MIFUMO DUME INAVYOWATESA WANAWAKE KATIKA VYAMA VYA SIASA

 




NA MARYAM NASSOR

“Niliingia katika siasa kwa sababu, niliona maswala mengi ya wanawake hayaingii kwenye sera mipango na bajeti kwa kuwa, nafasi nyingi za maamuzi  zimeshikiliwa na wanaume.”

   Hii ni kutokana  na kushamiri kwa mifumo dume katika vyama vya Siasa nchini “nilitamani kuingia kwenye  uongozi kufanya jambo la ziada  kwa  kuhakikisha masuala yanayohusu wanawake na makundi mengine, yanaingia kwenye sera, mipango na bajeti, binafsi  niliamini  kila mwanamke ni kiongozi, anahitaji tu uthubutu na kuamua kushika hatamu” amesema Lucy .

Lucy John Mtembo, 40 ni miongoni mwa  wanachama hai wa Chama cha Mapinduzi -CCM na  Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Tanzania -UWT Mkoa wa Kaskazini Unguja.  alianza  harakati za siasa miaka ya 2010, ambapo enzi hizo nafasi za uongozi kama udiwani, Uwakilishi na Ubunge ulikuwa unashikiliwa na mfumo dume, na wanawake walikuwa ni wapiga debe tu,katika kampeni.“ Katika maisha nimejifunza kuwa tunapaswa kuwa na uthubutu na utayari kujifunza mambo mapya na kujiwekea mipango inayotekelezeka ili tuwe viongozi wazuri”  amesema Lucy akionesha msisitizo.

 Mwenyekiti huyo, wa Umoja wa Wanawake Tanzania, kupitia Chama cha Mapinduzi -UWT, chama ambacho hujinasibu kuwepo kwa usawa wa kijinsia wa viongozi wake kwenye uwakilishi  amesema bado wanawake wapo kidogo katika nafasi za uongozi na vyombo vya maamuzi.” Sisi wanawake tuko wengi kuliko wanaume,lakini  huu wingi wetu hauakisi bado katika nafasi za  uongozi  na  vyombo vya maamuzi” amesema Lucy.

Licha ya Tanzania na Zanzibar kuridhia mikataba na matamko mbali mbali ya kikanda na kimataifa, yenye wito wa usawa katika uwakilishi na ushiriki wa wanawake na wanaume katika siasa, wanawake bado wana uwakilishi mdogo katika  vyombo vya maamuzi na nafasi za uongozi, na  baadhi ya sababu zinazochangia hali hii zimetajwa  ni  mfumo dume, mitazamo hasi ya kibaguzi na mgawanyo wa majukumu kijinsia.

Takwimu zinaonesha Zanzibar, hadi sasa kuna wanawake nane tu, waliowahi kugombania nafasi za uongozi majimboni, ambao walishinda uwakilishi, wanawake 18 walipata uwakilishi kupitia nafasi za viti maalum na hivyo, kufanya idadi ya wanawake katika Baraza la Wawakilishi kuwa 29 kati ya 77 waliyochaguliwa sawa na asilimia 40.

Fatma Abdul Habib Ferej ni Mwenyekiti wa Ngome ya wanawake wa Chama Cha ACT Wazalendo , ambae aliwahi  kushika nafasi mbalimbali za uongozi katika serikali ya Mapinduzi Zanzibar, amesema  bado wanawake wako kidogo katika nafasi za uongozi jambo ambalo linahitaji kuangaliwa. “ Licha ya Serikali kukubali mikataba mbali mbali ya kikanda na kimataifa , ya kuhamasisha usawa wa kijinsia  katika nafasi za uongozi  na  vyombo vya maamuzi lakini bado,  ushiriki wa wanawake haujaridhisha” amesema  Mwenyekiti  huyo wa ngome ya Act Wazalendo.

Amesema katika chama chake cha Act Wazalendo, wana mabaraza ya wanawake na kamati  kuu ya chama, ambayo yana ushiriki wa wanawake kwa asilimia 52 ya washiriki wote.“ushiriki sawa wa wanawake katika kufanya maamuzi hauhitaji haki au demokrasia tu, bali nilazima uonekane kama sharti  muhimu la msingi  ili maslahi ya wanawake yazingatiwe. “ amesema  Mwenyekiti wa Ngome ya Act Wazalendo.

Naibu Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Anna Athanas Paul, amesema tathimini iliyofanywa na wizara hiyo, katika taasisi mbali mbali imeonesha kuwa wanawake bado wapo kidogo katika nafasi za Uongozi, ukilinganisha na wanaume jambo ambalo linahitaji kuangaliwa.

‘’Takwimu zilizokusanywa na wizara kutoka taasisi mbali mbali kwa mwezi machi mwaka 2024, zinaonesha ni asilimi 30 tu ya wanawake ambao wako katika  uongozi, ukilinganisha na wanaume ambao ni asilimia 70’’ Amesema Naibu Waziri Anna.

Anna, ameongeza kuwa Serikali inaendelea na jitihada katika kufikia malengo yaliyowekwa kupitia Dira ya 2050 na mpango wa Maendeleo (ZADEP) 2021/2026 ambapo lengo katika nafasi za uongozi ni kufikia 50/50. “ Serikali imejipanga kuhamasisha  ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi na vyombo vya maamuzi na  lengo ni kufikia 50/50” amesema Anna.

Ripoti ya sensa ya watu na makaazi ya Tanzania ya mwaka 2022, inaonesha  kuwa Zanzibar ina wakaazi milioni 1.8 kati ya hao wanaume  ni 915,492 na wanawake ni 974,281.hii ina maana kwamba  wanawake ni asilimia 51.6 ya wakaazi wote wa Zanzibar, lakini wingi huo hauonekani katika nafasi za uongozi.

Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar, - TAMWA ZNZ ni Taasisi isiyo ya kiserikali, inayojishuhulisha na maswala ya utetezi wa haki za mtoto wa kike na kuhamasisha wanawake kushiriki katika nafasi za uongozi, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA ZNZ, Dk Mzuri Issa amesema  katika vyama vingi vya siasa nchini, vimetawaliwa na mfumo dume jambo ambalo linawarudisha nyuma  wanawake kugombea  nafasi za uongozi.

”Wanawake wenye nia ya kugombea wasivunyike moyo na wawe majasiri ili kuongeza wingi wao katika nafasi za uongozi mwaka 2025 ili kufikia ile 50/50 tunayoitaka ” Amesema Dkt Mzuri .

Naibu Msajili wa vyama vya Siasa Tanzania, kwa upande wa Zanzibar Mohamed Ali  Ahmed, amesema kuongezwa kwa kifungu cha 10 C ndani ya sheria ya vyama vya siasa nchini, kinatoa nafasi kwa wanawake kuongeza ushiriki wao” Kutokana na kuongezwa kwa kifungu hicho, vyama vya siasa vitawajibika kwa kuwa na sera ya jinsia kwa muda wote, na kitasaidia kuongeza ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi” amemaliza   Naibu Msajili  huyo.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

No comments

Powered by Blogger.