ZAMECO YASIKITISHWA NA TUME YA UTANGAZAJI ZNZ, KUTISHIA KUVIFUNGIA BAADHI YA VYOMBO VYA HABARI VYA MTANDAONI.
Kamati
ya Wataalamu wa Masuala ya Habari Zanzibar (ZAMECO) inasikitishwa na hatua ya Tume ya Utangazaji
ya Zanzibar kutoa taarifa inayoweka orodha ya Vyombo vya Habari vya
Mtadaoni inavyovitaja kuwa vinafanya kazi kinyume cha sheria ambayo Tume hiyo
inaisimamia na kutishia kuvichukulia hatua kali za kisheria iliyoitoa tarehe 20
Mwezi Oktoba 2025 na nyakati nyengine tofauti.
ZAMECO
ambayo ni Kamati inayojumuisha watendaji wabobezi wa sekta ya Habari na utetezi
wa haki za binadamu kutoka asasi mbambali za kiraia zilizopo Zanzibar,taarifa hiyo imesema inalichukulia tamko hilo kuwa ni hatua inayoweza kudhoofisha jitihada za sekta
binafsi kukuza uhuru wa kujieleza na kuimarisha upatikanaji wa taarifa huru nchini.
Zanzibar ikiwa ni sehemu ya dunia inajitahidi kwenda na wakati,
kutoa mawazo mbadala na mifumo ya kisasa ya mawasiliano ya kiteknolojia (Social
Media), hatua hii ya
Tume inaonesha kurudisha nyuma jitihada hizi.
Vyombo
vilivyotajwa katika taarifa hiyo ni pamoja na TIFU ONLINE TV, MARHABA ONLINE TV, VUGA ONLINE TV, BUSATI ONLINE TV,
KASUSI ONLINE TV, DIGITAL ONLINE TV, DIGITAL ONLINE TV, LEADERS ONLINE TV,
ZANZIBAR YETU ONLINE TV, MAWENGI ONLINE
TV, JIMBI ONLINE
TV NA MU ONLINE TV.
Imesema ,Kuwepo kwa mitandao hiyo ya habari
kunawafanya pia vijana
waweze kujiajiri na kupata
kipato chochote kwa maisha yao na wengine
kufanyia kazi mafunzo
yao waliyosomeshwa vyuoni
wakati wakisubiria ajira za kudumu.
Ikumbukwe kuwa haki ya kupata taarifa
ni ya kikatiba kama inavyoelezwa kwenye Katiba ya
Zanzibar ya Mwaka 1984 (Toleo la 2010 katika Ibara ya 18 – pamoja na Mikataba ya Kimataifa ikiwemo Azimio la Ulimwengu la Haki za Binaadam (UDHR,
1948); Ibara ya 19,
Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa (ICCPR, 1966); Ibara ya 19(2)
na Mkataba wa Afrika wa Haki za Binaadam na Watu (ACHPR, 1981) kupitia Ibara ya
9.
Hivyo, kitendo cha Tume kuvitaja
vyombo hivyo hadharani bila ya kuhusisha “majadiliano jumuishi” na wadau inaleta taswira
ya kuzuia uhuru wa kujieleza na haki ya watu kupata
taarifa hasa kipindi hiki cha uchaguzi mkuu.
Katika
mustakbali wa kujenga demokrasia iliyo madhubuti, kazi ya Tume ya Utangazaji ni
kusaidia na kuinua vyombo vya habari ikiwemo kujua maendeleo na changamoto zao
na kuweza kuwatatulia na kwamba jambo la kuwafungia linapaswa kuwa la mwisho
baada ya kufuatwa utaratibu mzuri wa ushirikishi na uwazi.
Katika kufuatilia kwake kwa baadhi ya vyombo hivi, ZAMECO imegundua
kuwa kuna vyombo vimepata changamoto za kifedha na baadhi yake vimehusishwa na
makosa ya kimaudhui ambayo hayajaweza kubainishwa ipasavyo.
