DHANA YA MICHEZO KWA MAENDELEO ILENGE PIA USHIRIKISHWAJI WA TIMU ZA WATU WENYE ULEMAVU

NA MARYAM
NASSOR
Dhana ya michezo kwa maendeleo , imekuja kuwapa hamasa vijana wanaotaka
kujiajiri kupitia sekta ya michezo bila ya kubagua jinsia zao .
Wakiwa na
imani kuwa, ajira ni ngumu kupatikana
lakini kupitia fursa zinazotokana na michezo wanaweza ‘ kutoboa’ kimaisha.
Kwa hapa
Zanzibar kuna vyama 42 vya michezo, vilivyosajiliwa na ofisi ya mrajisi wa
vyama vya michezo, vikiwemo vyama vya michezo ya watu wenye ulemavu.
Katika
makala haya mwandishi, anaangazia umuhimu wa kushiriki michezo kwa maendeleo,
kwa watu wenye ulemavu.
Michezo wanayoshiriki timu za watu wenye ulemavu hapa Zanzibar ,
zinakabiliwa na changamoto lukuki ingawa
wakienda kuiwakilisha nchi nje ya nchi, wanarudi na medali za dhahabu au fedha.
Kassim
Mohamed Ramadhan, mchezaji wa timu ya watu wenye ulemavu wenye mguu mmoja na
mkono mmoja, akizungumza na mwandishi wa makala haya, amesema michezo imemrudishia tabasamu lake tena.
Amesema,
miaka 13 iliyopita baada ya kupata ajali
mbaya iliyopelekea kukatika kwa mguu wake mmoja, akiwa na umri wa miaka 7
alikuwa mtoto mnyonge sana.
Alisema kuwa, alikuwa katika hali ya ulemavu na watu katika kijiji chao, walimtenga lakini hakukata tamaa alisoma kwa bidii na kujiunga katika timu ya watu wenye ulemavu.
Amesema, baada ya kukatwa mguu hakuwa na
matumaini yoyote katika maisha yake, lakini kwa sasa michezo ndio uponyaji wake
na sehemu inayompa matumaini mapya.
“ kwangu
mimi naamini kuwa, michezo ni ajira lakini bado kwa sisi watu wenye ulemavu
hatujafikia huko, lakini mimi naichukulia kama uponyaji wangu na sina mawazo
nikishiriki michezo”alisema.
Aidha
alisema kuwa, mwaka jana alishiriki michezo ya AFCON alikuwemo katika kikosi
cha timu ya taifa cha tembo warrious walipoenda nchini misri na kutokea mshindi
wa tatu kwa timu ya Tanzania.
“Kutoka
kutengwa na jamii hadi kusimama kwenye jukwaa na kupeperusha bendera ya nchi,
ama kweli hiyo ndiyo nguvu ya michezo “alisema.
Aidha, aliiomba Serikali kama mdau nambari moja kuzidi kufanya uwekezaji katika sekta ya michezo, ili ile dhana ya michezo kwa maendeleo izidi kuonekana kwa wote.
Nae, kocha
timu ya watu wenye ulemavu wa mguu mmoja
na mkono mmoja, Hassan Haji Silima, alisema bado timu za watu wenye ulemavu zinakabiliwa
na ukosefu wa kiwanja maalum cha kufanyia mazoezi.
“ Timu za
watu wenye ulemavu, hatuna kiwanja maalum cha kufanyia mazoezi, mwanzo tulikuwa
tukifanyia uwanja wa Amaan ndani, tukahama wakati kinafanyiwa matengenezo na
kwasasa bado hatujarudi tena kule” alisema.
Amesema
kuwa, hawana ufadhili wanaupata katika
timu zao, hilo linawapelekea kufanya mazoezi mara chache kutokana na kuwa
wachezaji wanakaa mbali na wenye magari
hawapendi kuwachukuwa watu wenye ulemavu.
Nae,mwenyekiti wa timu ya special olympik ya
Zanzibar( SOZ) Saada Hamad Ali amesema
kuna umuhimu mkubwa kwa watu wenye ulemavu kushiriki michezo kwa maendeleo.
Amesema
kuwa,timu za watu wenye ulemavu zikishiriki kwenye mashindano zinafanya vizuri
kuliko za wale waliyokuwa hawana ulemavu.
Lakini tatizo liliopo ni kutengwa na kudharauliwa kwa timu hizo, kwani washashiriki mashindano ya olympik mara saba nje ya nchi na mara zote wanashinda na wanarudi na medali.
Aidha
amesema kuwa, mwaka jana timu yao ilishiriki special olimpik na kutokea mshindi
wa kwanza, nchini ugiriki na Rais wa Zanzibar alikwenda kuwaona wakati wako
kule na kuahidi wakirudi waendee kumuona, lakini mpaka leo bado hawajafanikiwa
kumuona kutokana na ahadi yake hiyo.
“Mwaka jana
wakati tuko nchini Ugiriki, Rais Dk Mwinyi alikuwepo kule kwenye ziara zake za kiserikali
na alikuja kutuona na kututaka tukirudi nyumbani, twende tukamuone Ikulu na watoto
wetu lakini huu ni mwaka sasa ,kila tukienda kuulizia utaratibu tunazungushwa huku na kule’’alisema.
Alisema kuwa, michezo ni muhimu hasa kwa kuimarisha urafiki baina yao, na kutekeleza mkataba wa haki za watu wenye ulemavu.
Aidha
alisema kuwa, changamoto wanazokumbana nazo kabla ya kwenda mashindano hayo, ni
kuwa hawana fungu la bajeti ya timu zao,
kwani hawajawahi kupatiwa fungu kutoka tasisi za umma tokea kuasisiwa kwa
mashindano hayo mwaka 1988.
Nao, baadhi
ya wazazi wenye watoto walemavu,waliyozungumza
na mwandishi wa makala haya, walisema kuwa michezo kwa watu wenye ulemavu ni
muhimu mno.
Walisema
kuwa, watu wengi wenye ulemavu ni wenye msongo wa mawazo kwani huwa
hawashirikishwi katika mambo mengi ya kijamii, hivyo kukutana kwenye michezo ni
jambo linalowapa faraja.
Na kuitaka Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kuendelea kuzisaidia timu hizo na kuwasaidia kutafuta wadhamini ili kuwe na ligi za mikoa na wilaya kama timu nyengine.
Hija Mohamed Ramadhani, mshauri wa maswala ya jinsia katika michezo kutoka shirika la Ujerumani (G IZ)hivi karibuni alipokutana na wandishi wa habari, alisema mradi wa michezo kwa maendeleo hapa Zanzibar utaboresha mazingira mazuri ya mindombinu ya viwanja na inalengo la kujenga viwanja saba Unguja vinne na Pemba vitatu .
Lakini ipo haja kwa shirika hilo na taasisi nyengine kujitoa zaidi kudhamini ligi za timu za watu wenye ulemavu, ili kuwapa hamasa na kuiona hasa ile dhana ya michezo kwa maendeleo inavyofanya kazi kwani waswahili wanasema ‘ kuona ndio kuaminii’.

Post a Comment