RUSHWA YA NGONO SUALA LINALOWARUDISHA NYUMA WANAWAKE KUWA VIONGOZI

Rushwa ya Ngono,suala linawarudisha nyuma wanawake kuwa Viongozi

Na –Maryam Nassor.





Zanzibar: ‘’Niliishiwa na nguvu wakati aliponiambia kama unaitaka hii nafasi basi lazima tukutane kimapenzi kwanza ndio uiptae”Amesema Sharifa.Huku kitu pekee kilichomjia kichwani kwake ni kuliweka jambo hilo liwe siri, libaki  milele kwenye shimo la nafsi yake, hakutaka mume wake ajuwe nini kilimkuta hata akaachana na siasa mwaka 2015 labda  ingeweza kumnusuru  na wimbi la aibu na fedheha.

Hii ni baada ya kutakiwa kimapenzi na kiongozi wake ndani ya chama, katika kikao cha kujadiliwa ili agombee nafasi ya mjumbe wa kamati kuu ya Chama hicho huko Wilaya ya Chake chake Mkoa wa Kusini Pemba.

Sharifa*39 mama wa watoto wanne,anayeishi na mume wake Kisiwani Pemba, aligombea nafasi ya ujumbe w Kamati Kuu ya Taifa ya Chama, Wilaya ya Chake Chake mwaka 2015,  katika kikao cha kujadiliwa aliitwa na kiongozi wake wake na kumpa sharti kama anaitaka nafasi hiyo kwanza wakutane kimapenzi.

“Maneno yake yalinivunja moyo na nikajiona kama nimevuliwa nguo,aibu niliona na nikajihisi kama sijui hata nisemeje mimi” Aliendelea kusema Sharifa mwaka 2015 ulikuwa mgumu kwake, baada ya ndoto yakee ya kuwa kiongozi kuishia hapo kutokana  na ukatili wa kisaikolojia uliopitia.”Sikuwa na ujasiri wa kumuhadithia mtu kadhia hiyo iliyomkuta mpaka nikaachia ngazi,na kujitoa katika kinyanj’anjiro hicho, na hilo lilipelekea kupata  matatizo ya kisaikolojia.” Aliishia hapo Sharifa.

Udhalilishaji wa kijinsia na suala linawatafuna wanawake waliopo kwenye vyama vya sasa hii Tatu*40 ambae alikatisha ndoto zake za kuwa kiongozi mwaka 2020 Wilaya ya Kaskazini ‘A’ Unguja.

Tatu mama wa watoto wawili mama wa nyumbani mkaazi wa Wilaya ya Kaskazini ‘A’ Unguja, ni miongoni mwa wanawake waliokatisha ndoto zao za kuwa viongozi, kwa sababu ya ukatili wa kisaikolojia uliompata wakati anagombea.

Sababu kubwa ya kukatisha ndoto zake, ni baada ya kukumbwa na ukatili  wa kisaikolojia , baada ya kutakiwa kimapenzi na msaidizi wake wa kampeni na kuliweka jambo hilo kuwa siri, kwa kuhofia ya aibu na fedheha kutoka kwa wanajamii.

‘’Sikuwa najua kama ningekutwa na mkasa ule, kwani yule mtu aliyenitaka kimapenzi ni mtu ambae, anaaminika na mume wangu, nilihofia hata kumuhadithia kadhia ile” Amesimulia huku akiinamisha sura kwa aibu.‘’Nilipata msongo wa mawazo, nilikuwa nakaa ndani nalia pekee yangu, nikihofia siri ile kuja kujulikana, sura yangu nitaiweka wapi’’ Amehoji Tatu.

Utafiti uliofanya na Wizara ya Maendeleo ya Jamii,Jinsia,wanawake na Makundi Maalum, imeonesha  idadi kubwa ya wanawake na wanaume  wanaofanyiwa ukatili wa kingono, kimwili na kisaikolojia.Matokeo ya utafiti huo, wa SIGI -2022 yanaonesha asilimia 55 ya wanawake wenye umri wa miaka 15-49, wameshawahi kufanyiwa aina moja wapo ya ukatili.Ambapo, asilimia 16 wameshawahi kufanyiwa ukatili wa kisaikolojia, asilimia 15 ukatili wa kimwili na asilimia 7 wameshawahi kufanyiwa ukatili wa kingono.

