaotumia vituo hivi kama ilivyokusudiwa. Sababu kuu ni ukosefu wa uelewa, hofu ya unyanyapaa, umbali wa vituo na wakati mwingine upungufu wa wataalamu waliobobea katika kushughulikia  changamoto za vijana.

Hata hivyo, katika maeneo ambayo elimu imetolewa vya kutosha na jamii kushirikishwa, matumizi ya vituo hivi yamekuwa makubwa na yameonesha mafanikio ya kupunguza changamoto zinazowakabili vijana.

 Ripoti mpya ya Shirika la Umoja wa Mataifa  la Afya Ulimwenguni (WHO) imesema  kunahitajika  uwekezaji wa kutosha na wa haraka  wakukabiliana  na changamoto za kiafya kwa vijana unaoongezeka.

Kuhakikisha  mahitaji ya Afya ya akili, afya ya uzazi na afya ya ngono kwa vijana  bilioni 1.3 duniani kote yanatimizwa, kulingana na ripoti hivyo ujana ni hatua ya kipekee na muhimu katika maendeleo ya binadamu ambapo  misingi ya  afya bora ya muda mrefu huwekwa.

                                   Mwisho

 

 

 

 

                                        

 

 

 

 

 

 

No comments

Powered by Blogger.