UKATILI WA KIMTANDAO UNAVYORUDISHA NYUMA VIONGOZI WANAWAKE



  NA MARYAM NASSOR 

Azma ya kufikia usawa wa kijinsia  kwa karne ya 21 imekuwa ni ajenda  inayotiliwa mkazo kimataifa na kitaifa kuhakikisha  wanawake wanashiriki kikamilifu katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kisiasa.

Jitihada mbali mbali zinachukuliwa siku hadi siku za kuona kuleta usawa wa  kijinsia wa 50/50 katika nafasi za uongozi.

Hii ikijumuisha  idadi ya wanawake  974, 281  ambayo ni sawa na asilimia  51 ya wanaume ambao ni asilimia 49. Hii ni  kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makaazi ya mwaka 2022 kwa Zanzibar.

Licha ya wingi wao, wamekuwa wakikabiliwa na aina mbalimbali ya vikwazo.

Wanaharakati na watetezi wa haki za wanawake wanakiri kwamba mtandao ya kijamii imekuwa na mchango mkubwa katika kuwadhalilisha wanawake.

Asma Mohamed ni Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake Wilaya ya Kati Unguja,  ambae alishawahi kugombea nafasi mbali mbali za uongozi katika Chama cha Mapinduzi -CCM anakiri uwepo wa ukatili wa kimtandao kwa  viongozi wa kike.

"Hali hii imeshawapata viongozi wengi wanawake  wa kisiasa na kwa kweli  haifurahishi," anasema Asma.

Anasema kuwa, wakati akiwaita wandishi wa Habari kuzungumza nao au kuweka kitu mtandaoni, basi hutokea   baadhi ya watu utakuta wanazodoa kile alichoposti, “ lakini mimi huwa siyachukulii kwa uzito mkubwa hayo, kwani najua lengo langu nikufika mbali kisiasa," anasema Asma.

Anaongezea kusema kuwa wengine humtukana kupitia mitandao ya kijamii hasa kutokana na yeye kuwa kiongozi

"Yaani naonekana kama sifai kuweka kitu mtandaoni  si haki yangu  kuwa kwenye mitandao," anasema.

Hadi mwaka 2023 , takribani watu milioni  10.5 nchini Tanzania  wanatumia  mitandao ya kijamii, katika majukwaa maarufu kama vile  Facebook , Whatssap, Instagram na Tiktok ambayo yanatumia zaidi kwa  mawasiliano, burudani na Biashara ,Huku wanawake takribari  asilimia 40 -45 ambao ni  zaidi ya milioni  5  wanatumia internet  nchini Tanzania.

Kwa mujibu wa ripoti Maalumu ya Uchaguzi iliyotolewa na Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania kwa upande wa Zanzibar , inaeleza kuwa, nafasi ya uwakilishi  kwenye majimbo 50 ya Uchaguzi , wanawake ni asilimia 16  ambao ni wanane, wabunge wanao iwakilisha Zanzibar wanawake ni wanne, sawa na asilimia 8.

Mawaziri wanawake ni sita sawa na asilimia 33, makatibu wakuu ni saba sawa asilimia 39, kwa upande wa Wakuu wa Mikoa  mwanamke ni mmoja tu sawa na asilimia 20.

Tunu Juma Kondo ni Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania -  UWT wa Chama cha Mapinduzi CCM amesema janga la ukatili wa mitandao ya kijamii ni changamoto  ambayo, baadhi ya viongozi wanawake wa CCM wamekumbana nayo.

“Hii ni mbaya na inanyong'onyesha sana wanawake, wengine hurudi nyuma  kwa woga  kwani husemwa sana na kupewa sifa mbaya  na kuathiri nguvu ya uthubutu wa wanawake,” anasema Tunu.

Ukatili wa kimtandao dhidi ya viongozi wanawake  wa vyama vya siasa  ni tatizo linalo athiri  siasa na jamii kiujumla, kwani mara nyingi  hulenga kuharibu  sifa za viongozi hao, na hata kashfa zisizo ukweli.

Dk Mzuri Issa ni Mkurugenzi wa Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania -TAMWA ZNZ amesema ukatili wa kimtandao  unalenga wanawake ni miongoni mwa udhalilishaji  ambao umekuwa ukiwazuia baadhi ya wanawake kushiriki kikamilifu katika  siasa.

“Watu ni vyema washindane kwa hoja  na sio kudhalilishana  hususani katika majukwaa ya mitandao ya kijamii ,hali hii inawaumiza sana wanawake” anasema Dk Mzuri huku akiwataka viongozi wanawake waliopo kwenye siasa wasivunjike moyo na wasiogope kupigwa mitandaoni.

Sheria ya Uchaguzi ya Jamhuri ya Bunge na Madiwani inazungumza kuwa, ukatili wa wanawake ni uhalifu hivyo wakati umefika kuchukuliwa hatua muafaka kwa wale wanaowadhalilisha kwa kuwavunjia heshima na utu sambamba na vyombo husika kusimamia sheria za makosa ya mtandao hii itaondoa hofu kwa wanawake wanaofanya  ukatili huo.

Afisa Sheria kutoka Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa Tanzania kwa upande wa Zanzibar Abdul Razak  Said Ali, amesema uwepo wa Sheria inayosimamia  makosa ya mitandao  Tanzania  ya mwaka 2015 lengo ni  kuhakikisha ulinzi wa wanawake na unyanyasaji mitandaoni.

“Masuala yote kuhusiana na makosa ya kimtandao yanadhibitiwa na sheria hiyo, lengo ni kuwasaidia wanawake wanaopata haki zao pindi wakikumbana na ukatili kwenye mitandao” amesema.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania – TCRA Jabir Bakari amesema mamlaka hiyo inaendeleza kutoa elimu ya masuala ya kidigitali na usalama mitandaoni kwa kuhakikisha mazingira salama na imara  ya matumizi bora ya mitandao.

“Ingawaje mipango ya kuengeza  uelewa wa umma ni ajenda ya kudumu ya TCRA ,kampeni hii inatokana na umuhimu wa kipekee kuwapatia  watanzania mbinu za kujilinda dhidi ya mashambulio ya mitandao ya internet na simu niwaombe hii pia ni kujilinda dhidi ya uhalifu mtandao” 

Ameyasema hayo, Dar es Salamu wakati wa uzinduziwa kampeni ya ‘Ni Rahisi Sana” inayolenga kuelimisha wananchi kwamba mazingira salama mitandaoni.

Mwanaharakati kutoka vugu vugu la ukombozi wa mwanamke Duniani kwa Tanzania, Rahima Mussa Hassan amesema kuwa ukatili wa kimtandao   umekithiri na unaathiri viongozi wanawake kwa  kiasi kikubwa na madhara yake ni makubwa.

“Matusi, dharau na maneno yasiyo na staha ni mengi kwa wanawake kwenye mitandao ya kijamii hususani kwa wanawake waliopo kwenye siasa” amesema Rahima  huku akisisitiza  kuwa, lengo la vugu vugu wa ukombozi wa mwanamke ni kukata mizizi inayokwamisha  mwanamke kutofikia ndoto zake.

                       MWISHO

  

  

 

No comments

Powered by Blogger.