SERIKALI IMEONGEZA TIJA YA UZALISHAJI WA KILIMO CHA MPUNGA ZANZIBAR



NA MARYAM NASSOR

WAZIRI wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo, Mhe. Suleiman Masoud Makame amesema Serikali imeongeza tija ya uzalishaji wa kilimo cha mpunga kwa kutoa ruzuku inayowezesha upatikanaji wa zana za kisasa za kilimo, zinazotumika , katika kutoa mafunzo kwa vijana wanaohudumia mabonde ya mpunga.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo kuhusu siku 100 za mafanikio ya uongozi wa awamu ya pili ya Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa mageuzi ya sekta ya kilimo unaolenga kuwaunganisha vijana katika kuimarisha thamani ya kilimo.

Amesema, lengo la Serikali ni kuwaunganisha vijana hao na taasisi za kifedha ikiwemo Benki ya Kilimo Tanzania (TADB) ili kuwawezesha kupata mikopo nafuu kwa ajili ya ununuzi wa zana na teknolojia za kisasa za kilimo.

 “Nia ya Serikali ni kuhakikisha wakulima wanapata zana bora za kisasa zitakazoongeza uzalishaji wa mpunga na mazao mengine ya kilimo,” alisema Mhe. Makame.

Aidha, amefahamisha kuwa Serikali imeendelea kuimarisha sekta ya mifugo kwa kuanzisha miradi ya ufugaji wa kuku ikiwemo kiwanda cha vifaranga kilichopo katika eneo la Kwambani chenye uwezo wa kuzalisha vifaranga 30,000 kwa wiki.


“ Tunawapa vijana mafunzo ya vitendo ili waweze kuwa wataalamu katika kuhudumia mabonde ya mpunga na kuongeza tija katika uzalishaji,” aliongeza Waziri.

Ameongeza kuwa, mwekezaji mwingine katika eneo la Pangeni yupo katika hatua za mwisho za kukamilisha ujenzi wa kiwanda cha vifaranga pamoja na kiwanda cha uzalishaji wa chakula cha kuku, miradi ambayo inatarajiwa kuimarisha sekta ya ufugaji wa kuku na kupunguza utegemezi wa uagizaji wa bidhaa hizo kutoka nje ya nchi.

“Haya yote yasingewezekana bila ya uwepo wa mashirikiano mazuri baina ya wakulima, wafugaji na wataalamu wa wizara wenye jitihada za dhati na malengo ya pamoja ya kuleta mageuzi ya kilimo kutoka kilimo cha kujikimu na kuwa kilimo-biashara,” ameeleza Mhe. Makame.

Aidha, amewasisitiza vijana kujikita katika shughuli za kilimo na ufugaji ili kujiimarisha kiuchumi, akieleza kuwa sekta hiyo imeendelea kuwa mkombozi mkubwa katika kuleta maendeleo ya wananchi, kukuza uchumi wa nchi na kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja.

 

 

 

 


No comments

Powered by Blogger.