WANAWAKE NA NAFASI ZAO MUHIMU KATIKA JAMII: MCHANGO WAO KATIKA UCHUMI, USALAMA WA CHAKULA NA MAAMUZI YA KIJAMII





NA MARYAM NASSOR,

WANAWAKE wanatambulika duniani kote kama nguzo muhimu ya maendeleo ya familia na jamii kwa ujumla, Ingawa mara nyingi kazi zao hazionekani moja kwa moja katika takwimu rasmi.

Mchango wao katika uchumi wa kaya, usalama wa chakula, maamuzi ya familia na kijamii ni mkubwa na wa lazima. Katika vijiji na jamii nyingi za Kiafrika, wanawake huchukua jukumu kubwa la kuhakikisha familia inapata kipato, chakula na ustawi wa kijamii.

Kwa mujibu wa  takwimu kutoka Shirika la Chakula na kilimo la Umoja wa Mataifa ( FAO) zinaonesha  kuwa, katika nchi zinazoendelea asilimia 43 ya nguvu kazi ya kilimo ni wanawake,  ambapo wana mchango mkubwa katika uzalishaji wa chakula, wanazalisha  chakula  kwa asilimia 60/80.

Ripoti ya Mradi wa Maendeleo  wa Umoja wa Mataifa ( UNDP)   ya mwaka  (2023)  inaonesha kuwa nchini Tanzania  asilimia 67 ya wafanyakazi  wa kike wameajiriwa katika kilimo na takwimu za IFAD zinaonesha kuwa wakulima wadogo wadogo wengi wao wakiwa ni wanawake ambapo huzalisha asilimia 80 ya chakula nchini.

Wanawake hushiriki katika shughuli mbalimbali za uzalishaji mali kama vile kilimo, ufugaji, biashara ndogo ndogo na ufundi. Pato linalopatikana kupitia juhudi hizi hutumika kulipia mahitaji ya msingi kama vile chakula, ada za shule, huduma za afya na makazi.

Akizungumza na mwandishi wa Makala hii, Asmaa Sadiki mnufaika wa mradi wa Zanz Adapt kutoka Shehia ya  Bungi, mkoa wa kusini Unguja amesema kupitia mradi huo, wamepata uwelewa mkubwa wa uhifadhi wa chakula na  kutambua mchango wao kiuchumi  na kijamii katika familia.

Amesema kuwa, Ujuzi na mafunzo waliyoyapata kutoka mradi huo, umewabadilisha  maisha yao kiuchumi na kimtazamo kwani wanaziona fursa nyingi kupitia kilimo na usarifu wa mazao.

“ Kwa sasa tumejiajiri kupitia  kilimo na  usarifu wa mazao  kwa kutengeneza jamu, achari , tomato na majani ya chai ambapo vipato vyetu vimeongezeka” amesema Asmaa.

 Amesema kuwa, Utafiti unaonyesha kuwa wanawake wanapopata kipato, sehemu kubwa ya fedha hizo hutumika kwa maendeleo ya familia kuliko matumizi binafsi. Hii inaonesha wazi kuwa mchango wa wanawake ni msingi wa ustawi wa kaya na Familia.

“ Kupitia elimu tuliyoipata katika mradi wa Zanz Adapt   tumeweza  kushiriki katika shughuli mbali mbali za kiuchumi, kijamii na kukuza pato la familia zetu” amesema Asmaa.

 Wanawake na Usalama wa Chakula

Kwa mujibu   wa tafiti kutoka  shirika la chakula duniani  ( FAO ) ya mwaka 2021 inasema, Wanawake ndiyo wazalishaji wakuu wa chakula vijijini, wakihusiana moja kwa moja na kilimo cha mazao ya chakula, usindikaji na uhifadhi. Pia wao ndiyo wanaohakikisha mlo bora kwa familia.

 Zakia Mansab mkaazi wa Unguja Unguu na mkulima kiongozi, amesema Wanawake wanahakikisha kuwepo kwa usalama wa chakula nyumbani na katika jamii kwa ujumla.

 “ Bila nguvu kazi ya wanawake, changamoto za upungufu wa chakula zingekuwa kubwa zaidi hasa huku vijijini kwani baadhi ya wanaume  hawashiriki kikamilifu katika  shughuli za udhalilishaji  “ amesema Zakia.

