UWEZO MKUBWA WA ASKARI POLISI WA KUKAMATA NA KUPEKUWA CHOMBO CHA HABARI NI KILIO KWA WANAHABARI.


NA MARYAM NASSOR

ZANZIBAR ni nchi yenye sheria mbaya ambazo zinaminya uhuru wa habari  kiasi ambacho waandishi wa habari wanashindwa kuandika habari za uchunguzi na kuikosoa Serikali.

Taaluma ya uandishi wa habari ni kazi kama kazi nyengine ambazo zipo rasmi na zinatambuliwa kisheria duniani kote kutokana na umuhimu wake katika kuhabarisha jamii na taifa kwa ujumla.

Inaaminika kuwa tasnia ya habari, kutokana na umuhimu wake inaweza kuwa ni muhimili wa nne wa nchi ukitoa Bunge, Serikali na Mahakama.

Uwepo wa sheria ambayo inampa mamlaka makubwa Askari Polisi kukamata na kupekua gazeti lolote popote linapopatikana kwa kushuku kuwa limechapishwa kinyume na sheria kitendo hicho kinanyima uhuru wa habari nchini.

Kifungu cha 27(1) cha Sheria ya Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu Na.5 ya 1988 na marekebisho yake Na.8 ya 1997 kinasema, “Afisa polisi yeyote anaweza kukamata gazeti lolote, popote linapopatikana, ambalo limechapishwa au ambalo anashuku kuwa limechapishwa, kinyume na Sheria hii.”

Hiki ni kifungu chenye matatizo sana na ni miongoni mwa vifungu vinavyonyang’anya haki ya kutoa habari iliyoainishwa na Katiba.

Akizungumza na mwandishi wa Makala hii, Mjumbe wa Kamati ya masuala ya Habari Zanzibar( ZAMECO ) Jabir Idrisa anasema sheria hii ni kikwazo kikubwa kwa wandishi wa Habari Zanzibar kwani inanyima uhuru wa  Habari na inakwenda kinyume na katiba ya nchi.

Amesema kuwa, uwezo aliyopewa Askari Polisi wa kupekuwa na kukamata gazeti popote litakapopatikana unaathiri uhuru wa habari nchini kwani  waandishi wengi wa habari wana hofu na wasiwasi na vyombo vyao kuandika habari zinazokosoa Serikali na viongozi wake.

Amesema kuwa, “utendaji kazi wa Askari Polisi unajulikana ulivyo si wa kupewa mamlaka hayo, kwani Polisi wengi hawana uelewa wa vyombo vya habari anaweza kuyatumia vibaya mamlaka hayo,” anasema.

Aidha amesema  kuwa, Polisi wanaweza kuyatumia mamlaka hayo vibaya  au kwa upendeleo kulenga vyombo vya upinzani [Ma1] bila sababu za msingi na kupelekea kuviuwa vyombo hivyo.

“Sisi tunataka sheria hii irekebishwe au ifutwe kabisa kwani  ni ya muda mrefu na imepitwa  na wakati” anasema Jabiri.

Naye, mwanasheria  kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar Ali Amour  amesema  , tasniaasisi  ya Hhabari ni fani kama fani nyengine  haiwezi kuingiliwa  na  askari polisi kwa kushuku  tu bila  ya uhakika.

Amesema kuwa ni vyema sheria hiyo ikabadilishwa ili kutoa uhuru wa habari, mamlaka makubwa ya Askari Polisi aliyopewa yanaweza kutumika vibaya na kuathiri uhuru wa habari nchini.

 Aidha mwanasheria huyo, alishauri kuwa kabla Askari Polisi hajapekuwa na kukamata chombo cha habari ni vyema angeshirikiana na Bodi ya Habari kuhakikisha kuwa haminyi uhuru wa habari nchini.

Akizungumzia kuhusu sheria hiyo, mwandishi wa Habari Mkongwe Kisiwani Unguja Bw. Salim Said Salim anasema sheria nyingi zimekuwa zikirekebishwa na mchakato wake hauchukui hata miezi sita, kama Sheria ya Uchaguzi na Sheria ya Huduma na posho kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi.

“Sheria hii ya Habari iko zaidi ya miongo miwili sasa tunafanya uchechemuzi bila ya mafanikio yoyote, je, ugumu wa kurekebishwa uko wapi?” amehoji Bw. Salim.

Amesema kuwa uwezo aliopewa Askari Polisi wa kupekua na kukamata gazeti popote litakapo patikana  na ambalo limechapishwa au anashuku  kuwa limechapishwa kinyume na sheria hii , unaathiri uhuru wa habari nchini.

Aidha ameiomba Serikali kusikiliza kilio cha muda mrefu cha waandishi wa habari na wadau cha kutaka kuwapo kwa sheria rafiki za habari ambazo zitaendana na wakati wa sasa.

Shadida Omar ni Afisa Programu kutoka Mtandao wa  Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania Zanzibar - THRDC  anasema  kifungu cha 27 (1) cha sheria ya Sheria ya Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu kimempa mamlaka makubwa Askari Polisi kupekua au kukamata gazeti au kufungia chombo cha habari, hii inazuia ufanisi wa utafutaji wa taarifa na utoaji wa  taarifa.

Amesema kuwa, sheria  hii ni mwiba kwa vyombo vya habari kwani  inaweza kupelekea Askari kutumia vibaya nafasi hiyo kwa maslahi ya kisiasa kuua vyombo vya habari vinavyomilikiwa na vyama vya upinzani au hata vyombo vya habari binafsi.

Naye Afisa  Programu wa mradi wa sheria kutoka TAMWA ZNZ, Zaina Mzee amesema mradi huu ni muendelezo kuwanoa waandishi wa habari ili wawe mahiri zaidi katika kuchambua masuala ya sheria za habari na kufanya uchechemuzi ili sheria kandamizi zifutwe.

Amesema kuwa, ni vyema waandishi wasichoke kufanya uchechemuzi ili hatimayezipatikane sheria rafiki za habari kwani itasaidia kuondokana na sheria mbaya na ambazo zimepitwa na wakati.

Dkt Mzuri Issa ni Mkurugenzi wa Chama Cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA ZNZ) amesema ni kweli sheria hizi zimepitwa na wakati na zinaenda kinyume na Katiba ya nchi.

“Huu sio wakati tena wa kuwa na sheria kama hizi za habari, hivi sasa dunia imekua kijiji kutokana na maendeleo ya Sayansi na Teknolojia na tunaona umuhimu wa kuwa na uhuru wa habari na jinsi unavyoshajiishwa duniani kote, iweje mpaka leo Zanzibar tuwe na sheria kandamizi za habari?” Amehoji Dkt Mzuri.

Aidha ameongeza kuwa, kwanini Zanzibar haifuati nchi kama Afrika ya Kusini ambayo mara tu baada ya kujikomboa kutoka katika utawala wa ubaguzi wa rangi, walivipa uhuru vyombo vya habari kuandika kwa uwazi na kuikosoa Serikali ili kuharakisha maendeleo.

                          Mwisho


 [Ma1]vyombo vya upinzani ndiyo vipi?

No comments

Powered by Blogger.