WANAWAKE WAMETAKIWA KUWA VIONGOZI KATIKA KUKABILIANA NA MABADILIKO YA TABIANCHI


NA MARYAM NASSOR,

WANAWAKE wa shehia nne za Unguja waliyopatiwa mafunzo na Jumuiya ya Community Forest Pemba,(CFP) wametakiwa kuwa viongozi katika kulinda Mazingira ,kwa kupanda mikoko ili kujilinda na madhara ya  mabadiliko ya Tabianchi.

Ameyasema hayo, Mkurugenzi wa Jumuiya hiyo, Mbarouk Musa Omar, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari huko, katika  Ukumbi wa Tamwa Tunguu Unguja.

Amesema  kuwa, lengo la mradi huo ni  kuwafanya wanawake kuwa viongozi  katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kupanda mikoko, na kulima kilimo msitu ili kushiriki kikamilifu katika kutunza mazingira.

Aidha amesema kuwa, kupitia mradi huo wa ZanziAdapt, wametoa elimu na miche mbali mbali ya matunda na misitu ya  muda mfupi na mrefu , katika kukabiliana na Mabadiliko ya tabianchi na kuifanya Zanzibar  kuwa ya kijani.

“Sisi Jumuiya ya Commuity Forest Pemba, tumeitikia kwa vitendo wito, wa Rais wa Zanzibar wa kuifanya Zanzibar iwe ya kijani na bado tunaendelea kuhamasisha jamii kutunza mazingira’’ amesema Mkurugenzi Mbarouk.



 Shaban Peter Majo, ni Afisa Teknolojia ya uzalisaji wa kilimo katika mradi huo, amesema mradi huo umewafikia wanufaika wa moja kwa moja elfu nne ambao ni shehia nne za Unguja na Shehia nne Pemba.

Amesema kuwa, lengo kuu la kutoa mafunzo kwa wanawake wa shehia hizo ni kuinua kipato cha kina mama, kwa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

‘’ Tumefanikiwa kuwafikia wanawake zaidi ya asilimia 80, katika vijiji hivyo na tayari wameanza kunufaika na mradi huu’’ amesema Peter.

Nae, Mtoro Simai Vuai mkaazi wa kijiji cha Bungi, Mkoa wa Kusini Unguja, amesema mafunzo waliyoyapata kutokana na mradi huo. yamewasaidia kulima tena kwani walikuwa wameacha kutokana na mabadiliko ya tabia nchi.

Amesema kuwa,  katika shehia yao, wananchi walikuwa wanakata mikoko kwa ajili ya kuni na mkaa, na kusababisha madhara ya mabadiliko ya tabianchi, lakini baada ya kupata mafunzo hayo, wanawake wako mstari wa mbele katika kulinda mikoko na kutunza Mazingira.

‘’ Wanawake sasa tumejitolea katika kutunza Mazingira kwa kupanda miti ya mikoko na kulima kilimo msitu, ambacho ni himilivu kwa Mabadiliko ya tabianchi’’ amesema.

Mradi huo, wa Mabadiliko ya tabianchi (ZanziAdapt) unatekelezwa  na shirika  la Misitu Duniani (CFI)  Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ)  na Jumuiya ya Community Forest Pemba,(CFP)  kwa Unguja unatekelezwa katika shehia nne za Uzii, Ng’ambwa, Bungi na Unguja Ukuu.

No comments

Powered by Blogger.