Tatu Ali Abass ni daktari na  mwanasaikolojia wa maswala ya afya ya akili, Hospitali ya Wilaya Vitongoji  Mkoa wa kusini Pemba,amesema madhara makubwa huwapata watu wanaopata ukatili wa kisaikolojia, ikiwemo msongo wa mawazo na endapo hawatatibiwa mapema, wanaweza wakapata ugongwa wa afya ya akili na ugongwa wa sonona.“Wathirika wa vitendo vya ukatili wa kisaikolojia, wamekuwa wagumu kutoa taarifa kuhusu vitendo hivyo, kutokana na kuhofia aibu na fedheha kutoka kwa wanajamii ila kusema ni moja wapo ya tiba”Amesema Daktari Tatu.

Ripoti ya sensa ya watu na makaazi ya Tanzania ya mwaka 2022 inaonesha kuwa Zanzibar ina wakaazi 1,889,773 kati ya hao, wanaume ni 915,492 na wanawake ni 974,281.Hii, ina maana kwamba wanawake ni asilimia 51.6 ya wakaazi wote wa Zanzibar, lakini wingi wao huo hauonekani katika nafasi za uongozi na vyombo vya maamuzi kutokana na vikwazo vingi lakini pia, ukatili wa kisakolojia.

Anna Athanas Paul, ni Naibu Waziri wa wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, amesema tathimini iliyofanya na wizara hiyo, katika taasisi mbalimbali imeonesha kuwa wanawake bado wapo kidogo katika nafasi za Uongozi, ukilinganisha na wanaume jambo ambalo linahitaji kuangaliwa.‘’Takwimu  zilizokusanywa na wizara kutoka taasisi mbalimbali  kwa mwezi machi mwaka 2024,zinaonesha ni asilimi 30 tu ya wanawake  ambao wako katika uongozi, ukilinganisha na wanaume ambao ni asilimia 70’’ Amesema Naibu Waziri Anna.

Anna, ameongeza kuwa Serikali inaendelea na jitihada katika kufikia malengo yaliyowekwa kupitia Dira ya 2050 na mpango wa Maendeleo (ZADEP) 2021/2026 ambapo lengo katika nafasi za uongozi ni kufikia 50/50.

Ziko Mamlaka ambazo zinahusika na maswala ya rushwa na uhujumu Uchumi- ZAECA, kupitia Afisa Elimu wake Yussuf Juma Suleiman amesema kuwa, ‘’ Sheria ya kuzuia Ruchwa na uhujumu Uchumi Zanzibar, sheria namba 5 ya mwaka 2023 kifungu cha 52, kitasaidia  kwa kiasi kikubwa kupunguza vitendo hivyo’’ Amesema Yussuf huku akiwataka wanawake wanaotaka kugombea nafasi za uongozi kwanza kusoma elimu ya uraia, ili kutambua haki zao bila ya kubabaishwa na mtu.

Chama cha wandishi wa habari Wanawake Tanzania Zanzibar,-TAMWA ZNZ  ni Taasisi isiyo ya kiserikali,inayojishuhulisha na maswala ya utetezi wa  haki za mtoto wakike, Mkurugenzi mtendaji wa TAMWA ZNZ, Dk Mzuri Issa amesema wanawake wanaogombea nafasi za uongozi wanakumbwa na vitendo vingi vya ukatili wa kijinsia na kisaikolojia.”Wanawake wenye nia ya kugombea wasivunyike moyo na wawe majasiri ili kuongeza  wingi wao katika nafasi za uongozi mwaka 2025 na kuripoti vitendo hivyo katika taasisi husika ili waweze kupata msaada” Amesema Dkt Mzuri

Mohamed Ali Ahmed, ni Naibu Msajili wa vyama vya Siasa Tanzania,kwa upande wa Zanzibar,amesema kuongezeka kwa kifungu cha 10 C ndani ya sheria ya vyama vya siasa nchini, kinatoa nafsi kwa wanawake kuongeza ushiriki wao,na kuwajibika kwa vyama kwa kuwa na sera ya jinsia muda wote, kwani hapo awali havikupaswa vyama kuwa na sera hiyo.”Wanawake wanatakiwa kuwa wajasiri na wenye uthubutu ili kuongeza wingi wao katika nafasi za uongozi, na kuviripoti vitendo vyote vya udhalilishaji na ukatili wa kijinsia vinavyowakumba, kwani kugombea nafasi za uongozi ni haki ya kila mmoja raia wa Tanzania’’ Amemaliza Mohamed.

          


No comments

Powered by Blogger.