WANDISHI WA HABARI WATAKA KUPATIWA TAARIFA SAHIHI KUELEKEA UCHAGUZI MKUU WA 2025.


Zanzibar- Sept 28, 2025

Siku ya haki ya kujua duniani ni siku muhimu hasusan katika kuimarisha ufahamu wa wananchi
na waandishi wa habari kama nguzo kuu za kuimarisha demokrasia, utawala bora na uwajibikaji
ambapo ni vigezo muhimu katika kuleta maendeleo ya nchi, ufanisi wa wananchi na haki yao ya
msingi ya kuweza kufahamu na kujua masuala mbali mbali ambayo yataweza kuimarisha maisha
yao na kuwa na maendeleo katika jamii na taifa kwa ujumla.

Siku  hii ya  kujua huadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 28 Septemba, kwa lengo la kukuza uelewa kwa wananchi na hata waandishi wa habari juu ya haki hii, kwani imekuwa ni changamoto kupata taarifa muhimu pale wananchi au waandishi wa habari wanapohoji masuala  mbalimbali ya shughuli za serikali au taasisi za binafsi.

Katika maadhimisho haya, tunapenda kuangazia umuhimu wa haki hii kama chombo cha  kuimarisha demokrasia na uwajibikaji ambapo kaulimbiu ya mwaka huu ni “Kuwezesha upatikanaji wa Taarifa za Mazingira katika Ulimwengu wa Kidijitali.” (“Ensuring Access to  Environmental Information in the Digital Age).

Katika dunia ya leo, changamoto za kimazingira kama mabadiliko ya tabianchi, uchafuzi wa hewa  na maji, uharibifu wa misitu na rasilimali asili zinahitaji wananchi wapate taarifa kwa haraka na  kwa usahihi ili kushiriki kikamilifu katika maamuzi ya maendeleo endelevu.

Siku hii haikuja kwa bahati mbaya bali ni muhimu iliyotambuliwa na kuridhiwa  na Umoja wa  Mataifa chini ya tamko la haki za binaadamu la (Universal Declaration of Human Right) mwaka 1948 na  Tamko la Umoja wa Mataifa la Haki za Kisiasa na Kiraia(ICCPR) kama ni sehemu ya
uhuru wa kujieleza  kwa jamii.

Tunapoelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, ni muhimu kusisitiza nafasi ya haki ya kujua kama msingi wa demokrasia na inayowapa wananchi uwezo wa kupata taarifa sahihi, kwa wakati, na kwa uwazi kuhusu wagombea, vyama vya siasa, sera, taratibu za uchaguzi na matumizi ya rasilimali za umma kwani bila ya taarifa, wananchi hawawezi kufanya maamuzi
sahihi katika mchakato wa uchaguzi.

Aidha haki ya kujua huwezesha wananchi kufanya maamuzi sahihi kwa kuzingatia sera na mipango ya wagombea, hupunguza uvumi na taarifa potofu pia huimarisha uwajibikaji wa vyama vya siasa, wagombea na taasisi za umma.

Hata hivyo ni lazima tukiri kuwa bado kuna upatikanaji mdogo wa taarifa muhimu kutoka kwa taasisi za umma na ucheleweshaji wa taarifa rasmi au utolewaji wa taarifa zisizo kamili na kuenea kwa habari za upotoshaji (fake news) kupitia mitandao ya kijamii.

Changamoto nyengine ni ukosefu wa usawa katika upatikanaji wa taarifa na zaidi kwa waandishi wa habari kuzingatia habari za matukio na sauti za viongozi na kuacha kuripoti habari za makundi ya pembezoni na wananchi wa vijijini ambao nao wana nafasi kubwa katika hatua mbali mbali za uchaguzi.

Hivyo wakati huu wa kuadhimisha siku ya kujua ni muhimu kwa vyombo na waandishi wa habari kuhakikisha taarifa zinazotolewa ni sahihi, zenye usawa, uhuru na bila kuwa na upendeleo wa vyama au wagombea. Ni muhimu kufanyakazi kama walinzi wa demokrasia na kuimarisha vyanzo tofauti vya habari pamoja na sauti za wasio na sauti ili lengo la kuwa na siku ya kujua
liimarike na kuzingatia makundi yote.

Pia ni muhimu kufahamu kuwa Katiba ya Zanzibar ya 1984 chini ya  Ibara ya 18 ambayo inaeleza haki ya kila mtu kutafuta, kupokea na kutoa taarifa bila kizuizi, isipokuwa kwa mipaka ya kisheria inayolinda usalama wa taifa, maadili au haki za wengine sambamba na kanuni za Maadili ya
Uchaguzi Zanzibar zinazohimiza vyombo vya habari na wadau wote kutoa taarifa sahihi, na Tume kushirikiana na wananchi katika utoaji wa taarifa.

Mambo makuu yanayohusu haki ya wananchi kupata taarifa ndani ya sheria ya Uchaguzi ya
mwaka 2017 ni:

- Kutoa taarifa za uchaguzi: ZEC ina wajibu wa kutoa taarifa kuhusu uandikishaji wa wapiga kura, maeneo ya kupigia kura, majina ya wagombea walioteuliwa, na matokeo ya
kura.
- Uwajibikaji wa ZEC: Sheria inailazimisha ZEC kuchapisha taarifa muhimu katika Gazeti  la Serikali na vyombo vya habari, ili wananchi wapate ufahamu wa mchakato mzima.
- Uangalizi na uwazi: Sheria inaruhusu wawakilishi wa vyama vya siasa, waangalizi wa uchaguzi na waandishi wa habari kusimamia baadhi ya hatua za uchaguzi ili kuhakikisha
uwazi.

Aidha kwa upande wa waandishi na Vyombo vya habari pia kumekuwa na changamoto ya upatikanaji wa taarifa, vitisho kwa waandishi wa habari pamoja na kutokuwepo kwa uhuru wa uhariri katika vyombo vya habari na kuzingatia habari za matokeo bila ya kuwa na uchambuzi yakinifu.

Katika muktadha huu , Kamati ya Wataalamu wa masuala ya habari Zanzibar (ZAMECO) inasisitiza umuhimu wa Serikali na Taasisi husika kuzingatia Sheria na Kanuni zinazohakikisha upatikanaji wa taarifa na  Serikali  kuimarisha mifumo ya uwazi, kutoa mafunzo kwa watumishi wa umma, na kuhamasisha jamii kuhusu haki ya kujua.

Kwa waandishi wa habari kuzingatia weledi na umahiri katika kuleta ufanisi wa kazi zao
na kuripoti pale inapotekea vitisho, kuvunjiwa haki na kudhalilishwa wakati wakiwa
katika majukumu yao.

Haki ya kujua si chaguo, bali ni msingi wa uchaguzi huru, wa haki na wa kuaminika.

Tunatoa wito kwa wadau wote - Serikali, Tume ya Uchaguzi, Vyombo vya habari, Asasi za kiraia na Wananchi — kushirikiana kuhakikisha kuwa Uchaguzi Mkuu wa 2025 unafanyikakwa uwazi na wananchi wanapiga kura wakiwa na taarifa sahihi.

Dkt. Mzuri Issa,
Mkurugenzi, TAMWA ZNZ.

                                                                         Abdallah Mfaume                                                                                                  Mwenyekiti ZPC. 

No comments

Powered by Blogger.