WAWAKILISHI WANNE HAWATOSHI KATIKA MAJIMBO 50 YA UCHAGUZI ZNZ
Na Maryam Nassor
Katika majukwaa ya siasa za Zanzibar, mjadala kuhusu
usawa wa kijinsia katika uongozi umeendelea kushika kasi, hasa baada ya
kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa Tanzania wa mwaka 2025.
Katika uchaguzi
huo ,jumla ya wagombea wawakilishi 484 waliogombea katika nafasi ya uwakilishi
katika majimbo 50 ya uchaguzi Zanzibar kwa vyama vyote 11 vilivyoshiriki katika
uchaguzi mkuu wa mwaka huu, 2025.
Lakini cha
kusikitisha ni wanawake wanne tu, ndio waliyoshinda nafasi hiyo ya
uwakilishi katika majimbo , na wanaume walipata majimbo 46.
Wanawake wanne
pekee, katika majimbo 50 ya uchaguzi ni ishara tosha kwamba ushiriki wa
wanawake katika uongozi bado ni mdogo na unahitaji nguvu mpya za kisera na
kijamii ili kufikia uwiano wa kweli wa kijinsia.
Hali hiyo ,imeibua
mjadala mpana kuhusu mustakabali wa ushiriki wa wanawake katika siasa na
utekelezaji wa Dira ya Endelevu ya Maendeleo Zanzibar (ZADEP 2021–2026),
inayolenga kufikia asilimia 50/50 katika nafasi za uongozi na ngazi za maamuzi.
Mboja Ramadhan Mshenga, kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM),
mkoa wa Kaskazini Unguja aliyeibuka
mshindi katika uchaguzi huo, anasema wanawake wana uwezo wa kuongoza,wanachohitaji
ni fursa na mabadiliko ya mitazamo katika jamii kuhusu wanawake na uongozi.
Anasema kuwa, tatizo si uwezo wa wanawake bali ni mazingira
yanayokwamisha ushiriki wao kwani wengi wanakosa rasilimali fedha za kampeni na uchaguzi . “Wanawake huwa tunajitokeza kwa wingi
kugombea nafasi za uongozi kwa sababu tunao uwezo, lakini wengi hawapewi nafasi
za kugombea na matokeo yake hatufikii usawa wa kijinsia,” anasema Mboja,
mwakilishi wa jimbo la Mahonda.
Mboja anaeleza kuwa, mfumo wa kisiasa uliopo bado
haujatoa nafasi ya kutosha kwa wanawake kushiriki kikamilifu katika michakato
ya uongozi, kutokana na kujengeka kwa dhana kwamba uongozi ni wa wanaume. Hali
hii, anasema hupunguza uungwaji mkono hata kutoka kwa wanawake wenyewe.
Pamoja na hatua zilizopigwa katika usawa wa kijinsia,
uchaguzi wa mwaka 2025 umeonesha kuporomoka kwa uwakilishi wa wanawake kisiasa,
ambapo idadi ya wanawake waliochaguliwa imepungua kutoka wanane katika kipindi
cha 2020/2025 hadi wanne katika kipindi cha 2025/2030.
Aidha anasema
kuwa, mfumo wa special seats hauwezi
kutatua changamoto hiyo kwani hauwapi wanawake nafasi ya ushindani wa moja kwa
moja majimboni.
Anashauri, kuwepo kwa sheria mahsusi zitakazolazimisha
uwiano sawa wa kijinsia katika nafasi za kugombea, ili kutoa nafasi zaidi kwa
wanawake kushiriki katika majimbo.
Kwa upande wake, Kiongozi wa Wanawake katika chama cha
Alliance for Democrats Change (ADC), Nadhira Ali Haji, anasema kuwa asilimia
50/50 katika nafasi za uongozi ni haki ya kijamii na si upendeleo.
Anaeleza kuwa,
wanawake Zanzibar bado wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na
ukosefu wa rasilimali, elimu ya kisiasa na uungwaji mkono wa kijamii.
Nadhira anasema wanawake wanapojitokeza kugombea
hukabiliwa na vitisho, kubezwa, pamoja na kukatishwa tamaa na familia na jamii.
Hali hiyo husababisha wengi kushindwa kufika mbali katika safari ya kugombea
nafasi za uongozi.
Anapendekeza
kuwepo kwa mfumo wa kitaifa unaolazimisha vyama vya siasa kuweka asilimia
maalum ya wagombea wanawake katika majimbo.
“Usawa wa kijinsia si ombi, ni haki ya wanawake ambayo
imechelewa kutimizwa,” anasisitiza Nadhra.
Mashavu Bakar kutoka chama cha ACT-Wazalendo anasema kuwa
Serikali bado haijaonesha utayari wa dhati wa kuwapa wanawake nafasi za uongozi
ili kufikia 50/50.
Anasema kuwa, wanawake wengi kutoka vyama vya upinzani
wanajitokeza kugombea, lakini hawapewi nafasi stahiki.
“Kufikia asilimia 50/50 katika vyombo vya maamuzi na
nafasi za uongozi ni nadra katika Serikali zetu zisizokuwa na usawa katika
uchaguzi,” anasema Mashavu.
Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar
(TAMWA ZNZ) ni mdau muhimu katika
kuhamasisha wanawake kugombea nafasi za uongozi. Afisa Program wa mradi wa
Young Media Fellows (YMF), Tatu Ali, anasema changamoto kubwa inayoathiri
ushiriki wa wanawake ni mitazamo ya kitamaduni kwamba siasa ni kazi ya wanaume.
“Tumekuwa tukiwapa mafunzo wanawake viongozi kutoka vyama vyote vya siasa nchini, ili
kuongeza ushiriki wao katika nafasi za uongozi na vyombo vya maamuzi “ anasema.
Mchambuzi wa masuala ya wanawake na uongozi, Almasi Mohd,
anaeleza kuwa, Dira ya Maendeleo ya Zanzibar imeweka wazi umuhimu wa usawa wa kijinsia kama
msingi wa maendeleo jumuishi. Hata hivyo, utekelezaji wake unahitaji nguvu
zaidi, hasa katika kupunguza pengo la uongozi wa kijinsia.
Anapendekeza ,programu maalum za kuwaandaa wanawake
kuingia katika siasa na kuondoa dhana ya kwamba uongozi ni wa wanaume.
“Zanzibar haiwezi kufikia dira ya maendeleo bila kuwapa
wanawake nafasi sawa mezani kwa maamuzi, kwani wanawake ni wengi zaidi ya milioni 1.8 kwa mujibu wa Sensa ya
Watu na Makazi ya mwaka 2022 hivyo, ni lazima wapewa nafasi sawa katika nafasi
za uongozi na vyombo vya maamuzi,” anasema.
Mwisho
Post a Comment