SEKTA YA UTALII ZANZIBAR YACHANGIA ASILIMIA 30 YA PATO LA TAIFA

NA MARYAM NASSOR

WAZIRI wa Utalii na Mambo ya Kale, Mudrik Ramadhan Soraga, amesema sekta ya utalii ni mhimili muhimu wa uchumi wa Zanzibar, ikichangia zaidi ya asilimia 30 ya Pato la Taifa na kutoa ajira zaidi ya 65,000.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo kuhusu siku 100 za mafanikio ya uongozi wa awamu ya pili ya Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali inaendelea kuweka mikakati thabiti ya kukuza sekta hiyo kwa kuzingatia utalii endelevu, ubora wa huduma na ushirikishwaji wa wananchi.

Amesema katika kipindi hicho cha siku 100, Wizara imefanikiwa kutekeleza hatua mbalimbali, ikiwemo kuimarisha utalii wa mikutano, matamasha, michezo na matibabu.

“Tumeshiriki na kuratibu matukio ya kimataifa kama vile FITUR nchini Hispania, World Travel Market (WTM) London, Sauti za Busara, pamoja na tamasha na makongamano ya kitaifa na kimataifa. Hatua hizi zimeendelea kuitangaza Zanzibar kimataifa na kuongeza ushindani wake,” amesema.

Aidha, amesema katika juhudi za kuongeza idadi ya watalii, Zanzibar imepokea watalii 273,773 kutoka mataifa mbalimbali, ikiwa ni ongezeko la asilimia 115 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2020/2021. 

Ameongeza kuwa muda wa ukaazi wa wageni umeongezeka kutoka siku 6 hadi siku 8, jambo linalochangia kuongezeka kwa mapato na manufaa kwa wananchi.

Kwa upande wa uwekezaji, amesema kumekuwa na ongezeko la vyumba vya hadhi ya juu hadi kufikia zaidi ya 17,000, hatua inayolenga kuvutia watalii wenye matumizi makubwa.

Sambamba na hilo, Wizara inaendelea kuelimisha wadau wa sekta, kurasimisha huduma za “beach boys na beach girls”, pamoja na kuimarisha usimamizi wa bahari kwa kushirikiana na Wizara ya Uchumi wa Buluu kupitia mpango wa ‘Marine Spatial Planning’.

Katika kuendeleza utalii wa kijamii na vijijini (Community-Based Tourism), pamoja na kuimarisha utalii endelevu, Wizara imeendelea kutekeleza kampeni ya “Greener Zanzibar”, kuweka mfumo wa usimamizi wa taka katika maeneo ya utalii, na kuandaa miongozo ya viwango vya kimataifa vya utalii endelevu.

Zanzibar pia ni mwanachama wa Global Sustainable Tourism Council (GSTC) kwa miaka miwili mfululizo na inaendelea kujenga uwezo wa taasisi na wadau, ambapo taasisi hiyo hutoa miongozo ya viwango vya utalii endelevu duniani.

Kutokana na mafanikio hayo, Zanzibar imepata tuzo ya kimataifa ya World Travel Awards kama kituo bora cha “Corporate Retreat” kwa mara ya kwanza, jambo linalothibitisha ubora wa huduma na mazingira ya uwekezaji.

Aidha, Zanzibar imefanikiwa kushinda kuwa mwenyeji wa mkutano wa kimataifa wa Inter Island State Tourism Policy Forum (ITOP) utakaofanyika mwaka 2027, utakaowaleta pamoja viongozi na wadau wa utalii kutoka mataifa mbali mbali.



Top of Form

Bottom of Form

 

No comments

Powered by Blogger.