TAMWA ZNZ KUADHIMISHA SIKU YA REDIO DUNIANI KWA KUWAKUTANISHA WADAU WA HABARI.


NA MARYAM NASSOR,

CHAMA cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ)  kimeeleza dhamira yake ya kuitumia siku ya Kimataifa  ya Redio kama jukwaa la kutathimini mchango wa redio katika maendeleo ya jamii, hususani dhidi ya mapambano ya mabadiliko ya tabianchi.

 Katika kuadhimisha  siku  hiyo ,TAMWA ZNZ   inatarajia kuwakutanisha  wadau  mbali mbali wa  Habari kutoka  sekta ya  Habari  kwa Unguja na Pemba, wakiwemo  viongozi wa vyombo vya Habari,wahariri, wakuu wa vipindi , wandishi wa Habari  na viongozi  wa vyombo vya Habari kwa lengo la kujadili  nafasi ya redio  katika kuelimisha na kuchochea  mijadala kuhusu  mabadiliko ya tabianchi.

Kwa Mujibu wa Mkurugenzi wa TAMWA ZNZ, Dkt Mzuri Issa, kauli mbiu ya mwaka huu” Redio na Mabadiliko ya Tabianchi” inalenga  kuhamasisha  vyombo  vya Habari kutumia redio kama nyenzo ya kuelimisha jamii kuhusu athari za mabadiliko  ya Tabianchi na njia za kukabiliana nazo.

TAMWA ZNZ inasema kuwa, licha ya umuhimu wa redio katika kufikisha taarifa, tafiti  zinaonesha  kuwa redio bado haijatumika  ipasavyo kuzungumzia maswala ya tabianchi , utafiti  uliyofanya mwaka 2024 na chama hicho umebaini  kuwa kati ya vipindi 2,600 vilivyorushwa na ZBC na Assalam Radio ni vipindi  11 pekee (asilimia 0.9)vinavyohusu  mabadiliko ya tabianchi.

“Tafiti zinaonesha  kuwa sauti za wanawake hazipewi nafasi ipasavyo katika mijadala ya tabianchi,  hivyo tunaomba  redio na vyombo vya Habari vyengine  kuandika zaidi kuhusu  wanawake  na nafasi yao katika kupambana na mabadiliko ya tabianchi” amesema Dkt Mzuri.

Kwa mujibu wa TAMWA ZNZ,  Redio ina nafasi  muhimu katika kuelimisha  jamii  kuhusu athari za mabadiliko  ya tabianchi, kuhimiza matumizi ya mbinu endelevu za kilimo, uhifadhi wa mazingira, na kupunguza uchafuzi wa mazingira.

Mbali na suala la tabianchi, TAMWA ZNZ inasisitiza  kuwa redio  inaendelea  kuwa chombo  Madhubuti cha kupigania  haki za wanawake  na Watoto, usawa wa kijinsia   na ushiriki  wa wanawake katika uongozi.

 Katika mwaka 2024 pekee, TAMWA ZNZ ilichapisha Habari 778 kupitia  vyombo mbali mbali    vya Habari zikiwemo 101 kwenye redio, Habari hizo  zilihusu  maswala kama vile udhalilishaji wa kijinsia , Afya  ya uzazi, wanawake  katika uongozi na uhuru wa Habari.

TAMWA ZNZ inatoa  shukrani kwa vyombo vya Habari kwa mchango wao mkubwa katika kuhakikisha jamii inapata taarifa  sahihi kwa wakati, chama hicho kinapongeza juhudi za redio kufikisha ujumbe kwa jamii, hasa katika maeneo  ya pembezoni  ambapo  vyombo vingine vya Habari  vinafika kwa ugumu.

Siku ya Kimataifa ya redio huadhimishwa Febuary  13 kila mwaka tangu  ilipotangazwa  rasmi na UNESCO mwaka 2011 na kupitishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa  mwaka 2013, TAMWA ZNZ inazitakia redio zote madhimisho mema na mafanikio  katika mipango yao ya baadaye.

No comments

Powered by Blogger.