Mfano,
Sheria ya Wakala wa Maendeleo na Uanuwai wa Vyombo vya Habari ya mwaka 2022
(Media Development and Diversity Agency Act, 2002) ya Afrika ya Kusini imeweka
mfumo mzuri wa kusaidia vyombo vya Habari, katika kifungu cha 17 cha sheria hii
kimeeleza aina za msaada ambazo inaweza kutoa:
1. Msaada wa kifedha,
kama vile ruzuku za moja kwa moja au fedha za dharura zinazolenga kuimarisha au
kuokoa vyombo vya habari vinavyokabiliwa na changamoto za kifedha;
2. Mafunzo na ujenzi wa uwezo katika
nyanja za uzalishaji na usambazaji wa maudhui ya habari;
3. Msaada usio wa moja kwa moja, kwa mfano kupitia mashirika ya umma au taasisi za kifedha, kwa kupata punguzo la bei au viwango vya chini vya huduma kama vile matangazo, usambazaji wa matangazo ya redio/televisheni, barua, na huduma za simu.
Ni
wito wetu kwamba Tume ya Utangazaji itoe ushirikiano na wamiliki wa vyombo hivi
vya habari na Wadau wa Habari, badala ya kutumia mbinu ya vikwazo ili kuweka
mazingira rafiki kwa vyombo vya habari kufanya
kazi kwa mujibu
wa sheria lakini
bila ya kuathiri uhuru wa
habari. Ni muhimu kuzingatia kuwa katika kipindi cha kuelekea uchaguzi mkuu,
kila sauti na jukwaa la habari lina nafasi kubwa katika kukuza amani,
mshikamano na maamuzi yenye ufahamu miongoni mwa wananchi.
Tume ya Utangazaji ikumbuke kuwa kazi ya Uandishi wa habari ni ya
kitaaluma na ambayo inapaswa kufuata misingi yake na kujiendesha wenyewe na
kwamba vyombo vya sheria ndivyo kimsingi vinapaswa kushughulika na ambao
watakwenda kinyume na taaluma hiyo ya habari.
Sambamba na hilo, ZAMECO inasikitishwa na taarifa inazopokea kwa
Waandishi wa Habari hasa vijana za kunyimwa mashirikiano na watendaji wa
Serikali katika kupata taarifa katika ngazi zote kama kwamba katika kipindi
hichi masuala mengine yeyote yasiendelee. Hii inakatisha tamaa jitihada za
waandishi hawa wa habari ambao wana azma ya kujenga ustawi na haki za makundi
mbali mbali katika jamii na kuonesha kutokuwajibika kwa watendaji.
Wakati huohuo, ZAMECO inapongeza kipindi cha PAMBAZUKO
kinachorushwa na Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC Redio) kwa kuwa jukwaa
muhimu la kuwapa nafasi Wananchi ya kueleza
matatizo yanayoathiri maisha
yao ya kila siku hususan
kwenye eneo la huduma za
kijamii. Kupitia jukwaa hilo, Wananchi hutuma maelezo ya ujumbe mfupi (SMS) na
kusomwa hewani. Kinachofurahisha zaidi ni hatua wanayochukuwa waandaaji kipindi
ya kuwasiliana na watendaji wa Serikali na kuyaeleza matatizo hivyo kushawishi
utatuzi na majibu kutolewa katika muda mfupi.
Ni aina ya vipindi
vinavyohitajika sana kwa kuwa vinashawishi uwajibikaji wa mamlaka
za kiserikali. Na huu ndio mfano bora wa uandishi wa habari unaohimizwa
kwa vile unachochea uwajibikaji, ushirikishwaji na kuchagiza maendeleo ya
jamii.
ZAMECO inaendelea kusimama kidete kutetea
uhuru wa habari,
Uwazi, na Upatikanaji wa Taarifa, ikiamini kuwa jamii inayopata habari sahihi na kwa wakati
ni jamii yenye
nguvu, amani, na inayojua
wajibu wake katika
kulinda demokrasia na maendeleo endelevu
katika nchi.
IMETOLEWA NA:
Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC),
Chama Cha Waandishi
wa Habari Wanawake
Tanzania, Zanzibar (TAMWA-ZNZ) Waandishi wa Habari za
Maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA)
Baraza la Habari Tanzania, Zanzibar (MCT, ZNZ) na
Jukwaa la Watetezi
wa Haki za Binadamu Tanzania, Zanzibar (THRDC, ZNZ).

Post a Comment