Wanawake Wenye Ulemavu Zanzibar- Changamoto na Fursa za Uwakilishi kwenye siasa


Na Maryam Nassor

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imepiga hatua kubwa katika kujumuisha watu wenye ulemavu katika sekta mbalimbali, ikizingatia mikataba ya kimataifa na misingi ya usawa wa kijinsia kuhakikisha hakuna anayeachwa nyuma.

Hata hivyo, changamoto bado zipo  hususan katika kumjumuisha kikamilifu mwanamke mwenye ulemavu katika siasa ili kufikia malengo ya uwakilishi wa  asilimia 50/50.

Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, asilimia 11.2 ya Watanzania Bara ni wenye ulemavu kati ya zaidi ya watu milioni 60, huku Zanzibar ikionesha idadi kubwa zaidi ya asilimia 11.4 kati ya watu milioni 1.8. Hii ni ongezeko la asilimia 5 ikilinganishwa na takwimu za mwaka 2012.

 Pamoja na wingi huo, uwakilishi wao kwenye taasisi za kisiasa unabaki kuwa mdogo mno.

Kwa mfano, kati ya wajumbe 76 wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, ni watatu pekee wenye ulemavu — wawili kupitia viti maalum na mmoja kwa uteuzi wa Rais wa Zanzibar.

Sauti za Wanawake Wenye Ulemavu

Jamila Borafya,  ni mwanamke mwenye ulemavu wa uoni kutoka MwanaKwerekwe, Wilaya ya Magharibi "B" Unguja, anaeleza changamoto za watu wenye ulemavu wakati wakigombea nafasi za uongozi katika vyama vya siasa.

 Amesema , Mwaka 2020, alijitokeza kugombea nafasi ya Uwakilishi jimbo la Mwanakwerekwe kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), lakini jina lake halikurudi katika hatua za mwanzo za uchaguzi ndani ya chama.

“Changamoto kubwa niliyokumbana nayo ni kwamba vyama vya siasa bado haviamini uwezo wa watu wenye ulemavu kushiriki kwenye siasa za ushindani,” anasema Jamila kwa masikitiko.

Amesema kuwa, watu wenye ulemavu hawapewi haki yao ya kugombea kama watu wengine, hata kwenye nafasi zao  ambazo ni asilimia mbili katika Baraza la Wawakilishi na badala yake wanachaguliwa watu kutoka Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) ambao hawana ulemavu mkubwa na hawajui changamoto zao.

Jamila anaamini nafasi mbili za watu wenye ulemavu katika Baraza la Wawakilishi hazitoshi na hazitoi uwakilishi wa kweli kwa kundi hilo.

Anaeleza kuwa mara nyingi, wawakilishi  hao wanaoteuliwa hupitia Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) na si moja kwa moja kutoka jumuiya za watu wenye ulemavu.

“Wale wanaopelekwa pale kwenye Baraza la Wawakilishi mara nyingi hawajui changamoto zetu. Wanaposhindwa kututetea, si kosa lao  bali mfumo wenyewe hauwahusishi moja kwa moja kutoka  kwenye watu wenye ulemavu,” anasisitiza.

Kwa sababu hiyo, Jamila anaiomba serikali na UWT kuhakikisha uchaguzi mkuu wa oktoba 29 mwaka huu, unawaleta mezani watu wanaotoka moja kwa moja kwenye jumuiya za watu wenye ulemavu ili wakawe watetezi wao.

 

Mtazamo wa Viongozi wa Jumuiya

Bi Salma Haji Saadat, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake Wenye Ulemavu Zanzibar (JUWAUZA), anaweka wazi chanzo kikubwa cha changamoto zinazowakumba watu wenye ulemavu ni  mitazamo ya jamii.

“Jamii bado inawaona watu wenye ulemavu kama ombaomba au wasioweza. Lakini changamoto kubwa siyo ulemavu wao, bali  ni vikwazo vya kijamii vinavyowanyima haki na fursa,” amesema.

Amesema kuwa, tafiti zinaonesha Zanzibar ina idadi kubwa ya watu wenye ulemavu kuliko Bara — jambo linalothibitisha haja ya haraka ya kushirikishwa kikamilifu kwenye sekta zote, ikiwemo siasa.

 Kwa upande wake ,Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Zanzibar (SHIJUWAZA), Mwadawa Khamis Mohammed, anabainisha matumaini mapya kupitia mradi wa CADiR (Collective Action for Disability Rights) unaotekelezwa kuanzia 2025 hadi 2029.

“Mradi huu utaimarisha haki za watu wenye ulemavu kwenye elimu, siasa na sekta nyingine. Ni fursa ya kuhakikisha hatubaki nyuma tena,” anasema.

Wito wa Taasisi za Kiraia

Dk. Mzuri Issa, Mkurugenzi wa  Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA ZNZ)  anasisitiza kuwa watu wenye ulemavu wana uwezo mkubwa na maarifa — wanachohitaji ni kuwezeshwa na kuwekewa mazingira rafiki.

“Ndio maana dunia leo inazungumzia haki sawa. Jamii lazima ibadili mtazamo wake na kuwaona watu hawa kama nguvu ya maendeleo, si mzigo,” anasema Dk. Mzuri.

Msimamo wa Serikali

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Othman Massoud Othman, akizindua rasmi programu ya CADiR, alikiri kuwa bado mahitaji ni makubwa licha ya hatua zilizopigwa.

 Amesema, Serikali imelenga kuongeza uwakilishi wa watu wenye ulemavu kwenye vyombo vya maamuzi kutoka asilimia 2 ya sasa hadi kufikia asilimia 5 ifikapo mwaka 2030.

“Ni jukumu letu kuhakikisha kundi hili linafikiwa na kushirikishwa kikamilifu ili kutetea haki na maslahi yao,” amesema.ToBottom of Form

                             Mwisho

 

 

 


No comments

Powered by Blogger.