''YAKIKUFIKA MAFIKO MOYO UPE AMINIKO LISILO MWISHO HALIPO'' KAULI YA MTUHUMIWA WA DAWA ZA KULEVYA.
NAMARYAM NASSOR
MAHAKAMA Kuu ,iliyopo Tunguu Zanzibar, imemuhukumu kijana Abrahman Ismail Soli mwenye umri wa Miaka 33 mkaazi wa Kilosa, Mkoa wa Morogoro Tanzania bara, kutumikia kifungo Cha miaka 15 Chuo cha Mafunzo Kwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya.
Akisoma hukumu hiyo, Jaji Mohamed Ali Mohamed amesema mshtakiwa huyo, ametiwa hatiani baada ya mahakama kujiridhisha, na ushahidi uliyotolewa na upande wa mashtaka , uliyoongoza na Mwendesha Mashtaka wa Serikali kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar, Ali Amour.
Jaji Mohamed, alisema kuwa mshtakiwa huyo, mkaazi wa Kilosa,alikamatwa Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Amaan Abeid Karume, akisafiri kuelekea Dubai , alipatikana na mafurushi 10 ya bangi akiwa ameyatia kwenye Begi la kusafiria.
Kesi hiyo, yenye namba 82 ya mwaka 2023 , jumla ya mashahidi nane walisikilizwa kwa upande wa Mashtaka na upande wa utetezi kulikuwa na shahidi mmoja ambae ni mshtakiwa.
Aidha, mshtakiwa huyo, siku ya utetezi wake alisema msemo ufuatao" Yakikufika mafiko moyo upe aminiko lisilo mwisho halipo, mwisho wa kujitetea.
Awali Ilidaiwa na Mwendesha Mashtaka Ali Amour, kuwa mnamo siku ya tarehe 10/05/2023 majira ya saa 1:30 usiku huko, uwanja wa Abeid Amaan Karume (Terminal 3) bila ya halali alipatikana akisafirisha mafurushi 10 ya madawa ya kulevya aina ya bangi, yenye uzito wa kilogram 2.55 kutoka Zanzibar kuelekea Dubai kupitia shirika la ndege la fly Dubai.
Mtuhumiwa huyo, alishtakiwa Kwa kosa la kusafirisha madawa ya kulevya , kinyume na kifungu Cha 21 (1) (a) Cha Sheria ya Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za kulevya Zanzibar, Sheria Namba 8 ya mwaka 2021 Sheria za Zanzibar.
Mwisho


Post a Comment