WAANDISHI WA HABARI NA ASASI ZA KIRAIA WAMETAKIWA KURIPOTI MATATIZO YANAYOIKUMBA JAMII NA KUYATAFUTIA UFUMBUZI
NA MARYAM NASSOR
WAANDISHI
wa habari pamoja na viongozi wa Asasi za Kiraia wametakiwa kuyaripoti matukio
yanayoikumba jamii na kushiriki kikamilifu katika kuyatafutia ufumbuzi.
Akizungumza
na waandishi wa habari na viongozi wa Asasi za Kiraia katika ukumbi wa mikutano
wa Skuli ya Tumekuja, Kijangwani Zanzibar, Mratibu wa Mtandao wa Haki za
Binadamu Zanzibar (THRDC), Suleiman Muyuni Baitani, amesema waandishi wa habari
na viongozi wa Asasi za Kiraia wana nafasi kubwa ya kuibua matatizo
yanayoikumba jamii na kusaidia kuyatafutia ufumbuzi.
Amesema
ni vyema waandishi wa habari wakajifunza mbinu bora zaidi za kuandika habari za
kijamii ili kuweza kusaidia kutatua changamoto za wananchi kwa kuziripoti
kupitia vyombo vya habari.
“Ni
jukumu letu kuibua changamoto za jamii na vijana na kushirikiana katika
kutafuta ufumbuzi wa matatizo yao,” amesema Baitani.
Naye
Afisa Programu kutoka Pamoja Youth Initiative (PYI), Daudi Kassim, amesema
lengo la mafunzo hayo ni kuwaongezea uwezo waandishi wa habari na viongozi wa
Asasi za Kiraia katika kuripoti matukio yanayoikumba jamii.
Amesema
kuwa matukio yanayoikumba jamii si mageni, bali changamoto iliyopo ni uelewa
mdogo wa namna ya kuyatambua na kuyafanyia kazi, hivyo lengo kuu la mafunzo
hayo ni kuwajengea uwezo washiriki kuyatambua na kuyaripoti ipasavyo.
Aidha,
amesema katika kuripoti matukio ya kijamii ni muhimu kwa waandishi wa habari
kuwa na vielelezo na uthibitisho wa taarifa wanazoziripoti pamoja na kuielewa
vyema sheria za nchi.
Kwa
upande wake, Mkuu wa Utawala katika taasisi ya Pamoja Youth Initiative (PYI),
Mussa Mbwara, amewataka waandishi wa habari kusaidia katika kutatua changamoto
zinazoikumba jamii, hususan vijana.
Amesema
taasisi hiyo inafanya kazi kwa karibu na vijana, hivyo inaelewa changamoto
wanazokumbana nazo ikiwemo ukosefu wa fursa za mikopo na mitaji ya kuanzisha
biashara.
Hivyo, amewaomba washiriki kuyafanyia kazi mafunzo hayo ili taasisi hiyo ifikie malengo yake na jamii kwa ujumla ipate uelewa kuhusu haki na wajibu wao.
Nao
baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo akiwemo Ahmed Abdullah, mwandishi wa habari
wa blogu ya Zanlight, wamesema mafunzo hayo yamewasaidia kuelewa namna bora ya
kuripoti habari za kijamii na kushiriki katika kutatua matatizo yanayowakumba
wananchi.
Naye
Abdul Yakuti kutoka Jumuiya ya Wanawake Wenye Ulemavu Zanzibar (JUWAUZA)
amesema mafunzo hayo yamemsaidia kuyaona kwa undani matatizo yanayowakabili
watu wenye ulemavu na kutafuta njia za kuyatafutia ufumbuzi.
Mafunzo
hayo ya siku mbili yameandaliwa na Pamoja Youth Initiative (PYI) kwa waandishi
wa habari na Asasi za Kiraia kwa lengo la kuwapatia uelewa na uwezo wa kuripoti
matatizo yanayowakumba jamii.


Post a Comment