Aidha amesema kuwa, kupitia mradi wa Zanz Adapt wamejifunza mambo mengi ikiwemo kilimo msitu, upandaji mikoko lakini pia usarifu wa mazao , hivyo umesaidia utuzaji wa chakula.

‘’Tuna shukuru sana mradi huu wa Zanz Adapt kwa kweli umetusaidia , zamani msimu wa matunda tulikuwa tunayatumia na msimu ukimalizika ndio basi lakini kwa sasa tunaweza kuyasarifu na kuyatumia baadae” amesema Zakia.

 

 Ushiriki wa Wanawake katika Maamuzi ya Kaya

 Asha Bakar  mkaazi wa Shehia ya Unguja ukuu, amesema kuwa Mwanamke anaposhiriki katika maamuzi ya kifamilia—hasa yanayohusu bajeti, elimu ya watoto na afya—maisha ya familia huwa bora zaidi.

  Amesema kuwa ,Hata hivyo  mila na desturi katika jamii nyingi bado hupunguza nafasi ya mwanamke kushiriki  katika maamuzi kikamilifu, Kupaza sauti za wanawake na kuwashirikisha ni msingi wa ustawi wa kijamii na kiuchumi.

 Mchango wa Wanawake katika Maisha ya Kijiji

Katika vijiji vya Unguja Ukuu , wanawake  wana mchango mkubwa  na huchangia katika maendeleo ya Taifa kupitia shughuli za kijamii kama vikundi vya akiba, vikoba na ushirikiano wa kijamii.

  Asha Bakar mkaazi wa Kijiji hicho amesema, Wanawake mara nyingi huendesha miradi midogo midogo ya kilimo na  maendeleo inayosaidia sio kaya zao tu bali jamii kwa ujumla.

“ Kwa mfano, miradi ya bustani za kijiji au vikundi vya usindikaji vyakula huchangia ajira na kipato kwa wanakijiji wengi “ amesema Asha.

 Wanawake na Maamuzi ya Kijamii

 Asha amesema kuwa, Hata kama mara nyingi nafasi za uongozi hukaliwa na wanaume, wanawake wanapopewa nafasi ya kushiriki katika mikutano ya kijiji na maamuzi ya jamii, maamuzi hayo huwa jumuishi zaidi.

  Aidha amesema kuwa, Ushiriki wao hupelekea huduma bora za kijamii kama elimu, maji safi na afya, kwa sababu wanawake huelekeza mawazo yao kwenye mahitaji ya msingi ya familia na jamii kwa ujumla.

Wanawake na Uchumi wa Jamii

 Salama Juma  mkaazi wa  Shehia ya Unguja ukuu.  amesema Wanawake wanaposhirikishwa ipasavyo katika shughuli za kiuchumi na kijamii, pato la jamii huongezeka.

Amesema kuwa, Hii ni kwa sababu wanawake huleta mawazo mapya, ubunifu na nidhamu ya kifedha. Miradi ya maendeleo inayoongozwa na wanawake mara nyingi hufanikiwa zaidi kutokana na mshikamano na uwajibikaji wao.

“Mchango wa wanawake katika familia, kijiji na jamii kwa ujumla ni muhimu na hauwezi kupuuzwa, Ni dhahiri kuwa wanawake ni nguzo kuu za uchumi, usalama wa chakula, ustawi wa familia na maendeleo ya kijamii” amesema Salama.

 Aidha amesema kuwa, ni  wajibu wa jamii na serikali kutambua mchango huo, kuwawezesha wanawake kwa elimu, mitaji na nafasi za uongozi ili kuhakikisha usawa na maendeleo endelevu.

Peter Shaaban ni Afisa kilimo na teknolojia kutoka mradi wa ZanzAdapt amesema katika mradi huo wamewawezesha wanawake wa vijiji vya Unguja ukuu, Uzi, Ngambwa na Bungi   kulima kisasa  na kukabiliana  na athari za  mabadiliko ya tabianchi.

Aidha amesema kuwa, katika mradi huo zaidi ya asilimia 80  ya walengwa wa mradi  ni wanawake ambao ni 2,400 na wanaume ni 600 .Top of Form

                                 Mwisho

 Bottom of Form

 



No comments

Powered by Blogger.