USARIFU WA BIDHAA ULIVYOWAINUA KIUCHUMI WANAWAKE WA MKOA WA KUSINI



 NA MARYAM NASSOR

Katika miaka ya hivi karibuni,  ujuzi wa kusarifu matunda umekuwa  mchango mkubwa katika kuboresha Maisha ya  wanawake katika jamii za vijiji mkoa wa kusini Unguja.

Usarifu wa matunda unahusisha mbinu zakulinda, kuhifadhi  na kutengeneza bidhaa mbali mbali  kutokana na matunda, hali inayopelekea  faida nyingi  ikiwemo kuongezeka kwa kipato, ulinzi wa mazingira  na kusaidia kutunza afya.

Tafiti zinaonesha  kuwa, ujuzi wa kusarifu bidhaa ni nyenzo muhimu kwa maendeleo ya wanawake hasa wa vijijini. 

 Katika Shehia ya Bungi wanawake wanatumia vikundi vya kusarifu    bidhaa kama njia ya kujikwamua kiuchumi na kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi na kijamii.  

Sabra Abdalla Ali kutoka  katika shehia ya Bungi ni Mwenyekiti wa kikundi cha Nani Kaoni akiwa ni mnufaika wa  elimu na ujuzi wa kusarifu mazao kutoka katika mradi wa ZANZI ADAPT.

 Anasema kuwa, hapo zamani msimu wa matunda kama maembe na mapapai walikuwa hawajui umuhimu wa kuyatunza ili  kutumia baada ya msimu kuisha.

 Sabra ambae ni mama wa Watoto  saba, anasema baada ya kupata elimu ya kusarifu matunda na  tea masala kutoka katika mradi wa ZANZ ADAPT   kipato cha wajasiriamali kimeongezeka  na kupata hadi elfu 30 kwa wiki jambo ambalo hapo awali walikuwa hawana.

Amesema kuwa,  wanawake wengi wanajishughulisha na usarifu wa matunda, ambapo wameweza kuanzisha biashara ndogo za kutengeneza na kuuza bidhaa kama juisi,  jamu na pilipili katika maeneo ya vijijini  kwa kutumia matunda kama maembe ,  mapapai na tungule ” Hii bishara sii tu inatupa kipato lakini inatusaidia  kuwa na uhuru wa kiuchumi” anasema Sabra.   

Amesema kuwa, matunda mengi yalikuwa yanapotea , lakini baada ya kupata elimu ya kusarifu tungule na matunda mengine yameongeza kipato” kwasasa  tungule moja ukiisarifu inaweza kukupa hadi elfu 3000 badala ya mia tano ikiwa haija sarifiwa” anasema Sabra.

   Asma Sadiki Hussein, mkaazi wa Kijiji cha Bungi na mwanachama katika kikundi cha kusarifu Matunda anasema,  usarifu wa matunda unachangia katika kuboresha  afya  za wanawake na familia zao, kwa kutengeneza bidhaa zenye virutubisho kutoka katika  matunda.

“Jamii nyingi za vijijini  zimeweza kubaini umuhimu wa kutumia matunda katika milo yao ya kila siku, hivyo kupunguza magonjwa yanayotokana na lishe duni” amesema Asma.

Amesema kuwa, wanawake wanaoshiriki katika usanifu wa matunda wanachangia katika uhifadhi wa mazingira ,kwani wanatumia mbinu za kienyeji za kutengeneza bidhaa na kukausha matunda , hii njia inasaidia kupunguza matumizi ya plastiki na kuongeza thamani ya matunda.

Nae, Salama Hussein mkaazi wa Shehia ya Unguja Ukuu amesema elimu ya kusarifu  matunda imewasaidia kupika bidhaa tofauti tofauti kwa lengo la kuyahifadhi matunda na kufanya biashara.

Amesema kuwa, ujuzi wa kusarifu matunda waliyoupata umewasaidia kuinua kipato chao,  ambapo hutengeneza biashara ndogo ndogo  na kuuza sokoni.

Zulfa Mbwana, ni Afisa mradi wa mabadiliko ya tabianchi kutoka  Community Forest  Pemba ( CFP) anasema wamewapa mafunzo ya usindikaji wa bidhaa za matunda wanawake kutoka  shehia  nne, ambazo ni Unguja Ukuu, Bungi , Uzi na Ng’ambwa kwa lengo la kuongeza thamani na kuinua kipato cha wakulima.

Amesema kuwa, wajasiriamali hao ambao ni wakulima viongozi wamepatiwa elimu ya uhifadhi  wa hesabu na usarifu wa mazao mbali mbali  ya ujasiriamali ili kukuza kipato chao na kuwa na uhuru wa kiuchumi” Mafunzo haya ya ujasiriamali ni kwa ajili ya kuongeza thamani za bidhaa za wakulima  na  utuzaji wa hesabu” anasema  Zulfa.

Mbarouk Omar Mussa  ni Mkurugenzi katika taasisi ya Community Forest Pemba anasema mradi wa ZANZ ADAPT umewawezesha wanawake kuhifadhi  na kusarifu bidhaa za matunda mbali mbali ili kuongeza thamani na kuongeza kipato kwa wajasiriamali wanawake.

Aidha amesema kuwa, usarifu wa matunda unatoa fursa nyingi kwa wanawake  katika jamii  ikiwemo uhifadhi wa mazingira,  kuboresha Maisha ya wanawake na jamii zao kwa ujumla.

Mradi wa ZANZ ADAPT unatekelezwa na taasisi ya Community Forest Pemba ( CFP) na Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar  -TAMWA ZNZ na kufadhiliwa na Community Forest Internation ( CFI ).

                      

 

 

No comments

Powered by Blogger.