UKOSEFU WA WATAALAMU WA AFYA BADO NI KITENDAWILI KWA WAKAAZI WA KISIWA CHA UZI.


 NA MARYAM NASSOR

 KISIWA  cha Uzi   kiko pembezoni mwa  kisiwa cha Unguja  kina mkoa wa kusini, kina  shehia mbili zenye wakazi 4,233.

 Shehia hizo ni  Uzi yenye  wakaazi  3,075 (wanawake 1,510 na wanaume 1,565) na Ng’ambwa yenye wakazi 1,158 (wanawake 571 na wanaume 587). Wote wanategemea Kituo cha Afya cha  Uzi kupata huduma za afya. 

 Kituo  cha Afya cha Uzi kinachotoa huduma za matibabu muda saa za kazi tu; kuanzia saa 1:00 asubuhi hadi saa 9:00 alasiri siku za wiki (Jumatatu hadi Ijumaa). Wikiendi hakuna huduma inayotolewa kituoni  huko.

Uzi ni miongoni mwa visiwa 52 vinavyoizunguka  Zanzibar (saba vinakaliwa na watu vikiwa na huduma muhimu kama vile umeme, maji na vituo vya afya).

Kilio kikubwa cha wakazi wa kisiwani Uzi ni kukosekana  kwa  watoa huduma za Afya ya  uzazi, jambo wanaloliona  linaweka hatarini  maisha ya  mama na mtoto.

Furaha Yassin  (36)  mkazi wa kisiwa hicho, anasema alishuhudia kwa macho yake vifaa vinaondoshwa katika kituo  hicho chaAfya.

 Anasema kuwa, vitu vyengine vilipakiwa kwenye gari hawakujua  wapi vinapelekwa , wakabaki wanajiuliza vinapelekwa wapi .

“ Kwa hiyo mpaka sasa  watu wanaendelea kuzaa katika maboti binafsi yangu alikuja mgeni tukamuuguza kwa uchungu tukatafuta gari ikabidi tumtie kwenye  faiba  akazaa kwenye chombo hicho”


Anasema kuwa, Jengo zuri la Hospitali wanalo lakini hawana madaktari wa kuwahudumia wananchi wa kisiwa hicho.

Jokha Salim ( si jina lake halisi )  almanusura apoteze uhai baada ya kujifungua akiwa katika boti saa nane usiku wakati akipelekwa kupata huduma nje ya kisiwa hicho.

"Ninakumbuka ilikuwa may  mwaka  jana , saa  sita za  usiku  uchungu umenikaza kituo chetu cha afya hakifanyi kazi kwa muda huo lakini pia hakina daktari wa huduma ya mama ya  kujifungua," anasimulia  Jokha .

Mama huyo mwenye  watoto wanne anasimulia Wakati uchungu umekaza, maji ya bahari nayo yameshafungamana kisiwani  huwezi kutumia mtumbwi wa kawaida kutoka nje ya kisiwa  lazima utumie usafiri wa boti.

Usafiri unaotumika kisiwani hapa ni gari au bodaboda (pikipiki) kwa nyakati ambazo maji ya bahari hayajaingia kisiwani na kufunga Barabara  Kutoka hapa Uzi hadi kijiji cha Unguja Ukuu ni wastani wa kilomita tatu. 

Jokha  anasema kuwa wakiwa katikati ya bahari, akipelekwa Kituo cha Afya Unguja Ukuu, alijifungua chini ya usimamizi wa mkunga wa jadi aliyemsindikiza.

"Wakati ninatoka nyumbani kwangu, niliongozana na baadhi ya wanafamilia pamoja na mkunga wa jadi ambaye hutusaidia kutuzalisha wakati wa dharura hapa kisiwani ’’ Anasema.

 Anasema kuwa, Ni jambo la kusikitisha kwamba, kisiwa cha Uzi kina kituo cha afya kizuri, chenye vifaa tiba, lakini hakina wataalamu wa huduma za uzazi.

"Hii kero inatukwaza na kutudhalilisha sisi wanawake kwa sababu wakati wa kujifungua kunahitaji faragha chini ya usimamizi wa wataalamu wa afya.

"Kwa kweli siku ile sitoisahau maishani mwangu, kujifungua katika boti! Lakini ninamshukuru Mungu alinisaidia nikajifungua salama mtoto wangu wa kike ambaye hivi sasa anakaribia kutimiza umri wa mwaka mmoja," anasema Jokha .

Mkasa wa Jokha   unafanana na wa  Zakia  Ali  (32), mama wa watoto  wa wawili  na mkazi wa   kisiwa hicho aliyejifungua ndani ya gari wakati akiwahishwa Hospitali ya Unguja Ukuu nje ya kisiwa hicho.

