CHANGAMOTO ZA WATU WENYE ULEMAVU WA UZIWI KATIKA MAHOSPITALI YA ZANZIBAR


NA MARYAM NASSOR,

 WATU  wenye ulemavu wa usikivu (viziwi) ni miongoni mwa makundi maalum yanayohitaji huduma za afya zenye mazingira rafiki na ya kueleweka.

 Zanzibar, kama sehemu nyingine duniani, viziwi wanakutana na changamoto kubwa wanapohitaji huduma za kitabibu katika hospitali na vituo vya afya. Lugha ya alama ndiyo njia kuu ya mawasiliano kwao, lakini mara nyingi hakuna wakalimani wa lugha hiyo katika hospitali.

 Hali inayopelekea ukosefu wa mawasiliano kati ya mgonjwa na mhudumu wa afya. Makala hii inaleta taswira ya changamoto wanazopitia viziwi, mtazamo wao, msimamo wa serikali, maelezo ya viongozi wa afya, na nafasi ya sheria katika kulinda haki zao.

Akizungumza na mwandishi wa Makala hii, Faidha  Abdalla mwanamke mwenye ulemavu wa uziwi huko Nyumbani  kwao  Mkokotoni wilaya ya Kaskazini ‘A’ Unguja amesema   changamoto kubwa  zinazowakumba  Viziwi wanapofika hospitali mara nyingi  huwa ni mawasiliano.

Amesema , alishawahi Kwenda katika Hospital ya  Wilaya akakosa huduma kutokana na kushindwa kujielezea kwa daktari na kuamua kurudi nyumbani.

 Kuna siku nilikuwa naumwa na homa ,nilishindwa kupata huduma  Hospital kwa sababu daktari hanielewi na  yeye hajui lugha ya alama, akanishauri nikienda  kupata huduma niende na ndugu yangu anaenielewa” anaeleza Faidha akitafsiriwa  na mkalimani.

 Amesema  kuwa , wanashindwa kueleza matatizo yao kwa madaktari na wauguzi, na Hali hiyo husababisha kucheleweshwa kupata huduma, kupatiwa matibabu yasiyo sahihi, au hata kutengwa.

Ameeleza kuwa, hospitali nyingi hazina wakalimani wa lugha ya alama, jambo linaloleta ugumu wa kupata huduma ya haraka,

Aidha amesema kuwa,Mara nyingine  viziwi hulazimika kuja na ndugu au rafiki wa kutafsiri, lakini si kila wakati wanakuwa na mtu wa kuambatana nao.
“Mara nyingi tunalazimika kuja na ndugu kutusaidia kutafsiri. Lakini afya ni siri, mtu anaweza kutaka kumueleza daktari tatizo lake binafsi, lakini anashindwa kwa sababu hana wakalimani. Hii ni sawa na kukosa haki yetu ya usiri na matibabu bora.”

Aidha amesema kuwa, Baadhi ya watumishi wa afya hufanya mzaha au kupuuza mahitaji ya viziwi, kutokana na ugumu wa mawasiliano. Hali hiyo  hupelekea viziwi kuhisi kudharauliwa na haki zao za msingi  kuhisi haziheshimiwi.

Amesema kuwa, licha ya kuimarika  kwa huduma za afya Zanzibar lakini bado viziwi hawajawekewa mindombinu rafiki katika Hospitali, kwani   nyingi  hazina mabango au maandishi ya kuelekeza huduma kwa maandishi rahisi, jambo linaloweza kusaidia viziwi kupata mwongozo wa huduma.

Viziwi Wenyewe Wanasemaje?

Watu wenye ulemavu wa usikivu Zanzibar wanasema hali ya sasa inawanyima haki ya msingi ya afya. Wengi wanalalamika kuwa wanapofika hospitali wanachukuliwa kama wagonjwa wa kawaida bila kuzingatia changamoto za mawasiliano.

Mmoja wa viongozi kutoka Chama cha  Viziwi Zanzibar (CHAVIZA)  A bdallah Alawi Abdallah amesema  watu wenye ulemavu wa uziwi wanapata shida wakienda katika baadhi ya hospital kwa sababu hakuna wakalimani.

