MICHEZO HUIMARISHA AFYA NA TIBA MUJARABU KWA MAGONJWA YASIYOAMBUKIZA



NA MARYAM NASSOR,

MICHEZO  ni fursa, ni ajira na  huimarisha afya, inaaminika duniani kote  kuwa, michezo  ni tiba mujarabu kwa magonjwa yasiyoambukizwa  ambayo ni tishio kwa afya za binaadamu.

Michezo   hupunguza uwezekano wa kupata magonjwa
yasiyoambukizwa  kama vile saratani, kisukari, magonjwa ya moyo , shindikizo la juu la damu na huzuia  uwezekano wa kupata kiharusi ( stroke).

Magonjwa yasiyoambukiza (NCDs) yanachangia takribani ya asilimia 33 % ya vifo vyote  nchini, huku  takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa mwaka 2020 zinaonesha kuwa magonjwa hayo  yalichangia  zaidi ya vifo milioni 41 sawa na asilimia 71% ya vifo vyote Duniani ukilinganisha na vifo  milioni 57 kwa mwaka 2016.

Waziri wa Afya wa Zanzibar Nassor Ahmed Mazrui, alipokuwa akizindua utafiti wa kitaifa wa viashiria  vya magonjwa yasiyoambukizwa, katika ukumbi wa mikutano mjini Dodoma.

Alisema kuwa, takwimu zinaonesha kuwa magonjwa yasiyoambukizwa, yameongezeka  mara 5 hadi 9 zaidi kati ya miaka  ya 80, ambapo yalikuwa ni asilimia 1 tu, kwa watanzania waliokuwa na kisukari ni asilimia 5.  lakini kwa sasa  tatizo la kisukari limefikia asilimia 9 , wakati shindikizo la juu la damu limeongezeka hadi kufikia asilimia 25.

“Takwimu hizo zote, tumekusanya kutoka kwenye vituo vyetu vya kutolea huduma za kiafya nchini, ambazo  zinaonesha ongezeko kubwa sana la magonjwa hayo” amesema Waziri  Mazrui.

Aidha amesema kuwa, katika kukabiliana na  ongezeko la magonjwa hayo, Serikali inaongeza vituo vya afya na kutoa elimu kwa jamii  kuhusu namna bora ya kujikinga na magonywa hayo  Pamoja na kuimarisha  mifumo ya utoaji wa huduma za afya nchini.

 Aidha alishauri jamii kubadili mtindo wao wa  Maisha, na kujenga tabia ya  kula mlo kamili  na kufanya mazoezi ili kujikinga  na magonjwa yasiyoambukizwa.

  Nae, Makamo wa kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe, Othman Massoud Othman,  hivi karibuni alipokuwa akifungua bonanza la  michezo kwa wote  la Pemba Fitness Club kwa kushirikiana na Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake  Tanzania Zanzibar ( TAMWA ZNZ)  huko katika uwanja wa  Gombani amewataka wananchi kufanya mazoezi na  kushiriki michezo mbali mbali  ili kuipunguzia gharama Serikali ya kuagiza dawa za matibabu ya magonywa yasiyoambukizwa, na familia katika kutafuta  fedha kwa ajili ya gharama za matibabu.

“ Serikali imekuwa ikitumia Fedha nyingi kuagiza dawa nje ya nchi, kwa maradhi yasiyoambukizwa, hivyo ipo haja kwa jamii kubadili mtindo wa Maisha kwa kula vyakula vyenye afya na kufanya mazoezi” ameshauri Makamo wa kwanza wa Rais.

Katika bonanza hilo, aliwataka wanamichezo wa Club hiyo na jamii  kwa ujumla kuwa na mazoea ya kufanya mazoezi, kwani  kuna athari nyingi za kutokufanya mazoezi   ikiwemo kuongezeka uzito wa mwili na  kusababisha udhaifu katika msukumo wa damu.

Nasra Juma Mohamed ni Naibu kamishna wa Timu ya Uhamiaji Zanzibar na kocha wa Mpira wa Miguu, amesema ipo haja Kwa  wanajamii kushiriki michezo mbali mbali kwani michezo ni tiba.

Amesema kuwa, mtu anae shiriki michezo afya yake inakuwa tofauti na yule asiyeshiriki michezo, kwani michezo ni tiba kwa magonjwa mbali mbali yasiyoambukizwa.

 “Sisi wana michezo tunakuwa na afya mzuri ukilinganisha na watu wasioshiriki michezo, yale magonjwa ya mara kwa mara  ya kuumwa na miguu au Presha yanatuepuka kutokana na kuushughulisha mwili   “ amesema Kocha Nasra.

Aidha ameitoa  wito  kwa jamii, kushiriki michezo mbali mbali ili kuimarisha afya zao na kujikinga  na maradhi yasiyoambukiza.

Hija Mohamed Ramadhan mshauri katika maswala ya jinsia katika michezo, katika mradi wa michezo kwa maendeleo, unaofadhiliwa na shirika la Ujerumani nchini Tanzania (GIZ) amesema mradi huo una lengo la kujenga viwanja saba vya michezo, vinne Unguja na vitatu Pemba hivyo vitawarahisishia jamii kushiriki michezo.  

 Programu ya michezo kwa maendeleo, inatekelezwa na TAMWA ZNZ, ZAFELA na Center for Youth Dialogue (CYD) kwa kushirikiana na Deuth Gesellschaft fur intenational Zusammenrbeit (GIZ) shirika la Ujerumani ikiwa na lengo la kuhamasisha waandishi wa habari kuandika habari za michezo na ushiriki wa wanawake katika michezo.

 

   

 

No comments

Powered by Blogger.