"Mwaka  (2024), nikiwa na ujauzito wa mtoto wangu wa tano, nilijifungua ndani ya gari mchana kweupe baada ya kukosa wataalamu wa afya katika Kituo cha Afya Uzi.

 Anasema kuwa, Wakazi wa kisiwa hiki wanapobeba ujauzito huwa na hofu kutokana na kituo kutokuwa na wataalamu wa uzazi, hivyo baadhi hulazimika kuyahama makazi yao wanapokaribia kujifungua kwa kwenda kuishi kwa ndugu na jamaa nje ya kisiwa hiki.

"Mimi mimba zangu zote nimejifungua kwa wakunga wa jadi hapa kisiwani. Hii mimba yangu ya mtoto wa tano nilitaka nijifungulie hospitalini kwa sababu wakunga wa jadi sasa wamekatazwa kuzalisha, lakini sikufika hospitalini, nikajifungua ndani ya gari. 

Fadhili Omar  (40) baba wa watoto watano mkaazi wa  kisiwa hicho, anasema kituo chao kina daktari mmoja, hivyo wanahitaji wataalamu wa afya wa kutosha na wawepo kituoni muda wote ili wake zao wasijifungulie kwa wakunga wa jadi.

"Tatizo hili haliwaumizi wanawake tu, hata sisi wanaume linatuumiza, tunapata tabu sana katika kupata huduma. Mimi binafsi nilikwenda na mke wangu katika kituo hicho ili apate huduma ya kujifungua lakini kutokana na kituo kutokuwa na wataalamu wa uzazi, nilimsafirisha kumpeleka Kituo cha Afya Unguja Ukuu tulipofika tu  akajifungua.

"Kama tungechelewa kidogo tu kumfikisha Kituo cha Afya Unguja Ukuu, angejifungulia njiani. Kama hatuna wataalamu wa afya, ninafikiri serikali iendelee kuwapa fursa wakunga wa jadi kuzalisha ili kuwasaidia wajawazito kisiwani kwetu," anasema Fadhil.

 

UONGOZI WA SHEHIA

Othman Mwinyi Haji, Sheha wa Shehia ya Uzi, anakiri kuwepo changamoto ya wataalamu wa afya katika Kituo cha Afya Uzi, akisema: "Kituo chetu cha afya ni kizuri mno, tumejengewa na serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF). Kina vifaa tiba vinavyohitajika na tena tuna mpaka nyumba za kuishi madaktari, lakini kituo hakitoi huduma kwa saa 24.

"Nyumba za madaktari zilizoko hawaishi na hao wachache waliopo katika kituo chetu cha afya wanakuja na kuondoka. Changamoto hii tumeshaiwasilisha katika ngazi za juu serikalini, wananchi kuendelea kuvumilia, serikali itatatua changamoto hii.

"Nyakati za usiku wananchi wa kisiwa hii, hasa wajawazito wanapata shida kutafuta huduma za afya na wakati mwingine hulazimika kujifungulia njiani kabla ya kufikishwa hospitalini au kujifungulia kwa wakunga wa jadi, jambo ambalo ni hatari kwa afya ya mama na mtoto."

WASIMAMIZI WA KITUO

Daktari Dhamana wa Kituo cha Afya Uzi, Seleh Nila Ali, anasema changamoto iliyopo ni uhaba wa wafanyakazi, hasa kwa wakunga. Kituo hicho kina mkunga mmoja na kutokana na uhaba wa wataalamu wa afya kinashindwa kuwazalisha wajawazito.

Anabainisha kuwa kwa mwezi kituo kinatoa huduma kwa wastani wa watu 500 wanaofika kup ata huduma kituoni hapo. 

Daktari huyo anasema kituo kina upungufu wa wakunga watano na madaktari watatu ili kukidhi mahitaji ya kutoa huduma za afya. Anakiri   ni kero kubwa  kisiwani huko kujifungulia kwa wakunga wa jadi.

 Mkurugenzi Kinga  kutoka Wizara ya Afya  Zanzibar, Dk  Salim Slim amesema  Serikali itahakikisha  inapeleka wataalamu wa  Afya wa kutosha katika kituo hicho.

‘’ Ingawa  hatutomaliza tatizo hilo kwa asilimia mia moja  lakini  tutalipunguza kwani hakuna nchi hata moja waliofanikiwa kutatua changamoto za afya kwa asilimia mia’’ amesema Dk Salim.

 Aidha amesema kuwa, suala la wafanyakazi bado lina changamoto lakini wanaahidi wafanyakazi katika kituo hicho watapelekwa hivi karibuni.

                          mwisho

No comments

Powered by Blogger.