WANAWAKE NA HAKI YA KUMILIKI ARDHI NA RASILIMALI ZA UZALISHAJI: FURSA NA CHANGAMOTO ZANZIBAR


NA MARYAM NASSOR

UMILIKI na udhibiti wa ardhi ni msingi muhimu wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi, Katika jamii nyingi  hasa zile za Afrika Mashariki.

Ardhi ndiyo chanzo kikuu cha uzalishaji mali, usalama wa chakula na urithi wa kifamilia, Hata hivyo wanawake kwa muda mrefu wamekuwa wakikabiliwa na changamoto kubwa za kupata haki sawa ya kumiliki na kudhibiti ardhi na rasilimali za uzalishaji.

Katika muktadha wa Zanzibar, wanawake wanachangia pakubwa katika kilimo na kazi za uzalishaji, lakini bado idadi kubwa hawana haki ya kisheria wala kijamii ya kudhibiti ardhi.

 Hali hii imesababisha wanawake wengi kukosa uhuru wa kufanya maamuzi kuhusu ardhi, kushiriki kikamilifu kwenye shughuli za kiuchumi, na kubaki nyuma katika maendeleo.

Sheria ya Ardhi Zanzibar Inasemaje

Sheria ya Ardhi Zanzibar (Land Tenure Act, 1992) pamoja na marekebisho yake, inatambua haki ya kila mwananchi kumiliki na kutumia ardhi bila kujali jinsia.

Kifungu cha 5 cha Sheria hiyo kinasisitiza kuwa ardhi yote ni mali ya umma chini ya mamlaka ya Rais, lakini kila raia anayo haki ya kupewa umiliki au matumizi ya ardhi kwa mujibu wa taratibu, kwa maneno mengine, hakuna kizuizi cha kisheria kinachomnyima mwanamke kumiliki ardhi Zanzibar.

 Changamoto kubwa inabaki kuwa ni mitazamo ya kijamii na mila zinazomnyima mwanamke nafasi hiyo.

Nafasi ya Ndoa Rasmi katika Kulinda Haki za Wanawake

Ndoa rasmi ni nyenzo muhimu kwa mwanamke kuhakikisha anapata haki zake za ardhi na mali.

Shekh Ali Abdalla kutoka Msikiti wa Fuoni wilaya ya Magharibi ‘B’ Unguja  anasema, Mwanamke anapokuwa katika ndoa isiyo rasmi (kama ndoa ya kimila au bila kusajiliwa kisheria), mara nyingi anakosa haki ya kurithi mali za mume endapo mume atafariki.

  Amesema ,Sheria za urithi Zanzibar  kupitia Sheria ya Mahakama ya Kadhi, zinatoa mwongozo wa namna mali inavyogawanywa.

“Hata hivyo, haki za mwanamke hupata nguvu zaidi pale ndoa  ambapo imesajiliwa kisheria, jambo linalomlinda baada ya kifo cha mume wake kupata haki zake” amesema .

Haki za Mwanamke Baada ya Talaka na Kifo

Wanawake wengi hukosa taarifa sahihi kuhusu haki zao baada ya talaka au kifo cha mume. Kwa mujibu wa sheria na taratibu za Mahakama ya Kadhi Zanzibar:

Shekh Ali  amesema , Mwanamke aliyepewa talaka anastahili kupata haki zake za matunzo (nafaka) hasa ikiwa ana watoto wadogo.

 Aidha anasema  kuwa, Endapo mume atafariki  mjane ana haki ya urithi kwa mujibu wa masharti ya dini ya Kiislamu na sheria za urithi, na hii inaweza kuwa sehemu ya ardhi au mali nyinginezo.

“Wanawake pia wana haki ya kushiriki katika mgawanyo wa mali zilizochumwa pamoja katika ndoa  ikiwa mume atafariki ikiwemo ardhi” amesema .

