MANENO YENYE UKAKASI KWENYE SHERIA ZA HABARI NI KITENDAWILI.



Na - Maryam Nassor  

WAANDISHI wa Habari wa Zanzibar kwa muda mrefu wamekuwa wakililia sheria mbaya za habari zibadilishwe, na kilio hicho kwa takribani miongo miwili sasa kimekuwa kikipita kwenye masikio yenye nta

Sheria ya Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu Namba 5 ya Mwaka 1988  iliyofanyiwa marekebisho na Sheria no. 8  ya mwaka  1997, imekuwa kikwazo kwa wanahabari katika kutekeleza majukumu yao bila hofu kwasababu sheria hiyo ina mitego sana.

  Mkataba wa AFRIKAN CHART OF HUMAN AND PEOPLES RIGHT  unataka  kila nchi lazima ikuze demokrasia na uhuru wa  kujieleza, ingawa  wanaamini kuwa hakuna uhuru ambao hauna mipaka lakini kutokana na sheria mbaya zenye maneno yasiyo na maana halisi yanaufanya  uhuru usiwepo.

Kifungu cha 30(1) kinaeleza kuwa ‘’pale ambapo waziri atakuwa na maoni kwamba ni kwa masilahi ya umma au kwa ajili ya amani na utulivu, anaweza kuamrisha kusimamishwa kwa gazeti na gazeti hilo lazima lisimamishe kazi zake kuanzia tarehe ya amri iliyotolewa…

Kifungu cha 30(1) cha sheria hii kimempa Waziri mamlaka ya kulifungia gazeti kwa sababu mbili ambazo ndio msingi wa Makala hii.

Sababu ya kwanza; Kigezo cha maslahi ya umma, sheria hii haikufafanua maana ya neno ‘masilahi ya umma’ bali imeelezea kuwa endapo Waziri atakuwa na maoni kwamba kulifungia gazeti ni kwa maslahi ya umma, ni hatari sana, kwani maslahi hayo yanaonekana yapo au hayapo kutokana na maoni ya mtu mmoja (waziri) hivyo yameunganishwa na matakwa ya mtu.

Kigezo cha masilahi ya umma kimekuwa kikitumika kwenye sheria nyingi na kwa bahati mbaya hakuna sheria hata moja iliyofafanua neno hilo lina maana gani. Hata hivyo vigezo vifuatavyo vinaweza kuzingatiwa kama ni vigezo vya maslahi ya umma.

i.                    Uhakika wa taarifa husika iliyotolewa na ambao unaweza kuathiri jamii fulani.

ii.                   Taarifa yenye kueneza uchochezi wa siasa au dini;

iii.                 Taarifa yenye kuchochea ubaguzi wa kidini, kikabila au kisiasa.

iv.                 Taarifa za uongo na zenye uchochezi.

Ikiwa Waziri ataelezea moja kati ya sababu za hapo juu kuwa amefungia gazeti kwa sababu hizo inaweza kuzingatiwa kuwa amefungia kwa maslahi ya umma.

Sheria imempa mamlaka makubwa Waziri wakati inafahamika kuwa wadhifa huo ni wa kisiasa, hivyo yupo kwa ajili ya kulinda maslahi ya chama au mamlaka iliyopo, hivyo ikitokea habari ambayo inakosoa upande wake wa kisiasa anaweza kutumia mwanya huu wa sheria kulifungia gazeti husika.

Sababu ya pili; ni kigezo cha amani na utulivu ambacho kifungu cha 30(2) pia hakikufafanuliwa maana yake halisi.

Akizungumza na Mwandishi wa Makala hii, Afisa kutoka Ofisi ya Watetesi wa Haki za Binadamu Zanzibar ( THRDC)  Shadida Mohamed  anasema kuwepo na vifungu vyenye maneno magumu yasiyo na maana halisi katika sheria yanaviza uhuru wa  kujieleza.

Amesema kuwa, kifungu cha 30 cha sheria hii ya Usaliji wa Wakala wa Habari kinasema kuwa  endapo Waziri ataona ni kwa ‘maslahi ya umma’ au kwa ‘amani na utulivu’  anaweza kuamuru kufungiwa kwa gazeti na gazeti litakoma kuchapishwa kuanzia siku hiyo ni kitu kibaya sana kwa tasnia ya habari.

“Hasara ni kubwa kwa waandishi wa habari kutokana na sheria kama hizi ambazo zinakwenda kinyume na mikataba ya kimataifa ya kulinda haki za binadamu,” anasema Shadida.

Amesema kuwa, mamlaka hayo ya kiutendaji ni makubwa kwa Waziri na anaweza kuyatumia kwa maslahi yake binafsi au ya kisiasa badala ya maslahi ya umma, kwani  mawaziri wengi wanateuliwa kutokana na mrengo wa kisiasa.

“Lazimaa Sheria iainishe kwa uwazi maana halisi ya  maslahi ya Umma na Amaani na Utulivu na hali zipi zinaweza kufungiwa kwa gazeti” anashauri Shadida.

Naye, Mwanasheria Ali Amour kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar  anasema kuwa Waziri asipewe mamlaka ya kufungia gazeti kwani hiyo itapelekea kuathiri uhuru wa habari.

Amesema kuwa, hofu ya chombo cha habari kufungiwa inaweza kufanya vyombo vya habari kuepuka kuandika habari zinazokosoa Serikali hata pale panapohitajika.

“Ni vyema sheria zikafafanua kwa uwazi maneno kama hayo kwani yanaathiri vibaya tasnia ya habari,” anashauri Ali.

Naye, mwandishi wa habari mkongwe visiwani Zanzibar, Salim Said Salim anahoji ugumu wa kubadilishwa sheria kandamizi kama hizi uko wapi? Kwani sheria nyingi za zamani zinabadilishwa.

“Waandishi wa Habari tumechoshwa na sheria kandamizi zenye maneno yasiyo na maana halisi, tunataka sheria zinazokwenda na wakati na zinazojali haki za binadamu.” anasema Salim.

Naye, Mjumbe  katika  Kamati ya Wataalam wa Masuala ya Habari Zanzibar (ZAMECO) Jabir Idrissa anasema  sheria ilitakiwa ieleze kwa uwazi na upana wake maana halisi ya maneno  haya, ‘maslahi ya umma’ na ‘amani na utulivu.

Aidha amesema kuwa, dunia sasa imekuwa ni kijiji kutokana na kukua kwa teknolojia, hivyo ni vyema kuwepo sheria nzuri za habari ili waandishi watumie kalamu zao kuikosoa Serikali inapobidi  bila ya hofu ya kufungiwa vyombo vyao.

Zaina Mzee ni Afisa Programu ya Uchechemuzi wa Sheria za Habari kutoka Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania - TAMWA (ZNZ), amewataka waandishi wa habari kuendelea kufanya uchechemuzi kwa kuandika habari na makala ili sheria rafiki za habari zipatikane.

Aidha amesema kuwa, “huu ni wakati wa kuungana pamoja waandishi wa habari na wadau wa habari kupigania sheria rafiki ya habari ipatikane.”

                                Mwisho

 

No comments

Powered by Blogger.