ZACSO YAHAMASISHA UMMA KUHUSU MAADHIMISHO YA SIKU YA TAWAHUDI DUNIANI
Na Maryam Nassor
Taasisi ya Zanzibar Autism Care and Support Organisation (ZACSO) imeujulisha umma kuhusu maadhimisho ya Siku ya Tawahudi (Usonji) Duniani, yanayoadhimishwa kila mwaka tarehe 2 Aprili, kwa lengo la kuongeza uelewa wa jamii kuhusu hali hiyo na kuhimiza ushirikiano katika kuwasaidia watu wenye tawahudi.
Akizungumza na vyombo
vya habari katika ukumbi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania,
Zanzibar (TAMWA ZNZ) Tunguu, Mwenyekiti wa Taasisi hiyo, Munawarah Mahfoudh Haji, amesema kuwa tawahudi (usonji) ni
hali ya ukuaji wa ubongo inayoathiri uwezo wa mtu katika mawasiliano, mahusiano
ya kijamii pamoja na tabia.
Amesema kuwa, watoto na
watu wenye tawahudi wanahitaji aina tofauti za msaada kulingana na mahitaji yao
binafsi, lakini kwa uelewa sahihi, huduma stahiki na mazingira jumuishi, wana
uwezo wa kuishi maisha yenye tija na heshima kama watu wengine katika jamii.
Aidha, amesema maadhimisho ya mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu isemayo: “Autism and Humanity, Every Life Has Value” (Tawahudi na Ubinadamu, Kila Maisha yana Thamani), inayolenga kusisitiza umuhimu wa kutambua utu, heshima na thamani ya kila mtu mwenye tawahudi, pamoja na kuhakikisha anapata haki sawa katika nyanja zote za maisha.
Ameongeza kuwa,
kaulimbiu hiyo pia inahimiza jamii kuondokana na unyanyapaa na badala yake
kujenga mazingira jumuishi yanayowawezesha watoto na watu wenye tawahudi
kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii.
Amesema kuwa ,kuna ongezeko la utambuzi wa watoto
wenye dalili za tawahudi Zanzibar, jambo linaloonesha umuhimu wa kuendelea
kuelimisha jamii, kuimarisha huduma za afya na elimu jumuishi, pamoja na
kupunguza unyanyapaa unaowakumba watoto hao na familia zao.
Amesema ,Katika kuadhimisha siku hiyo muhimu, ZACSO imeandaa kongamano litakalofanyika Aprili 8, 2026, likiwakutanisha wadau kutoka sekta za afya, elimu, serikali, mashirika ya kiraia pamoja na jamii kwa ujumla.
Akieleza malengo ya
kongamano hilo, amesema ni pamoja na kuongeza uelewa wa jamii kuhusu tawahudi,
kuhamasisha mtazamo chanya na jumuishi, pamoja na kuwa jukwaa la kubadilishana
uzoefu na kujadili changamoto katika sekta za afya, elimu na jamii.
Aidha, ametoa wito kwa
jamii, wazazi, walezi, wataalamu na wadau wote kushiriki kikamilifu katika
maadhimisho hayo na kuunga mkono juhudi za kujenga jamii jumuishi inayotambua
na kuheshimu haki za watu wenye tawahudi visiwani Zanzibar.
Amesisitiza kuwa, kwa pamoja, jamii inaweza kujenga mazingira
yanayokubali tofauti na kutoa fursa sawa kwa kila mtu.
MWISHO
Post a Comment