IIT MADRAS ZANZIBAR INATEGEMEA KUTEKELEZA PROGRAM YA KITAALUM PAMOJA NA ZUT.

 

TAASISI ya Teknolojia ya India Madras Kampasi ya Zanzibar (IITMZ) inategemea kuanza utekelezaji wa programu za kitaaluma za pamoja katika masuala ya teknolojia kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Teknolojia cha Zambia (ZUT).

Hayo yamebainika kufuatia mazungumzo yaliyofanyika baina ya uongozi wa IITMZ na uongozi wa ZUT ikiwa ni miongoni mwa hatua za ufatiliaji wa Hati ya Makubaliano ya Maelewano  (MoU) yalifikiwa na taasisi hizo mbili mapema mwaka 2025. 

Mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ofisi za IITMZ yameongozwa na Mkurugenzi Dhamana IITMZ Prof. Brabhu Rajagopal pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa ZUT Dk. Betty Shitima Bweupe.

Akizungumza juu ya ugeni huo Mkurugenzi Dhamana wa IITMZ Prof. Prabhu Rajagopal amesema kuwa, ni furaha kubwa kwa uongozi wa ZUT kufika katika kampasi za IITMZ, ikizingatiwa kuwa ZUT ni miongoni mwa vyuo vinavyoongoza katika elimu ya teknolojia nchini Zambia. Na kuthibitisha kuwa, ameona maono makubwa kuelekea kuendeleza ushirikiano baina ya taasisi hizo mbili kusudi kuleta elimu ya teknolojia iliyo bora ndani na nje ya nchi.

 Ameongezea kwa kusema kwamba, kazi ya IITM Zanzibar ya kupanua mipaka ya sayansi ya data na kuendeleza taaluma za kisasa za uhandisi imepokelewa kwa hamasa kubwa na wajumbe wa ZUT.

“Tumekubaliana kushirikiana katika maeneo mbalimbali, ikiwemo kubadilishana wahadhiri na wanafunzi, hususan katika ngazi za Shahada za Uzamili na Uzamivu (Masters na PhD), pamoja na kuimarisha ushirikiano wa utafiti kati ya nchi za Kusini mwa Dunia (South-South Collaboration).

Ameongezea kwa kuthibitisha kuwa, uwezo wa IIT Madras katika nyanja za vihisishi (sensors), akili unde (AI) na roboti una umuhimu mkubwa kwa Ukanda wa madini wa Copperbelt nchini Zambia ambako ZUT ipo.

Aidha, uwepo wa wanafunzi wengi wa Zambia katika kampasi ya IITMZ umeifanya ziara hio kuwa ya kipekee na ya kukumbukwa sana.

Akitoa maoni yake juu ya ujio wa ugeni huo, Mkuu wa Taaluma wa IITMZ, Prof. A.K. Suresh, amesema wamejadili maeneo mbalimbali ya ushirikiano wa kitaaluma kati ya IITMZ na Chuo Kikuu cha Teknolojia cha Zambia (ZUT), yenye lengo la kuimarisha maendeleo ya elimu ya juu na utafiti nchini.

Prof. Suresh amesema kuwa licha ya ZUT kuwa taasisi iliyopo kwa miaka mingi, kama chuo kikuu bado ni taasisi inayokua na yenye dira inayofanana na IITMZ katika kupanua ubora wa elimu na tafiti.

Ameeleza kuwa fursa zilizobainishwa ni pamoja na kubadilishana wanafunzi, kubadilishana wahadhiri kwa ajili ya ufundishaji na utafiti, pamoja na utekelezaji wa miradi ya pamoja ya utafiti.

Aidha, amesema kuwa kutokana na ZUT kuwa na utaratibu wa kuajiri wahitimu wa Shahada ya Uzamili katika kitivo chake, pia wamejadili uwezekano wa wahitimu wa Shahada ya Uzamili kutoka IITMZ kupewa nafasi za ualimu chuoni hapo, hatua itakayochangia kukuza rasilimali watu wenye ujuzi wa hali ya juu Zanzibar.

Nae Mkurugenzi Mtendaji wa ZUT Dk. Betty Shitima Bweupe amesema hatua ya kuitembelea kampasi ya IITMZ  ni kwa lengo la kupitia makubaliano ya kiutendaji yaliyokubaliwa awali, kadhalika kushudia utendaji halisi wa IITMZ kwa mujibu wa programu za kitaaluma zinazotegemwa kunufaisha pande zote mbili na Taifa kwa ujumla.

Pia, amethibisha kuridhishwa na hatua za kimaendeleo zilizofikiwa na IITMZ ndani kipindi kifupi tokea kuanzishwa kwake mwezi Oktaba, 2023.

‘Uwepo wangu katika kampasi ya IITMZ umeniachia matumaini makubwa, nimefurahia ubora wa taaluma inayotolewa na Taasisi hii. Amesema Dk. Betty.

Akiedendela kuizungumzia IITMZ Dk. Betty ameongezea kwa kusema kuwa, ZUT itatilia mkazo utekelezaji wa programu mfanano ambazo zinatekelezwa na taasisi hizo.

Vile vile, amesema kuwa, ZUT kuwa na chuo  pekee nchini Zambia kinachotoa taaluma ya masuala ya teknolojia kina nafasi kubwa zaidi ya kufanya kazi karibu na IITMZ kubadilishana utaalamu.

Adha, Dk. Betty amethibitisha  kufurahishwa na msimamo wa wanafunzi wa IITMZ ambao ni raia wa Zambia wanaondelea na masomo yao katika kampasi hiyo kwa kuonesha utayari wao wa kutumia ujuzi wao kushirikiana na taasisi mbalimbali kutatua  changamoto za kijamii, kitaaluma na kiteknolojia nchini Zambia mara tu watakapomaliza masomo yao.

Ujumbe wa ZUT katika kampasi za IITMZ  ulilenga pia kupitia na kufahamu kwa kina programu zinazoendesha na IITMZ, kuwatambua wataalamu kitaaluma pamoja na kushuhudia mazingira halisi ya kimafunzo yanayoendesha katika kampasi hiyo.

Kutoka ZUT wengine walioshiriki katika ziara hiyo ya siku mbili ni Dk. Gabriel Musonda ambae ni Mkurugenzi Taaluma na Dk. Geofrey Mumba, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara na Masoko.

No comments

Powered by Blogger.