“Majukumu ya nyumbani sio kikwazo tena kwa wanawake kugombea uongozi”

Na Maryam Nassor,Zanzibar

Tanzania  ni miongoni mwa nchi zilizoridhia  mikataba mbali mbali ya kikanda na kimataifa ya kuondoa  aina zote za ubaguzi dhidi ya wanawake, kama mkataba wa Cedaw ambao umeanzishwa  mwaka 1987 na kuheshimu haki za wanawake kama haki za binaadamu.

Licha ya kuwa katiba ya nchi inatambua haki za raia wote, bado wanawake kama walivyo raia wengine, hawajui haki zao na namna ya kuzitafuta  hii inatokana  na  sheria kuandikwa kwa lugha ya  kigeni na  ya kisheria.

 Katika ulimwengu wa sasa suala la usawa wa kijinsia, limekuwa suala muhimu  sana hasa linapozungumziwa ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi na vyombo vya maamuzi.

Miongoni  mwa mambo yanayowarudisha nyuma wanawake katika kugombea nafasi za uongozi  ni mifumo dume, mila na desturi lakini pia  mgawanyo wa majukumu kijinsia jambo ambalo kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka huu  2025 wanawake wamejipanga, na majukumu ya nyumbani sio kikwazo tena  kwa wanawake kugombea nafasi za uongozi.

Pavu  Juma Abdallah Naibu Katibu Mkuu wa  haki za Binadamu kutoka Chama cha ACT Wazalendo , ambae alishawahi kugombea nafasi mbali mbali katika chama hicho Ni mmoja wa wanawake wanao ona  kuwa, majukumu ya nyumbani sio kikwazo tena kwa wanawake  kuwa viongozi.

Amesema kuwa,  kwenye siasa kuna changamoto nyingi zinazowakumba wanawake  ikiwemo ukosefu wa fedha za kujikimu wakati wa kampeni lakini majukumu ya nyumbani hawayachukulii tena kama kikwazo cha wao, kushiriki na kugombea nafasi za uongozi,”majukumu ya nyumbani sihisi kama ni kikwazo kwani nilazima ujipange vizuri katika majukumu  na mikakati yako” amesema bi Pavu.

Amesema kuwa, kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka huu ni vizuri wanawake kugombea katika majimbo nafasi mbali mbali za uongozi ikiwemo udiwani, uwakilishi na ubunge kwani huko bado kuna upungufu wa wagombea wanawake” mwaka huu ni mwaka wa uchaguzi mkuu  wanawake tuwe na mikakati yetu na tujipange zaidi kila kwenye chanagamoto basi tuzichukulie kama fursa” ameshauri   bi Pavu.

 Maryam   Ali Mussa diwani wa viti maalum  kutoka Chama cha Mapinduzi – CCM amesema kuwa majukumu ya nyumbani ni mujibu kwa mwanamke mfano mzuri ni kwa mama Samia yeye ni Rais lakini tunamuona  siku anayokuwa na muda anaingia jikoni anapika kwasababu  ni kazi za mwanamke ,” kazi za nyumbani  tunafundishwa tokea tuko wadogo majumbani kwetu vipi ziwe kikwazo kwetu zitufanye tusishiriki katika kugombea nafasi za uongozi ambazo ni haki yetu ni kujipanga tu” amehoji Maryam.

Amesema  kuwa,  hayo sio kikwazo tena kwa wanawake  kwani upo mfano mzuri Tanzania wa rais mwanamke  ambae amejipanga hadi kufika pale,  kuelekea uchaguzi mkuu ni muhimu wanawake wakawa na uthubutu kujitupa majimboni kugombea nafasi mbali mbali za uchaguzi ili kuongeza ushiriki wao. Wanawake katika uongozi sio tu sauti za mabadiliko, bali ni chachu ya kufikia dunia yenye usawa na matumaini

Sensa ya watu na makaazi ya mwaka 2022 inaonesha Zanzibar ina watu  milioni 1.8 kati ya hao wanaume ni 915,492 na wanaake ni 974, 281, hii inamanisha  kwamba wanawake ni asilimia 51.6 ya wakaazi wote wa Zanzibar lakini wingi wao huo hauonekanikatika nafasi za uongozi.

   Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania- UWT kwa upande wa Zanzibar kutoka chama cha Mapinduzi  -CCM Tunu Juma Kondo  amesema ,Licha ya wanawake kuwa ni wengi bado kumekuwa na upungufu  wa wanawake kushiriki katika nafasi za uongozi kutokana na    hapo awali  wengi wa wanawake walikuwa hawajui kuwa kugombea  nafasi za uongozi ni haki yao na walikuwa wanadhani kuwa nafasi zile zipo kwa ajili ya wanaume tu.

 Akizungumzia kuhusu majukumu ya nyumbani kwa wanawake amesema sio kikwazo kabisa, kwani  wapo watu ambao ni wafanyakazi  wanaenda kazini lakini wakirudi nyumbani wanaihudumikia  familia na hawaoni kama ni kikwazo,” Tunatakiwa tujipange   kufanya majukumu yetu ya  nyumbani  lakini pia tushiriki katika nafasi mbali mbali za uongozi ili kuongeza  ushiriki wetu kwani ni haki yetu kugombea” ameshauri Tunu.

Amesema kuwa, takwimu zinaonesha  wanawake wapo kidogo katika nafasi za uongozi Hali hiyo inaonesha   haja ya wanawake kuongezeka  katika nafasi za uwakilishi  katika majimbo,  ifikapo  uchaguzi wa mwaka  huu 2025, kwani idadi ya  wanawake ni kidogo katika majimbo.

Kwa mujibu wa takwimu  kutoka baraza la wawakilishi Zanzibar (BLW)  idadi  ya wajumbe wote ni 78 kati yao wanawake ni 29 na wanaume 48, huku wanawake wawakilishi wa majimbo kupitia uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 ni wanne tu, wanaume wakiwa 42 na wanawake wa viti maalum ni 18 na wajumbe waliobakia ni nafasi za kuteuliwa na Rais.

Naibu Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Anna Athanas Paul, amesema tathimini iliyofanywa na wizara hiyo, katika taasisi mbali mbali imeonesha kuwa wanawake bado wapo kidogo katika nafasi za Uongozi, ukilinganisha na wanaume jambo ambalo linahitaji kuangaliwa. ‘’Takwimu zilizokusanywa na wizara kutoka taasisi mbali mbali kwa mwezi machi mwaka 2024, zinaonesha ni asilimi 30 tu ya wanawake ambao wako katika  uongozi, ukilinganisha na wanaume ambao ni asilimia 70’’ Amesema Naibu Waziri Anna.

Anna, ameongeza kuwa Serikali inaendelea na jitihada katika kufikia malengo yaliyowekwa kupitia Dira ya 2050 na mpango wa Maendeleo (ZADEP) 2021/2026 ambapo lengo katika nafasi za uongozi ni kufikia 50/50. “ Serikali imejipanga kuhamasisha  ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi na vyombo vya maamuzi na  lengo ni kufikia 50/50” amesema Anna.

 

Mohamed Ali Ahmed, ni Naibu Msajili wa vyama vya Siasa Tanzania ,kwa upande wa Zanzibar, amesema kuongezeka kwa kifungu cha 10 C ndani ya sheria ya vyama vya siasa nchini, kinatoa nafasi kwa wanawake kuongeza ushiriki wao ,na kuwajibika kwa vyama ,kwa kuwa na sera ya jinsia muda wote kwani hapo awali havikupaswa vyama  kuwa na sera hiyo.”amemaliza naibu msajili huyo .

 

                                             MWISHO

 

 

 

 

 

 

 

No comments

Powered by Blogger.