ULINZI WA WANDISHI WA HABARI KIPINDI CHA UCHAGUZI BADO NI KITENDAWILI



NA MARYAM NASSOR

PAMOJA na kufanya kazi kubwa ya kuhabarisha umma, waandishi wa Habari  ulimwenguni kote wanakabiliwa na mashambulizi yanayo hatarisha maisha na  usalama wao.

Tafiti zilizofanywa na shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu  Sayansi na Utamaduni “UNESCO”  zimebaini kuwa kati  ya mwaka 2016 na 2020, zaidi ya wandishi wa Habari  1,200 wameuwawa  kwa kuripoti  Habari za umma.

Utafiti huo, umeonesha  kuwa kati ya vifo 10 ni kisa  kimoja tu ndio muhusika au wahusika wanaadhibiwa au kufikishwa mahakamani .

Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa  Antonio Guterres anasema nafasi adhimu ya wanahabari kutumia nafasi yao, kuwezesha demokrasia na kuwajibisha mamlaka iko hatarini kwa sababu ya kufichuwa kwao ukweli.

Akizungumza na mwandishi wa Makala hii, Jesse Mikofu mwandishi wa Habari Mwandamizi kutoka gazeti la Nipashe  Zanzibar amesema  waandishi wa Habari wanafanya kazi kwa ajili ya umma , ni Daraja kati ya  jamii na Serikali  hivyo wanahitaji ulinzi.

 Amesema kuwa ,  kuna umuhimu mkubwa kwa Waandishi wa habari wanapokuwa salama,  kwani wanaweza kufanya kazi zao kwa uhuru bila hofu ya kulengwa na makundi yenye maslahi binafsi.

Aidha amesema kuwa,  waandishi wanatakiwa kujilinda wenyewe kabla hujafikwa na tatizo lolote kwani,hakuna chenye thamani  dhidi ya maisha yako.

“ Mimi binafsi nilishawahi kukutana  na misuko suko kadhaa nilishawahi kuwekwa ndani, wakati nafuatilia Habari ya vitambulisho  kule bara na hapa  Zanzibar pia  wakati nikitimiza majukumu yangu, nilishawahi kupigwa  na hata kupoteza vifaa vyangu ” anasema Jesse. 

Nae, mwandishi wa Habari kutoka sauti ya DW Zanzibar Salma Saidi amesema   waandishi wa Habari hawako salama duniani kote kwa sababu ya kazi zao za kuisemea jamii na kuiwajibisha Serikali .

Amesema kuwa,    Waandishi wa habari wana jukumu muhimu katika mchakato wa kidemokrasia, hasa katika vipindi vya uchaguzi. Wanatoa taarifa kwa umma, kufichua ukweli, na kuhakikisha kuwa wananchi wanapata habari sahihi ili kufanya maamuzi yaliyo na msingi.

“Lakini ukitaka kujua kama hakuna uhuru wa Habari basi mfuate mwandishi umwambie tufuatilie Habari Fulani hakuna aliye tayari kwa hofu ya maisha yake” amesema Salma.

 Aidha amesema kuwa,  kuna umuhimu mkubwa wa ulinzi kwa wandishi wa habari ,kwani  changamoto nyingi, huwakumbwa hasa kipindi cha uchaguzi ikiwa ni pamoja na vitisho, mashambulizi, na ukandamizaji kutoka kwa wadau mbalimbali wa kisiasa.

Aidha amesema kuwa ,Waandishi wa habari wanapokuwa salama, wanaweza kufanya kazi zao kwa uhuru bila hofu ya kulengwa na makundi yenye maslahi binafsi. Hili linahakikisha kuwa habari zinazotolewa hazijachakachuliwa kwa lengo la kupotosha umma.

Nae, mwandishi wa Habari mkongwe Kisiwani Zanzibar  Salim Said Salim amesema Katika historia ya chaguzi nyingi duniani , waandishi wa habari wamekuwa wahanga wa vitisho, utekaji nyara, na hata mauaji. Ulinzi wa kutosha unasaidia kupunguza matukio haya, hivyo kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa amani.

Amesema kuwa, Waandishi wa habari ni miongoni mwa wale wanaowajibisha wanasiasa kwa kuhakikisha kuwa wanatimiza ahadi zao na wanaheshimu misingi ya demokrasia. Bila ulinzi wa kutosha, wanasiasa na taasisi zenye nguvu huweza kuwanyamazisha waandishi kwa vitisho.

   “ Waandishi wa Habari wanapolengwa , jamii kwa ujumla  ndio inalipia gharama kwani wao wapo kwa ajili ya kuiwakilisha  jamii”

Aidha amesema kuwa,  jukumu  muhimu la waandishi wa Habari ni kufichuwa ukweli,  lakini ukweli huo huja na  gharama , hivyo ni vyema wapewe ulinzi  na mamlaka husika ili kutimiza wajibu wao.

Jabir Idrissa ni mmoja wa wajumbe wa kamati ya  Maswala ya Habari Zanzibar ( ZAMECO)  anasema upo umuhimu mkubwa wa ulinzi kwa wandishi wa Habari, kwani wanafanya kazi kubwa ya kuihabarisha jamii na  kuchochea maendeleo.

Amesema kuwa, bila ya wandishi wa Habari wazalendo kwa nchi yao,basi maendeleo hayawezi kupatikana.

“Habari zinazotegemea  ukweli na uchambuzi  hutegemea  ulinzi na usalama  wa wandishi wa Habari wanaofanya kazi zao kwa uhuru, bila woga na upendeleo” anasema Jabir.

Akizungumzia  umuhimu wa ulinzi, kwa waandishi wa Habari hususani kipindi cha uchaguzi , Shadida Mohamed kutoka Ofisi ya Watetezi wa Haki za Binaadamu Tanzania Zanzibar ( THRDC) anasema  wandishi wa Habari wanafanya kazi kubwa hasa kipindi cha uchaguzi, ni vyema ukaangaliwa usalama wao kwanza.

Amesema kuwa, wandishi wa Habari ni kiungo muhimu katika jamii na Serikali kwa ujumla, bila ya wandishi wa Habari hatuwezi kupata taarifa zenye ukweli na uwazi.

Nae, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni ‘UNESCO’ Audrey Azoulay amesema  kutokana na hali hiyo  dhidi ya vyombo vya Habari, Mataifa yana jukumu la kuwalinda wana Habari na kuhakikisha watekelezaji wa uhalifu dhidi ya Wandishi wa Habari wana wajibishwa.


                                               Mwisho

No comments

Powered by Blogger.