UMUHIMU WA SHERIA NZURI ZA HABARI ZANZIBAR



Na -Maryam Nassor

Katika jamii yoyote yenye demokrasia, sheria nzuri ya habari ni msingi wa maendeleo, uwazi, na utawala bora. Sheria nzuri ya Habari huweka misingi inayowezesha uhuru wa vyombo vya Habari.

Inalinda haki za waandishi wa habari na kuhakikisha kuwa raia wanapata habari sahihi na kwa wakati unaofaa. Katika makala haya tutajadili umuhimu wa kuwa na sheria nzuri ya habari na faida zake kwa jamii.

Sheria nzuri ya habari inahakikisha kuwa waandishi wa habari na vyombo vya habari vinaweza kufanya kazi zao bila hofu ya kuingiliwa au kubanwa na mamlaka.

Uhuru huu ni muhimu katika kuhakikisha kuwa vyombo vya habari vinaweza kutoa taarifa za ukweli na kusaidia wananchi kuwa na uelewa wa kina kuhusu masuala mbalimbali ya kijamii, kisiasa, na kiuchumi.

 Akizungumza na mwandishi wa Makala haya, Mjumbe wa Kamati ya Wataalam wa Masuala ya Habari Zanzibar ( ZAMECO)   Jabir Idrissa  anasema Sheria nzuri ya Habari inachangia uwazi katika utawala na taasisi mbalimbali za serikali na binafsi.

Anasema kuwa,  kupitia vyombo  huru vya  habari, wananchi hupata fursa ya kufuatilia shughuli za serikali, kubaini matumizi ya rasilimali za umma, na kuwawajibisha viongozi kwa matendo yao. Hii inasaidia kupunguza ufisadi na kuimarisha utawala bora.

 Aidha amesema kuwa, Sheria nzuri za Habari zitasaidia kulinda haki za wananchi za kupata habari sahihi kwani jamii ina haki ya kupata habari sahihi na kwa wakati.

“Sheria bora ya Habari inayolinda haki  kwa kuhakikisha kuwa vyanzo vya habari vinawajibika na kutoa taarifa zilizo sahihi na zisizo na upendeleo. Hii inasaidia kuepuka upotoshaji wa habari na kusambaa kwa taarifa za uongo,” anasema Jabir.

Naye, mwandishi wa Habari wa kujitegemea Thuwaiba Habibu  amesema Habari ni chombo cha maendeleo, kwani husaidia watu kufanya maamuzi sahihi kuhusu maisha yao. Sheria nzuri ya habari inahakikisha kuwa vyombo vya habari vinatoa habari za kielimu, afya, uchumi, na maendeleo ya kijamii, ambazo zinaweza kusaidia wananchi kuboresha maisha yao.

Amesema kuwa, Sheria nzuri ya habari inapaswa kuwalinda waandishi wa habari dhidi ya unyanyasaji, vitisho au mashambulizi kutokana na kazi zao. Katika mazingira mengi, waandishi wa habari hukabiliwa na changamoto kama vile kushambuliwa, kutishiwa maisha, au hata kufungwa kwa sababu ya taarifa wanazotoa.

Aidha amesema kuwa, Sheria  inapaswa kuwalinda na  kuhakikisha kuwa wanaweza kufanya kazi zao kwa uhuru na usalama bila ya vitisho na shinikizo kutoka vyombo vya dola.

 Shadida Omar  ni Afisa Programu kutoka Ofisi ya Watetezi za Haki za Binadamu Zanzibar ( THRDC) anasema kuwa i Ingawa uhuru wa habari ni muhimu, pia ni muhimu kuwa na sheria inayodhibiti matumizi mabaya ya habari, kama vile uenezaji wa taarifa potofu (fake news), uchochezi, au habari zinazokiuka maadili ya jamii.

Anasema kuwa, Sheria nzuri za Habari inapaswa kuweka miongozo thabiti kuhusu matumizi sahihi ya habari bila kuathiri uhuru wa Vyombo vya Habari nchini.

Aidha anasema kuwa, Sheria nzuri ya Habari ni msingi wa jamii iliyo huru, yenye maendeleo, na inayozingatia haki, inapohakikisha uhuru wa vyombo vya habari, inasaidia uwajibikaji, uwazi, na maendeleo ya kijamii.

 Hata hivyo’’ sheria hizi zinapaswa kuwekwa kwa uwiano mzuri ili zisitumike kama chombo cha kuwakandamiza waandishi wa habari au kuzima uhuru wa habari,” anasema Shadida.

Naye,  Afisa Programu ya Maswala ya Sheria za Habari kutoka Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar  - TAMWA ZNZ , Zaina  Mzee  anasema  serikali na wadau wengine wanapaswa kushirikiana kuhakikisha kuwa kuna mfumo wa kisheria unaounga mkono uhuru wa habari na kupatikana sheria rafiki ya habari itakayotoa  uhuru kwa waandishi.

Anasema kuwa, Sheria nzuri ya Habari itaharakisha Maendeleo kwani waandishi wa  Habari watapata fursa ya kufanya kazi zao bila ya upendeleo wala hofu kutoka kwa wenye mamlaka.

  Akijibu, maswali ya waandishi wa habari, katika kikao cha Tathimini ya Mafanikio ya miaka minne ya Dokta Hussein Mwinyi, Waziri wa Habari Utamaduni, Vijana na Michezo, Tabia Maulid Mwita, amesema  muswada wa Sheria ya Habari upo, katika Kamati ya Ufundi ya Taifa (N TC) ambako unashughulikiwa.

 Katika hatua nyengine, Waziri huyo amesema kuwa anatamani mswada huo ufikishwe katika Baraza la wawakilishi hivi karibuni.

"Sheria ya Habari itasomwa wiki ijayo na Mswada huo kwa  mara ya kwanza unatarajiwa kupelekwa Baraza la Wawakilishi katika kikao kinachoanza tarehe 7 na kwa vile Rais anapenda mambo  yaende  haraka tunatarajiwa sheria hiyo itapitishwa  kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka huu, tutakuwa na sheria mpya ya  Habari" Waziri Tabia katika uzinduzi wa Mfumo mpya wa matangazo  ya ZBC RADIO, SPICE FM NA SPICE TV- huko karume Zanzibar mwezi  huu wa nne mwaka 2025.

Ni zaidi  ya miongo miwili sasa waandishi wa habari na wanaharakati wa haki za binadamu Zanzibar wameendelea kudai Sheria rafiki ya Habari bila ya mafanikio yoyote.

                                    MWISHO


 [U1]

No comments

Powered by Blogger.