Umuhimu wa Mabadiliko ya Mitazamo ya Kijamii

Salama Juma Mkaazi wa  shehia ya Unguja Ukuu amesema, Ingawa sheria zinatoa mwanya kwa wanawake kumiliki ardhi, bado kuna vikwazo vikubwa vinavyotokana na fikra za kijamii.

“ Jamii nyingi bado zinaamini kuwa ardhi ni ya wanaume pekee, na kwamba mwanamke anapaswa kutumia ardhi kupitia baba, kaka au mume” amesema Salama .

Amesema kuwa, baada ya kupata elimu ya umuhimu wa umiliki wa ardhi kutoka katika mradi wa Zanz Adapt anamiliki ardhi yake mwenyewe ambayo anaitumia kwa shughuli za kilimo.

“ Baada ya kupata elimu ya umuhimu wa kumiliki ardhi sasa na mimi namiliki  ardhi yangu   ambayo naitumia kwa ajili ya kilimo” amesema Salama huku akiwataka wanawake wengine kuona umuhimu wa kumiliki ardhi.

  Aidha amesema kuwa, Ili kubadilisha mitazamo ya jamii juu ya umiliki wa ardhi , elimu na uhamasishaji ni nyenzo muhimu.

 Amesema , Wanawake wanapaswa kuelimishwa kuwa wana haki ya msingi ya umiliki wa ardhi na rasilimali za uzalishaji. Kauli mbiu ya “Wanawake wanaweza na wanapaswa kumiliki ardhi” ni muhimu katika kuondoa vikwazo vya kimtazamo.

 Bi Furaha  Yassini  mkaazi wa Uzi mkoa wa Kusini Unguja amesema, Haki za wanawake kumiliki na kudhibiti ardhi na rasilimali za uzalishaji Zanzibar zipo kisheria, lakini changamoto kubwa inabaki kwenye utekelezaji na mitazamo ya kijamii.

 Aidha  amesema kuwa, Serikali,  jamii na taasisi za kiraia zina jukumu la kushirikiana katika kutoa elimu, kuhamasisha mabadiliko ya fikra, na kuhakikisha wanawake wanapata nafasi sawa katika umiliki na matumizi ya ardhi.

“ Kuna umuhimu mkubwa kwa wanawake kumiliki ardhi kwani, wanakuwa na uhakika na    wanachokilima kuwa chao,  ikitokea umelima shamba ya mume  na  mumeachana mwanamke huwa huna chako’’ amesema .

Nae, Sheha wa shehia ya Unguja Ukuu Khamis Ibrahim Shomari amesema bado elimu inahitajika kwa jamii juu ya umuhimu wa wanawake kumiliki ardhi.

Amesema kuwa, Serikali na taasisi binafsi zishirikiane katika kutoa elimu hiyo kwani jamii bado hawajaona umuhimu mkubwa kwa kumiliki ardhi na kuwa na hati za umiliki kisheria.

" Jamii bado hajawa na uwelewa mkubwa wa kumiliki ardhi na kuwa na hati miliki za maeneo yao  elimu zaidi inahitajika hasa huku vijini " amesisitiza . 

John Ngonyani ni Afisa kutoka  Jumuiya ya Kuhifadhi Misitu Pemba (CFP) amesema,  changamoto kubwa inayowapamba wakati wanatekeleza mradi huo mkoa wa kusini Unguja , wanawake wengi hawamiliki ardhi.

Amesema kuwa, kutokana na  Sheria ya Ardhi Zanzibar (Land Tenure Act, 1992) pamoja na marekebisho yake, inatambua haki ya kila mwananchi kumiliki na kutumia ardhi bila kujali jinsia, lakini ni asilimia 24.7 tu  ya wanawake ambao ndio wanamiliki ardhi ukilinganisha na wanaume .

 “ Ipo haja kubwa ya kuhamasisha jamii na wanawake kuona umuhimu wa kumiliki ardhi na kuwa na hati za umiliki  kisheria  kwani wananchi wengi hawajui umuhimu huo” amesema John.

 

Mwisho         Bottom of Form

  

 

 

 

 M     MM

 

No comments

Powered by Blogger.