MASHIRIKA YATAKA UZINGATIAJI MASLAHI YA UMMA, MABORESHO YA SHERIA ZA HABARI ZNZ

 

                                        

 

Mashirika yanayoshughulika na habari, haki za binadamu na waandishi wabobevu Zanzibar inatoa ripoti ya ufuatiliaji kuhusu masuala ya vyombo vya habari na kufanya uchambuzi wa kina kuhusu kada ya habari na utendaji wa waandishi wa habari katika kipindi cha mwaka 2025 hususan katika kuangalia wajibu wa waandishi wa habari, maadili, uhuru wa habari pamoja  na mafanikio na changamoto.                                                                       

Kwa mujibu wa ripoti ya Mashirika hayo, mafanikio kadhaa yamepatikana katika sekta ya habari, hususan kuimarika kwa uwezo wa waandishi wa habari kupitia mafunzo mbalimbali katika kipindi cha uchaguzi, pamoja na uchambuzi wa habari zilizoripotiwa. Hata hivyo, uchambuzi huo umeonesha kuwepo kwa ukiukwaji wa maadili ya uandishi wa habari, ikiwemo upendeleo wa vyanzo vya habari kwa kujikita zaidi katika kauli za viongozi wa kisiasa na kushindwa kutoa nafasi sawa kwa makundi mengine ya kijamii. Aidha, baadhi ya taarifa zilikosa uwiano na haki kwa kutowasilisha pande zote za hoja, pamoja na kushindwa kuzingatia maslahi ya umma kwa kupuuza changamoto na sauti za makundi yaliyo pembezoni, jambo linalokiuka misingi ya uandishi wa habari wa kimaadili na haki za kijamii

 “Habari za viongozi zimekuwa zikitolewa zaidi huku makundi ya pembezoni ikiwemo habari za wanawake, vijana, wazee na habari za vijijini kutopewa nafasi inayostahiki” ripoti inaeleza.

Ingawa kumekuwa na vyombo mbali mbali vya habari hususan vyombo vya mitandaoni (online media) ikiwa ni hatua muhimu ya kukuza na kuimarisha vyombo vya habari lakini habari zilijikita zaidi katika matukio (current affairs) na hivyo kutokuwepo kwa habari za uchunguzi na uchambuzi.

Ripoti hiyo, inayohusisha mwaka 2025, inaeleza kuwa mazingira ya kazi kwa waandishi wa habari haikuwa nzuri ikijumuisha vitisho, unyanyasaji, utekelezaji wa sheria kwa upendeleo, kunyimwa taarifa, na ufuatiliaji mkali wa vyumba vya habari na majukwaa ya mtandaoni. Kwa mujibu wa Mashirika hayo, hali hii ilidhoofisha uwazi katika kuripoti habari za uchaguzi, imani ya umma, na ushiriki wa wananchi katika mchakato wa kidemokrasia.

Katika ufuatiliaji wake wa kabla, wakati na baada ya uchaguzi, Mashirika yalibaini pia baadhi ya mifano mizuri, ikiwemo vipindi vya redio vinavyohamasisha ushiriki wa wananchi na vipindi maalum vilivyolenga wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, mfano kipindi cha “Pambazuko” kutoka ZBC redio kinachorushwa kuanzia saa 12:00 asubuhi hadi 4:00   asubuhi. Hata hivyo, mafanikio hayo yalifunikwa na ukiukwaji wa maadili ya habari pamoja na kukosekana kwa umahiri na uhuru wa habari.

Ripoti inaeleza kuwa waandishi wa habari walikumbana na manyanyaso ikiwemo kunyang’anywa vifaa vya kazi, kuitwa na mamlaka za serikali, kutishiwa kufungiwa au kusimamishwa, pamoja na kulazimishwa kufuta maudhui waliyoripoti, hasa waliposhughulikia masuala ya uchaguzi, utawala bora na uwajibikaji. Vyombo vya habari vya mtandaoni vililengwa zaidi kupitia barua za onyo, vitisho vya kunyang’anywa leseni na maagizo ya kuondoa maudhui.

