MFUMO DUME UNAVYOZIMA NDOTO ZA WANAWAKE KUWA VIONGOZI.

Na Maryam Nassor

“Nilipogombea nafasi ya udiwani kwa mara ya kwanza, sikukutana na changamoto ya wapinzani pekee, bali nilipambana na dhana iliyojengeka kwenye jamii kwamba siasa ni kazi ya wanaume. Wengi waliniambia, wanawake ni wa jikoni, siyo wa majukwaani.”

  Mwanachama  huyo wa chama cha ACT-Wazalendo ni mmoja wa wanawake wachache waliothubutu kugombea nafasi ya uongozi mwaka 2020.

 Asha, mwenye umri wa miaka 38, amesema ndoto yake ilikuwa kushirikiana na wananchi wake katika kuleta maendeleo, lakini mfumo dume uliokuwa ukitawala ndani ya chama na jamii ulimfanya akabiliane na upinzani mkali kutoka kwa wanaume na hata wanawake wenzake.

Anaamini kuwa kila mwanamke ana uwezo wa kuongoza, lakini changamoto kubwa ni vikwazo vinavyotokana na mila, mitazamo ya kijinsia, na mgawanyo wa majukumu ya kifamilia unaowafanya wanawake wengi wasione nafasi ya kushiriki kwenye siasa.

“ Mfumo dume bado ni tatizo katika jamii na  ndani ya vyama vya siasa ambapo mara nyengine unagombea katika uchaguzi wa ndani  wajumbe wanakupitisha anakuja mtu anakwambia  usigombee nafasi hiyo hutoiweza mwachie mwanaume agombee” amesema jambo linalorudisha nyuma jitihada za wanawake katika kugombea nafasi za uongozi.

 Amesema kuwa, wanawake wako wengi kuliko wanaume lakini mifumo dume inawafanya wasisonge mbele na kutimiza ndoto zao za kuwa viongozi.

 “Wanawake tuna nguvu, tuko wengi ukilinganisha na wanaume  na tuna maono. Lakini mfumo dume unatuweka pembeni. Ni jukumu letu sasa kuvunja kuta hizi na kuthibitisha kwamba ndoto za wanawake kuwa viongozi si za kufikirika bali ni za kweli.” amesema.

Kwa upande wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Bahati  Ali Rashid , ambaye ni kada wa chama hicho  na mgombea udiwani wadi ya Kihinani jimbo la Mfenesini  Unguja, amekiri  kwamba bado nafasi za uongozi zimejaa wanaume zaidi ya wanawake.

 ‘’Wanawake tuko wengi, takribani nusu ya wanachama wa chama chetu ni wanawake, lakini unapokuja kwenye maamuzi makubwa, bado mfumo dume unatawala,” amesema Bahati .

 Amewataka ,wanawake mwaka  huu wa uchaguzi kuwaunga mkono wanawake wenzao ambao wamepitishwa na vyama vyao  vya siasa ,kugombea nafasi mbali mbali  za uongozi  ili washinde na kuongeza ushiriki wao kwenye nafasi za uongozi na vyombo vya maamuzi.

Tanzania na Zanzibar tayari zimeridhia Mkataba wa Maputo na Mkataba wa Kimataifa wa Kutokomeza Aina Zote za Ubaguzi Dhidi ya Wanawake  na mkataba wa (CEDAW).

 Ambayo yote yanataka usawa wa kijinsia katika nafasi za uongozi, Pia kuna sera za kitaifa kama Sera ya Maendeleo ya Jinsia ya mwaka 2000 na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, yanayosisitiza usawa wa kijinsia. Lakini pamoja na makubaliano haya, ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi bado ni mdogo.

Takwimu za Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (2024) zinaonyesha wanawake wanaoshikilia nafasi za uongozi kitaifa ni asilimia 30 pekee, ikilinganishwa na wanaume ambao ni asilimia 70. Hali hii inapingana na lengo la kufikia uwakilishi sawa wa 50/50 kama lilivyoainishwa kwenye Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar (ZADEP 2021/2026).

Machavu Bakar Juma ambaye anakaimu nafasi ya  Mwenyekiti wa Ngome ya Wanawake wa ACT-Wazalendo,  amesema changamoto kubwa zaidi ni namna vyama vyenyewe vinavyoendeshwa.

 “Vyama vingi bado vinaongozwa kwa misingi ya mfumo dume. Wanawake wanapopewa nafasi mara nyingi huwaza heshima au kusaidia kampeni, badala ya kusimama kwenye nafasi za maamuzi,” amesema Machavu.

Kwa upande wake, Dkt. Mzuri Issa, Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA-ZNZ), amesisitiza  kuwa wanawake hawapaswi kukata tamaa. “Iwapo tutakubali mfumo dume ututawale, hatutafika. Wanawake wanapaswa kujitokeza kugombea nafasi zaidi  katika uchaguzi wa mwaka huu  2025 ili tufikie lengo la 50/50.”

Sheria  ya Vyama vya Siasa ya mwaka 1992  ambayo imeongezwa  Kifungu cha 10C, inavitaka vyama  vyote kuwa na sera ya jinsia na kuhakikisha wanawake wanashiriki ipasavyo katika siasa na uongozi.

Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa Zanzibar, Mohamed Ali Ahmed, amesema kifungu hicho ni hatua muhimu ya kuvunja mfumo dume ndani ya vyama. “Vyama sasa  vinatakiwa kuhakikisha wanawake wanapata nafasi sawa na wanaume,” amesema Mohamed.

Hata hivyo, bado changamoto kubwa ni utekelezaji wa sera na sheria hizo. Mara nyingi zipo kwenye makaratasi lakini hazionekani katika vitendo.

Ripoti ya Sensa ya Watu na Makazi ya 2022 imeonyesha Zanzibar ina wanawake wengi zaidi (asilimia 51.6 ya wakazi wote), lakini uwiano huo hauakisi kwenye uongozi. Wanawake wachache zaidi ndiyo waliowahi kugombea na kushinda nafasi za majimboni, huku wengi wakipata uwakilishi kupitia viti maalum pekee.

                                              Mwisho

No comments

Powered by Blogger.