Amesema kuwa, Kwa ujumla, viziwi wanataka serikali iweke mfumo rasmi wa kuhakikisha kila hospitali kubwa ina mkalimani wa lugha ya alama au teknolojia mbadala ya mawasiliano.

Wazazi wa  Watoto Wenye  Ulemavu wa Uziwi  wanasemaje.

Farida Kassimu mama wa mtoto mwenye ulemavu wa uziwi amesema ,Changamoto zinazowakumba viziwi katika hospitali za Zanzibar zinagusa haki ya msingi ya afya na heshima ya utu wao.

Amesema , Ukosefu wa wakalimani wa lugha ya alama, miundombinu rafiki, na uelewa wa watumishi wa afya huathiri pakubwa ustawi wa kundi hilo. Ingawa serikali imetoa ahadi na sheria zipo, bado utekelezaji wake ni changamoto.

Mussa Adhani Juma  baba wa mtoto mwenye ulemavu wa uziwi amesema, Ni muhimu Zanzibar ikawekeza zaidi katika kuajiri wakalimani wa lugha ya alama, kutoa mafunzo ya mawasiliano jumuishi kwa watumishi wa afya, na kuhakikisha miundombinu ya hospitali inakuwa rafiki kwa watu wenye ulemavu.

“Viziwi nao wana hamu ya kuona haki zao zikiheshimiwa na maisha yao yakiboreka bila ubaguzi” amesema Mussa Kwa jumla, hatua za dhati za kiutendaji ndizo zitakazohakikisha  watu wenye uziwi wanapata huduma za afya bora, na heshima sawa kama wananchi wengine.

Kauli za Viongozi wa Afya Zanzibar

Serikali ya Zanzibar, kupitia Wizara ya Afya, imekuwa ikitambua changamoto hizo. Viongozi kadhaa wa serikali wameeleza kuwa kuna mpango wa kuimarisha huduma kwa watu wenye ulemavu kupitia sera za afya shirikishi.

Daktari Dhamana katika Hospital ya Wilaya ya Kivunge Mkoa wa Kaskazini  ‘A’ Unguja , Haji Machano amesema katika hospital hiyo hakuna mkalimani anayeweza kumsaidia mtu mwenye ulemavu wa uziwi akifika katika hospital hiyo.

Amesema kuwa, mara nyingi watu wenye ulemavu wa uziwi  wanakuja Hospital na ndugu au jamaa zao wanaoweza kuelewana na wao ndio wanawasaidia kutafsiri kama wakalimani kwa madaktari au wahudumu wa afya.

“Mpaka sasa katika hospitali yetu ya wilaya ya Kaskazini ‘A’ Unguja Kivunge hatuna wakalimani kinachofanyika watu wenye ulemavu wa uziwi huja na jamaa au ndugu wa karibu kuwatafsiria ndipo wapate huduma” amesema Dr Haji.

Sheria na Haki za Viziwi

Sheria za Zanzibar na zile za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinatambua haki za watu wenye ulemavu. Kwa mfano, Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya 2006 ya Zanzibar inalenga kulinda na kuendeleza haki za watu wenye ulemavu, ikiwemo kupata huduma za afya bila vikwazo.

 Zanzibar imeridhia Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Haki za Watu Wenye Ulmavu (CRPD) ambao unalazimisha serikali kuhakikisha kuna huduma za afya zinazojumuisha wote.

Sheria hizi zinataka huduma za afya ziwe sawa na zinazoweza kufikiwa na watu wote, jambo linalojumuisha kuwepo kwa wakalimani wa lugha ya alama.

Viongozi wa Wizara ya Afya Zanzibar mara nyingi husema wanatambua umuhimu wa kuajiri au kushirikisha wakalimani hospitalini.

Wamekuwa wakiahidi kushirikiana na taasisi za kiraia ili kutoa mafunzo ya lugha ya alama kwa baadhi ya wauguzi na madaktari.

                                Mwisho

 

Top of Form

Bottom of Form

 

 

No comments

Powered by Blogger.