“Kwa mfano mwandishi wa habari wa Mawio TV kulazimishwa kuondoa taarifa mtandaoni iliyobeba malalamiko ya wanawake kuhusu haki, uwazi na uwajibikaji katika uteuzi wa viti maalum kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM). Vilevile kwa upande wa Unguja, Chum Online Media ilikumbwa na vitisho baada ya kuchapisha maoni ya wananchi wakidai haki kabla ya amani katika kuelekea uchaguzi, huku Zanzibar Yetu Online TV ikijumuishwa kwenye orodha ya vyombo vya habari vya mtandaoni ambavyo havijasajili leseni wala kulipa ada na kuwekwa katika hatari ya kufungiwa ambapo awali chombo hicho kilishafanya malipo hayo”, Ripoti hiyo inafafanua zaidi.

Ripoti pia inaonesha changamoto za kimuundo zinazotokana na mfumo wa sheria na sera za habari Zanzibar. Sheria nyingi za habari ni za zamani ikiwemo Sheria ya Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu ya mwaka 1988 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 1997 pamoja na Sheria ya Tume ya Utangazaji Zanzibar ya mwaka 1997 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2010 zinatoa mamlaka makubwa kwa viongozi wa serikali pamoja na kuingilia shughuli za vyombo vya habari. Ingawa Katiba ya Zanzibar inalinda uhuru wa kujieleza lakini utekelezaji wake hauendani kikamilifu na viwango vya kimataifa na kikanda vya haki za binadamu, hali inayoruhusu matumizi mabaya ya mamlaka.

Katika kipindi cha uchaguzi, baadhi ya waandishi wa habari na asasi za kiraia walizuiwa kuvifikia vituo vya kupigia kura, kuhesabu kura, na kupata taarifa za matokeo. Vyombo vya habari vya serikali vilipata upendeleo mkubwa, huku vyombo binafsi na huru vikinyimwa fursa sawa, jambo lililopunguza wingi wa sauti na haki ya wananchi kupata taarifa sahihi na tofauti.

“Vitendo hivi viliunda mazingira ya hofu na kujizuia kwa waandishi wa habari, na kudhoofisha jukumu la vyombo vya habari kama walinzi wa maslahi ya umma katika kipindi muhimu cha kidemokrasia,” inaeleza ripoti hiyo. “Bila vyombo vya habari huru na vinavyojitegemea, hakuna demokrasia ya kweli.”

Mashirika hayo yanatoa wito kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kufanya marekebisho ya haraka ya sheria za habari kandamizi na zilizopitwa na wakati, kufuata kwa vitendo Katiba ya nchi pamoja na mikataba ya kimataifa na kikanda ya haki za binadamu, na kuhakikisha uwajibikaji kwa wote wanaokiuka uhuru wa vyombo vya habari. Aidha, Mashirika yanaiomba Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kuangalia kwa kina taratibu zinazofuata sheria ili kuhakikisha mchakato wa uchaguzi unakuwa wazi, huru, na unaojumuisha vyombo vya habari na asasi za kiraia bila vitisho wala vikwazo.

Mashirika pia yanasisitiza upya dhamira yake ya kuendelea kutetea haki za waandishi wa habari, kukuza uandishi wa kitaaluma na wenye maadili, na kuimarisha uhuru wa vyombo vya habari Zanzibar. Sambamba na hilo Mashirika yanakumbusha kuwa uhuru wa habari ni nguzo muhimu ya maendeleo endelevu chini ya misingi ya demokrasia, utawala bora, na imani ya wananchi.

 

IMETOLEWA NA:

Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC),

Chama Cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA-ZNZ)

Waandishi wa Habari za Maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA)

Baraza la Habari Tanzania, Zanzibar (MCT, ZNZ)

Jukwaa la Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania, Zanzibar (THRDC, ZNZ)

 

 

No comments

Powered by Blogger.