WAANDISHI WA HABARI WATAKIWA KUTETEA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU
NA MARYAM NASSOR
WAANDISHI
wa Habari nchini wametakiwa kutumia kalamu zao,
kuibua na kutetea haki za watu wenye ulemavu ili kuongeza ushirikishwaji
wao katika kila Nyanja za maendeleo.
Kauli hiyo, imetolewa na Afisa program wa
mradi huo, Khairat Haji kutoka Chama cha
waandishi wa Habari wanawake Tanzania
Zanzibar (TAMWA ZNZ) wakati wa mafunzo
ya siku tatu kwa waandishi wa Habari huko katika Afisi za chama hicho Tunguu
Unguja.
Amesema,
wandishi wa Habari wana nafasi nzuri ya kuleta mabadiliko katika jamii kupitia
kalamu zao, hivyo ni vyema
kuhakikisha kuwa watu wenye ulemavu wanasikika , wanaonekana na kushirikishwa
katika mijadala ya kitaifa.
Amesema kuwa,
Mafunzo hayo yanalenga kuondoa pengo la muda mrefu la vyombo vya Habari kuripoti maswala ya
watu wenye ulemavu kwa mtazamo
tofauti kama kuwaonea huruma
badala ya haki na usawa .
“ Waandishi wa Habari wana nguvu za kubadili mitazamo na fikra za wanajamii lazima tuondokane na uwandishi wa kimazoea unaowaonesha watu wenye walemavu kama omba omba au wanahitaji matibabu na badala yake tuwaoneshe kama watu wenye nguvu na uwezo wa kupambana “ ameshauri Khairat.
Akiwasilisha
mada katika mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Jumuiya ya wanawake wenye ulemavu Zanzibar ( JUWAUZA) Bi
Salma Saadat amesema, hali ya ulemavu Zanzibar inaongezeka kuliko
Tanzania bara kutokana na sababu nyingi ikiwemo ugonjwa wa utapiamlo na ajali za barabarani.
Aidha alisema kuwa, asilimia 50 ya hali ya ulemavu inatokana na umasikini, huku asilimia 20 ni matokeo ya utapiamlo ambao huwakumba Watoto wengi kutokana na lishe duni.
“ Lengo la
mafunzo haya kwa waandishi wa Habari wawe mabalozi wazuri wa kuzitetea haki za watu
wenye ulemavu na ujumuishwaji katika kila sekta ya maendeleo “ amesema Bi
Salma.
Nao, baadhi
ya waandishi wa Habari walioshiriki mafunzo hayo, Berema Nassor
na Samira Abdallah wamesema mafuzo hayo yamewasaidia kubadili mitazamo
yao, ya kuwaona watu wenye ulemavu kama omba omba au wanahitaji matibabu.
Wamesema
kuwa, baada ya kupata elimu hiyo, wameacha kuwaona watu
wenye ulemavu kama watu wasio weza kitu
na wanahitaji huruma na badala yake wanawaona ni watu wenye uwezo
ambao wanahitaji kuwezeshwa.
Mafunzo hayo, ya siku tatu kwa waandishi wa Habari 20 wa Unguja yameandaliwa na TAMWA ZNZ kwa kushirikiana na SHIJUWAZA, ZANAB, MECP-Z na Baraza la Taifa la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar kwa lengo la kupaza sauti za watu wenye ulemavu na ushirikishwaji kupitia vyombo vya Habari.
Post a Comment