KUKOSEKANA KWA DAWATI LA JINSIA KWENYE MICHEZO , WAATHIRIKA WAPAZA SAUTI ZAO



NA MARYAM NASSOR

KANUNI na sera ya michezo ya Zanzibar ya  mwaka 2018, imetamka wazi nia njemaa ya Serikali  katika kuhakikisha  uwepo wa usawa  wa jinsia katika michezo.

Hata hivyo, nia  njemaa hii haifanyi kazi katika usimamizi wa kila siku, kutokana na mapungufu ya vifaa vya michezo na ukosefu wa dawati la jinsia ndani ya vyama vya michezo.

Umuhimu wa dawati la jinsia ndani ya vyama vya michezo ni mkubwa, kutokana na kutamalaki kwa vitendo vya ukatili na udhalilishaji ndani ya michezo na kuonekana ni vya kawaida. 

 Waswahili wanasema  lisemwalo lipo, Fatma Ali Bakari( si jina lake halisi) mchezaji wa mpira wa miguu timu ya wanawake, akizungumza na mwandishi wa Makala hii amesema  udhalilishaji kwenye michezo upo na wachezaji wanauchukulia ni hali ya kawaida.

Amesema kuwa, ni vigumu kuutambua udhalilishaji unaotokea kwenye michezo kutokana na kuwa watendaji wa matendo hayo ni watu ambao wanaaminika katika michezo,kwani mara nyingi  anaweza kuwa kocha hakupangi katika kikosi mpaka akutake kimapenzi.

‘’Mimi ni muhanga wa udhalilishaji katika michezo , niliacha kucheza mpira na kuihama timu yangu ya mwanzo kutokana na kocha kunitaka kimapenzi , nikaamua kuacha kwenda kufanya mazoezi’’ alisema.

Saada Saidi mchezaji wa timu ya mpira wa miguu warrious, amesema   dawati la jinsia ni muhimu mno kuanzishwa  kwenye vyama vya michezo, kutokana na kuwa wachezaji wakikumbana na vitendo vya ukatili ndani ya michezo hawajui wapi pa kukimbia.

Alisema kuwa, sheria iliyokuwepo ya michezo ibara ya 58 ya katiba ya fifa, inawataka wachezaji kupeleka malalamiko yao kwenye kamati za maadili ndani ya vyama vya michezo na  kesi za michezo zisipelekwe kwenye mahakama za kawaida.

‘’ Icho kitu hakiingii akili vipi unaweza kumpelekea malalamiko mtu ambaye aliyekubaka, atajihukumu vipi na wewe kweli utapa haki yako katika hali kama hiyo hatuwezi kufika, kamati inaundwa na kocha nay eye ndio mbakaji masalani, haki haiwezi ikapatikana’’ alisema.

Nae, mchezaji wa timu ya mwembeladu fc timu ya wanaume, Abubakar Mohamed Sharif amesema  ni vyema kuanzishwa  kwa dawati la jinsia ndani ya michezo, kwani udhalilishaji ni mwingi na wachezaji hawajui nani wakumueleza matatizo yao yanao wasibu.

‘’ Sisi wachezaji hatuna sehemu maalum ya kupeleka malalamiko yetu  kuhusu ukatili na udhalilishaji unaotokea ndani ya michezo, hivyo wengine huacha ndoto zao  zikapotea,tu kwasababu ya kutakiwa na makocha kimapenzi na kesi hizo ni nyingi kwenye michezo ‘’ alisema.

Nae, kocha wa  ngumi za kulipwa Maryam Charles amesema kuwa kama Serikali inataka vijana wengi wajiajiri kwenye michezo ni  wajibu wao kuweka mazingira mazuri na kuiangalia kwa umakini  sekta hiyo,ili wazazi wawe na uhakiki wa usalama wa watoto wao.

Alisema kuwa, michezo ni afya , ni fursa  nia pesa lakini pia ndio sekta yenye uhakika wa ajira kwa vijana awe kasoma au hajasoma ilimradi tu awe anapenda michezo anaweza kufanikiwa.

Aidha alisema kuwa, ni wakati sasa wa kuiangalia sheria ya michezo na kuitafsiri nini maana halisi na kwanini kesi za udhalilishaji zinazotokea ndani ya michezo  zisipelekwe katika vyombo vya sheria.


“ Nahisi mimi maana halisi ya ile ibara ya 58 ya katiba ya fifa bado haijaeleweka wala  haijakaa sawa kwa mazingira ya sasa inahitaji mabadiliko’’ alisema.

Makame Ameir Mgeni, kocha wa michezo kwa maendeleo amesema  kuna kesi nyingi za udhalilishaji  ambazo  zimetokea  ndani ya michezo, na wafanyaji hawakuchukuliwa hatua zozote na kupelekea kuuwa vipaji na ndoto za watoto hao.

Alisema kuwa, kuna makocha wanabaka kwenye michezo na wengine kuwapa mimba wachezaji lakini wachezaji hawana sehemu maalum ya kupeleka malalamiko yao, mwisho wa siku kuacha na mpira .

‘’ Wachezaji wanakumbana na udhalilishaji mkubwa kwenye michezo na wanakosa sehemu ya kukimbila , hivyo kuanzishwa kwa dawati la jinsia litawapa ujasiri na kujiamini wachezaji wetu na watajiona wako sehemu salama kwenye michezo’’ alisema.

Katibu wa shirikisho la mpira wa miguu Zanzibar ( ZFF) Hassan Ahmada Vuai amekiri kuwa kuna haja ya kuanzishwa kwa dawati la jinsia ndani ya michezo kutokana na umuhimu wake.

Alisema kuwa, kama wanataka kufikiwa ule usawa wa kijinsia ndani ya michezo basi ipo haja ya kuanzishwa kwa dawati  hilo ili lishuhulikie vitendo vya ukatili na udhalilishaji unaotokea ndani ya michezo.

Chama cha wandishi wa habari wanawake Zanzibar,( TAMWA ZNZ) kupitia mradi  wa michezo kwa maendeleo unaofadhiliwa na shirika la Ujerumani (GIZ)  kupitia Afisa wake Hairat Haji amewataka wandishi wa  habari kuhamasisha na  kuandika habari za michezo na changamoto zinazowakumba wachezaji ndani ya michezo ikiwemo ukosefu wa dawati la jinsia ili  changamoto hizo zifanyiwe kazi.

Nao, chama cha wanasheria wanawake Zanzibar  (ZAFELA) kupitia Afisa wake Ruffea Juma, kimesema kuwa katika mradi wa michezo kwa maendeleo  unaodhaminiwa na shirika la Ujerumani  nchini Tanzania ,(GIZ) kimeandaa muongoz ambao utawasaidia wachezaji kujitambua na kujikinga na udhalilishaji ndani ya michezo .

                                 MWISHO

No comments

Powered by Blogger.